RC SINGIDA AAGIZA ZANAHATI IPEWE WAHUDUMU WENYE SIFA

 
Na Nathaniel Limu, Singida
MKUU wa Mkoa wa Singida, Dk. Parseko Kone, amemwagiza Mkuu wa Wilaya ya Iramba ashirikiane na mkurugenzi mtendaji wa halmashauri kuhakikisha Zahanati ya Kitongoji cha Kipamba iliyopo Kata ya Mwangeza inakuwa na wahudumu wenye sifa mapema iwezekanavyo.

Agizo hilo lilitolewa mjini hapa juzi baada ya kulalamikiwa na wakazi wa Kitongoji cha Kipemba kwamba zahanati yao toka imalizike kujengwa zaidi ya mwaka moja haina muhudumu mwenye taaluma.

Imedaiwa kuwa kwa kipindi chote hicho, kuna vijana wawili wenye elimu ya msingi na ambao hawajasomea taaluma ya utoaji huduma ya afya ndio wanaotoa huduma.

“Haingii akilini zahanati ambayo imejengwa kwa msaada na Shirika la International Outreach Africa la nchini Marekani, imebaki bila mhudumu wa afya mwenye sifa stahiki. Wafadhili hawa wakija leo, hivi watatuelewaje,” alihoji Dk. Kone.

Kutokana na hali hiyo, aliagiza wahudumu wenye sifa stahiki, wapangwe haraka iwezekanavyo katika zahanati hiyo.

Kuhusu malalamiko ya ukosefu wa vitanda katika mabweni mawili ya Shule ya Msingi ya Munguli, aliagiza taratibu zifanywe haraka na hatimaye mabweni hayo yawe na vitanda vyitakavyokidhi mahitaji.

Baadhi ya wakazi wa Kitongoji cha Kipamba, wamedai kero zao nyingi hazipatiwi ufumbuzi wa kudumu kwa madai Mbunge wao, Salome Mwabu, hajawatembelea toka amechaguliwa kushika wadhifa huo.
Chanzo: Mtanzania

Wanahabari Watakiwa Kufuata Maadili Ya Uandishi Kuepuka Migogoro




MWENYEKIT wa Klabu ya wanahabari mkoa Singida SINGPRESS) Seif Takaza akizungumza kabla ya kumkaribisha Yahaya Nawanda, mkuu wa wilaya ya Iramba kufungua mkutano maalum wa kufanyia marekebesho KATIBA ya klabu hiyo(kushoto ni kuu huyo wa Wilaya).
Mkuu wa Wilaya ya Iramba Yahaya Nawanda, akifungua mkutano maalum wa klabu ya waandishi wa habari Mkoa Singida(Singpress) ulioandaliwa kwa ajili ya kuifanyia marekebisho katiba ya klabu,kuanzia kulia ni makamu Mwenyekiti wa Singpress, Jumbe Ismaely, anayefuata ni mwenyekiti wa Singpress Seif Takaza.



Mkuu wa wilaya Iramba Yahaya Nawanda (wa pili kulia - mwenye miwani),akiwa katika picha ya pamoja na wanahabari wa mkoa Singida, muda mfupi baada ya kufungua mkutano maalumu wa Katiba ya Singpress.





Na: Elisante John, Singida



Mkuu wa Wilaya Iramba Mkoani Singida, Yahaya Nawanda, ametoa wito huo alipofungua mkutano mkutano maalumu wa Katiba ya Klabu ya wanahabari mkoa Singida (SINGPRESS), uliofanyika ukumbi wa halmashauri, mjini Kiomboi.



Alisema kuna faida nyingi kwa kutii na kuzingatia katiba watakayoifanyia marekebesho, mojawapo ikiwa ni kuimarisha amani na utulivu ndani ya kikundi, nchi au sehemu yoyote ile kwa watu walioamua kushirikiana pamoja.




Pia alihimiza wanahabari hao waende sawa na mabadiliko yatakayofanyika ili kujenga umoja na upendo miongoni mwao na wadau wengine wa habari Mkoani Singida.




Aliwataka wasiingize ushabiki katika utendaji wao wa kazi za kila siku, kuepusha tasnia ya habari kuonekana kazi isiyofaa katika jamii.


WAHADZABE MKOANI SINGIDA WABAKIA NYUMBANI KUHESABIWA BAADA YA KUPEWA NYAMAPORI.




Mkuu mkoa wa Singida, Dk.Parseko Kone akimkabidhi boksi la chakula cha msaada mwenyekiti wa kitongoji cha Kipamba, Agostino (mwenye shati jeupe).Chakula hicho kimetolewa ili jamii hiyo isiende porini kuwinda ibaki kwenye kaya zao kuhesabiwa.(Picha na Nathaniel Limu).
Na Nathaniel Limu.
Jamii ya Kihadzabe inayoishi katika kijiji cha Munguli kata ya Mwangeza jimbo la Iramba mashariki, imejitokeza kwa wingi kushiriki sensa ya watu na makazi iliyoanza Agosti 26 mwaka huu.
Jamii hiyo ilijitokeza baada ya ‘kupewa motisha ya msaada wa nyamapori ya kutosha na vyakula mbalimbali.
Jamii hiyo iliiomba serikali ya mkoa wa Singida nyamapori ya kutosha ili isiende porini kuwinda wakati wa sensa.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Parseko Kone, amesema jamii hiyo ambayo chakula chake kikuu ni nyamapori, matunda pori, asali na mizizi ya miti pori, kabla ya kuanza kuhesabiwa, iligawiwa nyama ya nyumbu wakubwa watatu na nusu na mbuzi mmoja.
Amesema kitendo hicho kilisababisha jamii hiyo isiende kuwinda porini kama kawaida yao, ilibaki kwenye kaya zao kusubiri makarani wa sensa.
Mkuu huyo wa mkoa ameongeza kusema kuwa iliwalazimu kuwakubalia ombi lao la msaada wa chakula na nyama pori ili wabaki kwenye kaya  na kambi zao, ili waweze kuhesabiwa.
Jamii hii ilibaki kwenye kaya zao na ilijibu kwa ufasaha mkubwa maswali yote iliyokuwa ikiulizwa na makarani.
Hata hivyo, kulijitokeza tatizo dogo la mawasiliano, kwa maana ya kuwa baadhi ya Wahadzabe hawajui kuongea Kiswahili, kwa hiyo walitafutwa wakalimani na walifanya kazi vizuri ya kutafsiri na hapo madodoso yalijibiwa ipasavyo.
Dk.Kone alisema pamoja na nyamapori hiyo, pia walitoa msaada wa magunia mawili ya unga wa mahindi na tani moja ya chakula kilichotolewa msaada na shirika lisilo la kiserikali la Outreach International Africa lenye makazi yake nchini Marekani.
Katika hatua nyingine, mkuu huyo wa mkoa amesema kuwa katika sehemu zingine za mkoa, mambo yamekwenda vizuri mno.
Kulikuwepo na mapungufu madogo madogo nayo yalirekebishwa bila kuleta athari yo yote.
Dkt. Kone ametumia fursa hiyo kuwashukuru wakazi wa mkoa wa Singida kwa kujitokeza kwa wingi na kutoa ushirikiano wa dhati kwa makarani wa sensa.

HAYA NDIO MAISHA BORA KWA KILA MTANZANIA MIONGONI MWA JAMII YA WAHADZABE MKOANI SINGIDA.


Mkazi wa kitongoji cha Kipamba kata ya Mwangeza ambaye amekataa kutaja jina lake akiwa kwenye nyumba yake ya kuishi na familia yake.  
 Mkazi wa kitongoji cha Kipamba kata ya Mwangeza wilaya ya Iramba ambaye hakuweza kujulikana jina lake mara moja akiomba alipwe fedha za kumpiga picha. 
(Picha na Nathaniel Limu).

MTENDAJI WA KIJIJI AFUNGWA KWA KUOMBA RUSHWA

 
Na Petro Sungi, Singida
AFISA mtendaji wa Kijiji cha Misuke kilichopo katika Wilaya ya Singida, Omary Mandi amehukumiwa kwenda jela miaka mitatu, baada ya kukutwa na hatia ya kuomba na kupokea rushwa.

Hukumu hiyo ilitolewa Agosti 21, mwaka huu na Hakimu Mkazi wa Mahakama mkoani hapa, Ruth Massam mbele ya Ofisa Uchunguzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa mkoani hapa (TAKUKURU), Wilson Ntiro.

Katika hukumu hiyo mtuhumiwa alikutwa na hatia ya kuomba na kupokea rushwa mara mbili na kuhukumiwa kwenda jela miaka mitatu.

Awali Ofisa wa TAKUKURU alidai kuwa mtuhumiwa huyo alitenda makosa hayo Novemba 17, 2010 kwa kupokea rushwa ya Sh 40, 000 wakati Novemba 10 alipokea rushwa ya Sh 75, 000 kutoka kwa Mwenyekiti wa Misuke, Joseph Dwash.

Mtendaji huyo alidaiwa kuwa alimdanganya Dwash kuwa anaweza kumsaidia, ili aendelee kuwa mwenyekiti. Kesi hiyo ilifunguliwa Januari 31, mwaka huu na TAKUKURU.
Chanzo: Mtanzania

RC KONE AWATAKA WALIOVAMIA PORI LA WAHADZABE KUONDOKA


Mwandishi wetu, Singida Yetu 
SERIKALI imewataka watu waliovamia pori wanaloishi wananchi wa kabila la wahadzabe mkoani Singida kuondoka mara moja kabla hatua za kisheria hazijachukuliwa dhidi yao.
Pori  hilo lililopo katika Kijiji  cha Munguli wilaya  Mkalama umbali wa kilomita 120  kaskazini mashariki mwa mji wa Singida, limevamiwa na wahamiaji  kutoka Arusha, Manyara na  Shinyanga  ambao wamefyeka na kuchoma  moto kwa ajili ya  kilimo na ufugaji.
                                                                                 
Akizungumza  baada ya kuwatembelea wananchi  hao  maarufu kama watindiga Mkuu wa Mkoa wa Singida Dokta Parseko Kone amesema serikali haiwezi kuvumilia  kuona uharibifu wa mazingira ukiendelea katika pori hilo lililotengwa na kuhifadhiwa kwa mujibu wa sheria.

Dokta Kone amemwagiza mkuu wa wilaya ya Mkalama na mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, kuwaondoa wavamizi hao kwa nguvu iwapo hawataondoka kwa hiari yao.


Mbali na wavamizi, pori hilo linakaliwa na wahadzabe zaidi 400  ambao hujishughulisha na  uwindaji na kula vyakula  vya  asili ambavyo ni nyama pori, asali, matunda pori na mizizi
Blogzamikoa

Picha Mbalimbali Za Katibu Mkuu wa Chadema Dk Wilbrod Slaa Kwenye Mkutano wa Kuwashukuru Wananchi wa Jimbo la igunga

  Katibu
Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod
Slaa, akisalimiana na aliyekuwa mgombea wa ubunge jimbo la Igunga katika
uchaguzi mdogo mwaka jana, kupitia Chadema, Mwalimu Joseph Kashindye,
walipokutana katika mkutano wa kuwashukuru wananchi wa jimbo hilo kwa
ushiriki wao katika kesi ya uchaguzi wa jimbo hilo, ambayo Chadema
kiliibuka mshindi, uliofanytika kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Igunga
 Katibu
Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa
akikumbatinana na Mbunge wa Maswa Mashariki, Slyvester Kasulumbai,
walipokutana katika mkutano wa hadhara wa kuwashukuru wananchi wa jimbo
la Igunga kwa ushiriki wao katika kesi ya uchaguzi wa jimbo hilo, kwenye
Uwanja wa Sokoine mjini Igunga juzi.
Kutokana
na kilichoelezwa kuwekwa kwa lami chini yakiwango katika mlima Sekenke
mkoani Singida, imeharibika vibaya kama inavyoonyesha pichani magari
yakipita kwa shida baada ya lami hiyo kubomoka kwa kipindi kifupi tangu
iwekwe, kama ilivyokutwa jana.Picha na Joseph Senga

Katibu Mkuu wa Chadema,Dk. Willibrod Slaa Aung'uruma igunga



 Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod
Slaa akiwahutubia wananchi wa mji wa Igunga na vitongoji vyake, katika
mkutano wa hadhara wa kuwashukuru wananchi kwa ushiriki wao katika
kufanikisha kesi ya uchaguzi wa jimbo hilo, uliofanyika kwenye Uwanja wa
Kumbukumbu ya Sokoine mjini Igunga.
 Aliyekuwa mgombea wa jimbo la Igunga
katika uchaguzi mdogo mwaka jana, kupitia Chadema, mwalimu Joseph
Kashindye na aliyekuwa meneja wa kampeni,  Slyvester Kasulumbai,
wakiwasili kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine mjini  Igunga, ambako
kulifanyika mkutano wa hadhara.Picha zote na Joseph Senga)


NYAMAPORI KUTUMIKA KUIHAMASISHA JAMII YA WAHADZABE KUSHIRIKI SENSA YA WATU NA MAKAZI.

Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt.Parseko Kone (mwenye suti ya bluu) akisalimiana na mzee wa Kihadzabe mkazi wa kijiji cha Munguli kitongoji cha Kipamba ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja.
Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Parseko Kone akihamasisha jamii ya Kihadzabe wa kitongoji cha Kipamba kushiriki sensa ya taifa inayotarajiwa kufanyika nchini kote Agosti 26 mwaka huu.
Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Parseko Kone (mwenye suti ya bluu)akimkabidhi msaada wa chakula Mwenyekiti wa kitongoji cha Kipamba kijiji cha Munguli Edward Mashimba (mwenye shati jeupe).
Maboksi ya msaada wa chakula kilichotolewa na shirika lisilo la kiserikali la International Outreach International na nchini Marekani. Chakula hicho kina uzito wa zaidi ya tani moja.
Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Parseko Kone, akiwa amempakata mtoto wa Kihadzabe aliyebatizwa jina lake la Kone. Mtoto huyo alizaliwa asubuhi ya siku Dkt. Kone alipofanya ziara ya kwanza ya kikazi katika kijiji hicho miaka sita iliyopita. Nyuma ya mtoto huy ni Mkuu wa wilaya ya Singida Mwalimu Queen Mlozi.
Baadhi ya akina mama wa Kihadazbe waliohudhuria mkutano wa hadhara ambao mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Parseko Kone, aliutumia kuhamasisha jamii ya Kihadzabe na nyingine kushiriki sensa inayaotarajiwa kufanyika Agosti 26 mwaka huu. (Picha zote na Nathaniel Limu).
Na.Nathaniel Limu.
Serikali ya wilaya mpya  ya Mkalama mkoani SIngida imeahidi kutoa nyama pori ya kutosha kwa Wahadzabe wa kitongoji cha Kipamba kata ya Mwangeza, ili waweze kushiriki sensa ya kitaifa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika nchini kote Agosti 26 mwaka huu.
Kwa mujibu wa mkuu wa wilaya hiyo Edward Ole Lenga, msaada wa nyama ya wanyama pori hiyo, utasaidia jamii ya Wahdzabe kubaki kwenye kaya zao kipindi chote cha sensa.
Akizungumza muda mfupi kabla ya kumkaribisha mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Parseko Kone, awahamasishe Wahadzabe na wakazi wengine wa kata ya Munguli, kushiriki sensa.
Lenga amesema msaada huo wa  nyama pori, unatokana na ombi liliotolewa na jamii hiyo ambayo chakula chake kikuu ni nyamapori, mizizi, matunda pori na asali.
Akifafanua amesema Wahdzabe hao wanaokadiriwa kufikia 227, wametoa ombi hilo ili wakati wote wa sensa wasiende porini kuwinda na badala yake wabaki kwenye kaya zao wakisubiri kuhesabiwa.
Mkuu huyo wa wilaya amesema ombi hilo tayari limeshakubaliwa na maandalizi yote muhimu ya kuwinda wanyama pori siku moja kabla ya siku ya sensa, yamekwisha kamilika.
Kwa upande wake mkuu wa mkoa Dkt. Kone, ametoa msaada wa chakula chenye uzito wa zaidi ya tani moja, ambacho kitakidhi mahitaji kuanzia sasa hadi zoezi la sensa litakapokamilika.
Amesema kwa hali hiyo, kipindi chote cha sensa, hapatakuwepo na haja kwenda porini kutafuta wanyama pori, asali, matunda pori au mizizi.
Katika hatua nyingine, amewataka wahakikishe kila mmoja anahesabiwa mara moja tu, kwa madai kuwa wakishafahamika idadi yao na hali zao za maisha, itasaidia serikali kujipanga namna bora  ya kuwahudumia na kuwaletea maendeleo.
Wakati huo huo Dk. Kone, amesema pamoja na kunid la wawindaji, pia makundi mengine ya wavuvi, wachungaji wanaohama hama, watafutaji madini na baadhi ya wakulima ambao wana mashamba yaliyo mbali na makazi au makambi yao ya kawaida, warejee kwenye kaya na makambi yao ili waweze kuhesabiwa siku ya sensa.

DIALLO, GUNINITA WACHUKUA FOMU CCM



Na Waandishi Wetu, Dar na mikoani


*Wana CCM wamuonya Lembeli Shinyanga
MCHUANO mkali wa kuwania nafasi za wenyeviti wa CCM wa Mikoa, Tanzania Bara, umeanza.

Katika mchuano huo, baadhi ya vigogo wa CCM katika mikoa mbalimbali wameanza kuchukua fomu ili kutetea nafasi zao na wengine kuwang’oa wenzao walioko madarakani.

Katika Mkoa wa Mwanza, Mbunge wa zamani wa Ilemela, Anthony Diallo (CCM), jana alichukua fomu kugombea nafasi ya Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Mwanza.

Wakati Diallo alichukua fomu mkoani humo, Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Dar es Salaam, John Guninita, naye alichukua fomu ili kutetea nafasi yake hiyo.

Wakati hayo yakiendelea, mkoani Shinyanga nako mchuano mkali unatarajia kuwa kati ya Mbunge wa Kahama, James Lembeli (CCM) na Mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Shinyanga, John Mgeja.

Katika Mkoa wa Mwanza, Diallo, ambaye pia ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, (NEC), alichukua fomu hiyo jana saa mbili asubuhi na alikabidhiwa na Katibu Msaidizi wa CCM, Mkoa wa Mwanza, Zubeda Mbaruku, katika makao makuu ya CCM, Mkoa wa Mwanza.

Akizungumza baada ya kuchukua fomu hiyo, Diallo alisema amechukua fomu hiyo kama sehemu ya kutimiza wajibu wake wa kidemokrasia na aliahidi kuwatumikia kikamilifu wana CCM, Mkoa wa Mwanza.

"Mimi ni kiongozi wa watu, naijua CCM, kwa hiyo, nitakaposhinda, nitahakikisha nawaunganisha wana CCM wote bila kubagua na nitapambana na ubaguzi pamoja na makundi ndani ya chama chetu, ili kukifanya kiendelee kuaminika kwa wanachama na wananchi wa kawaida," alisema Diallo.

Wakati Diallo akichukua fomu, Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Mwanza anayemaliza muda wake, Clement Mabina, naye alichukua fomu ili kutetea nafasi yake hiyo.

Mbunge wa Kwimba, Shanif Hiran Mansoor (CCM), yeye alichukua fomu ili kutetea nafasi yake ya Mweka Hazina wa chama hicho, Mkoa wa Mwanza kwa kipindi kingine cha miaka mitano.

Wakati mchuano ukiwa hivyo jijini Mwanza, jijini Dar es Salaam nako mchuano umeanza, baada ya Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Dar es Salaam, John Guninita, kuchukua fomu ya kutetea nafasi yake hiyo jana.

Guninita alikabidhiwa fomu hiyo jana na Katibu wa CCM, Mkoa wa Dar es Salaam, Abilahi Mihewa, makao makuu ya chama hicho, Mkoa wa Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa kuchukua fomu hiyo, Guninita alisema akifanikiwa kuendelea na nafasi hiyo, atajenga uchumi wa kisasa na kiusalama kupitia miradi mbalimbali ya chama hicho.

Alisema pia kwamba, anatarajia pia kujenga mazingira ya kukuza uchumi kwa kuimarisha miradi yote ya chama.

Pia alijigamba kwamba, katika kipindi cha miaka mitano alichokuwa madarakani kwa kushirikiana na viongozi wenzake mkoani Dar es Salaam, amefanikiwa kutambua mali zote za chama, vikiwemo viwanja 300 na kwamba kati ya viwanja hivyo, 150 vimepata hati kwa ajili ya kupata uwekezaji unaoeleweka.

“Nimekuwa mwenyekiti kwa miaka mitano, nimejipima na kuona naweza kuwaongoza wana CCM katika kipindi kingine, ninawaomba na wanachama wapime uwezo wangu kama ninafaa tena kuonyesha uwezo wangu.

“Kikubwa tunachotaka ni kuhakikisha tunajenga uchumi wa kisasa na kiusalama kwa mali za CCM, vikiwemo viwanja.

Kuhusu changamoto za vyama vya upinzani, kikiwamo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ambacho kinaaminika kuungwa mkono zaidi na vijana, alisema:

“Kigezo cha chama chochote cha siasa kukubalika ni ushindi katika chaguzi zinazoshirikisha vyama vyote, kwa hiyo, CCM bado tuko juu, maana katika majimbo ya Dar es Salaam, tuliweza kushinda viti sita kati ya vinane, udiwani tulifanikiwa kuchukua kata 77 kati ya 90, sasa kwa nini tusiseme bado tunakubalika?” alihoji Guninita.

Kwa upande wake, Mihewa aliwaonya wana CCM wanaoomba nafasi za kugombea katika Mkoa wa Dar es Salaam, wahakikishe wanafuata sheria na kanuni zilizowekwa na chama chao.

“Nawasihi wagombea wote wasifanye kampeni za aina yoyote, wasubiri mpaka siku ya uchaguzi, ni marufuku kukutana, kuwakusanya wapiga kura na kuwasalimia, wasubiri siku yenyewe watakapokutana na wajumbe, atakayebainika akikiuka taratibu, ajue vikao vitamwengua mara moja” alionya Mihewa.

Wakati Dar es Salaam na Mwanza mchuano ukianza, mvutano mkali unatarajiwa pia mkoani Shinyanga, ambako Mbunge wa Kahama, James Lembeli (CCM), anatarajia kupambana na Mwenyekiti wa CCM, Mkoa huo, Khamis Mgeja, ingawa hadi sasa hakuna aliyechukua fomu kuwania nafasi hiyo.

Baada ya Lembeli kutangaza hivi karibuni, kwamba atamng’oa madarakani Mgeja, baadhi ya viongozi wa chama hicho mkoani humo ambao pia ni wajumbe wa mkutano mkuu wa CCM, Mkoa wa Shinyanga, wamemuonya mbunge huyo na kumtaka asiingilie uhuru wa wajumbe wa mkutano mkuu, kwa kuwa ndiyo wenye uwezo wa kuwang’oa viongozi wa ngazi ya mkoa.

Wakizungumza na MTANZANIA kwa nyakati tofauti mjini hapa jana, wajumbe hao wamesema kitendo cha Lembeli kusema atamng’oa Mgeja hakiwezi kukubalika, kwa kuwa wajumbe wa mkutano mkuu ndiyo wenye uwezo wa kuwaondoa viongozi wao madarakani.

Mmoja wa wajumbe wa mkutano mkuu wa chama hicho, Mkoa wa Shinyanga, Charles Shigino, alisema yeye na wenzake hawawezi kukaa kimya kwa kuwa kauli ya Lembeli inaonyesha anataka kuwachagulia kiongozi anayetakiwa kukiongoza chama hicho mkoani hapa.

“Kwa ujumla wajumbe wa mkutano mkuu hawakutegemea kusikia kauli hiyo kutoka kwa Lembeli, kwa sababu kauli hiyo inaingilia uhuru wa wajumbe wa mkutano mkuu wa CCM mkoa wa Shinyanga.

“Suala la kupigiwa kura na kushindwa au kushinda siyo kazi ya mgombea, hiyo ni kazi ya wapiga kura ambao ni wajumbe, wala siyo Lembeli.

“Sasa sisi kama wajumbe, tunamuonya Lembeli aache tabia ya kujitangaza eti anakuja kugombea nafasi ya Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Shinyanga kwa lengo la kumng’oa kigogo, hivi anataka kumng’oa kigogo huyo kwa umuhimu gani alionao?

“Haya majigambo hayana tija kwa sababu wapiga kura ndio wenye uamuzi na wenye mamlaka ya kumpa nafasi hiyo, sasa kwa kauli yake hiyo, ina maana Lembeli tayari ndiye Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Shinyanga.

“Lembeli ni Mwanachama wa CCM na ni Mbunge wa Kahama, kwa hiyo, ni vema kwanza ajue wazi kuwa hana uwezo wa kumng’oa kiongozi, kwani kazi hiyo ni ya wajumbe na wapiga kura tu na si vinginevyo, hivi ameshaongea na kila mjumbe na kumhakikishia kwamba atampa kura za kumng’oa kigogo huyo anayemtaja?

“Namuomba ndugu yangu Lembeli pamoja na wagombea wengine katika mkoa huu wa Shinyanga, waanze kuweka maji kichwani na kusubiri kunyolewa na wapiga kura ambao ni wajumbe na siyo Lembeli,” alisema Shingino.

Mbali na kiongozi huyo, mwingine aliyekerwa na kauli ya Lembeli ni Mwenyekiti wa CCM, Kata ya Shinyanga Mjini ambaye pia ni Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM mkoani hapa, Rajabu Makubuli, aliyesema Lembeli anahitaji msaada ili ajue namna mchakato wa uchaguzi unavyokwenda.

“Huyu jamaa ni mbunge, lakini inaonekana hajui taratibu za uchaguzi zinavyokwenda, kwa hiyo, nadhani kuna kila sababu ya kumweleza namna uchaguzi unavyofanyika, ingawa kwa kauli zale hizo wajumbe sasa wameshaanza kumjua tabia yake,” alisema Makubuli.

Naye Peter Lubinza ambaye pia ni Mjumbe wa CCM, Mkoa wa Shinyanga, alisema Lembeli alikosea kukaririwa na vyombo vya habari, akitamba kuwa atahakikisha anamng’oa Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Shinyanga.

“Kutokana na kauli yake anapaswa kutambua kuwa CCM na hasa wajumbe hivi sasa ni waelewa sana, wanajua kuchagua pumba na mchele” alisema.

“Yeye angekuja na hoja ya kujenga chama, hasa wakati huu ambao kinakabiliwa na changamoto nyingi za kisiasa, ikiwemo ya ushindani unaokikabili, badala yake anakuja na porojo zake kwamba anakuja kumng’oa kigogo, ngoja tumsubiri aje,” alisema Lubinza.

Chanzo: Mtanzania
 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa