Home » » MFUGAJI ATISHIA KUMBURUZA MAHAKAMANI DIWANI

MFUGAJI ATISHIA KUMBURUZA MAHAKAMANI DIWANI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

MFUGAJI na mkulima wa Kijiji cha Ufana, Kata ya Mgungira, Tarafa ya Sepuka, wilayani hapa mkoani Singida, Sawaka Kujelwa, ametishia kuwafungulia mashtaka mahakamani viongozi wawili wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kata hiyo kwa madai ya kuuza zaidi ya ekari 500 anazozitegemea kwa ajili ya makazi, kilimo na malisho.
Kujelwa, aliwataja viongozi hao kuwa ni Mwenyekiti wa CCM wa Kata, Nhende Shija na Diwani Mussa Ng’imba, ambao alidai waliamua kuvamia maeneo yake baada ya yeye kuugua ugonjwa wa kushindwa kwenda haja ndogo, Desemba 21, 2009.
Alisema baada ya kuugua ndipo alilazimika kwenda kwenye matibabu ambako alipita hospitali ya misheni ya Mtakatifu Gasper mjini Itigi, Makiungu, Puma na hatimaye hospitali ya Rufaa ya KCMC Moshi, mkoani Kilimanjaro mwaka 2010 alikopona.
“Baada ya kupata matibabu KCMC, madaktari walinishauri kukaa karibu na hospitali hiyo kwa uchunguzi zaidi, ambapo nilikaa hadi mwaka 2012 ndipo niliporudi nyumbani, lakini nikilazimika kufuata masharti ya madaktari ya kutofanya kazi ngumu,” alisema.
Aliongeza kuwa wakati akiwa kwenye matibabu Moshi KCMC, ndipo diwani kwa kushirikiana na mwenyekiti wa chama wa kata, walipoanza kuyavamia maeneo yake aliyokuwa akiyategemea kwa kilimo na malisho ya mifugo, na mwaka jana wakati anaendelea na mapumziko ya matibabu, watu walizidi kuvamia.
Alisema kuwa baada ya kuona hali hiyo, aliandika barua kwa Kaimu Ofisa Mtendaji wa Kijiji hicho, kumjulisha, lakini bila mafanikio na ndipo mwaka jana alimwandikia mwenyekiti wa kijiji kumfahamisha juu ya uvamizi huo.
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Matinje, Elius Milekwa na Mwenyekiti wa Kijiji cha Ufana, Machiya Nyorobi, walipotakiwa kuzungumzia malalamiko hayo, walikiri eneo lililovamiwa ni la Kujelwa na kwamba wanaoendesha shughuli za kilimo na malisho kwa sasa ni wavamizi na hawataki kuyaachia.
Mwenyekiti wa CCM Kata ya Mgungira, Nhende Shija alipoulizwa sababu za kuvamia maeneo hayo, alidai hakuvamia bali ni mali yake.
Diwani Ng’imba alisema kuwa, malalamiko hayo hayana ukweli wowote ila ni mali yake na mwenyekiti huyo, na kwamba Sawaka ni tapeli tu.
 Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa