Home » » MGIMWA AONYA MAAFISA MISITU

MGIMWA AONYA MAAFISA MISITU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
NAIBU Waziri wa Maliasili na Utalii, Mahmood Mgimwa amewatahadharisha baadhi ya wafanyakazi waliopewa dhamana ya kusimamia rasilimali za misitu kutokuwa kichocheo cha uharibifu wa misitu kutokana na kutowajibika ipasavyo pamoja na kufanyakazi kinyume cha maadili.
Mgimwa alitoa tahadhari hiyo wakati wa ufunguzi wa mkutano mkuu wa mwaka wa siku tatu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), uliofanyika mjini Singida.
“Katika mikakati hii hatutegemei kuona wafanyakazi waliopewa dhamana ya kusimamia rasilimali hizi, wanakuwa kichocheo cha uharibifu wa misitu yaani kunakotokana na kutowajibika ipasavyo na kufanyakazi kinyume cha maadili,”alisisitiza.
Alifafanua kuwa ni jukumu la wataalamu wote kutekeleza mipango kazi inayoanishwa katika mikakati yao ya kuongoza na kuendeleza rasilimali za misitu na nyuki.
Kwa mujibu wa Naibu waziri huyo, TFS kwa niaba ya serikali ya Tanzania anatakiwa ajipambanue kwa kufanya kila linalowezekana katika kulinda rasilimali za misitu zilizopo na kuziendeleza kwa kuongeza maeneo zaidi ya misitu.
Naye Mtendaji Mkuu wa TFS, Juma Mugoo alisema katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha wa 2010/2011 hadi 2013/2014, wameweza kutengeneza na kusambaza mizinga ya nyuki ipatayo 19,570 katika vituo vya wakala mizinga 5,729 na vijiji vilivyoko kando ya misitu ya Hifadhi mizinga 13,841.
Hata hivyo, Mugoo aliweka bayana kwamba vituo vya ufugaji nyuki vya Nyandakame Kondoa, Ukimbu Manyoni, Buha Kibondo na Mwambao wa Handeni vimewezeshwa kuwa vituo vya uzalishaji badala ya ilivyokuwa mwanzo kama vituo vya maonesho.
“Kiasi cha tani zaidi ya 7.6 za asali na kilo 458.5 za nta zilizalishwa na kuuzwa,vile vile wakala imeanzisha manzuki mpya 51 katika kanda za Kusini, Kaskazini, Mashariki, Kati na katika mashamba saba ya miti,”alisema.
Raisi wa Chama cha Wataalamu wa Misitu Tanzania (TAF), Prof. Reuben Mwamakimbullah alisema kwa kiasi kikubwa hali ya misitu nchini inasikitisha licha ya kuwepo wataalamu wanaolipwa kwa ajili ya kusimamia sekta hiyo. 
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa