Home » » TUSIKUBALI KAMWE KUGEUZWA KARAI LA ZEGE 2015

TUSIKUBALI KAMWE KUGEUZWA KARAI LA ZEGE 2015

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 
Hakuna ubishi waandishi wa habari wana nafasi kubwa sana ya kuipatia jamii viongozi bora na sio bora viongozi, kama wataweka mbele uzalendo na kuacha kuchukua hongo kutoka kwa wagombea kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Nafahamu wapo waandishi wengi wenye uadilifu, lakini kwa sababu kwenye msafara wa mamba na kenge wamo, si ajabu kukuta ambao njaa yao ya muda mfupi inatupatia viongozi wabovu.
Kipindi cha uchaguzi ni wakati ambapo baadhi yetu tunajulikana thamani zetu. Wapo wa Sh20,000, wengine Sh50,000, pia wa Sh100,000 na wale wanaopewa hongo zaidi ya kiasi hicho.
Hongo hizi wanazopokea ili kumpamba mgombea kuliko uhalisia wake, zimekuwa na athari kubwa kiuchumi, kisiasa na kijamii ikiwamo kupata viongozi wasiofaa na wanaotanguliza masilahi yao binafsi mbele.
Sote tunafahamu Uchaguzi Mkuu wa 2005 na 2010 namna ambavyo tuliwapamba baadhi ya wagombea wakiwamo wa ubunge, tukawaaminisha wapigakura wakawachagua, lakini leo wanajuta. Natamani utaratibu ule wa zamani urejee, kwamba kama wananchi walikuwa na hitaji la kiongozi walimtafuta wenyewe na kumuomba ili agombee, leo mtu anagombea tena kwa kuhonga wapigakura.
Mwaka huu huenda tukawa na uchaguzi wa Serikali za mitaa, lakini mwakani tukawa na uchaguzi mkuu wa Rais, wabunge na madiwani watakaotuongoza kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.
Ni kipindi ambacho thamani ya waandishi wa habari hupanda kwa kipindi kifupi sana na kisha wanasiasa wakishaingia madarakani, huwatelekeza kama mafundi wanavyotumia karai la zege.
Nafahamu asilimia 75 ya wanahabari wote nchini ni wa kujitegemea ambao kimsingi wanalipwa kulingana na habari ama makala zitakazochapwa au kutangazwa na vyombo vya habari.
Ni ukweli malipo haya ni kidogo, lakini hiyo haiwezi kuhalalisha baadhi yetu kujiingiza katika vitendo vya kupokea hongo kutoka kwa wagombea ili tu wawaandike vizuri hata kama hawafai.
Maadili ya Uchaguzi Mkuu 2010 kwa wanahabari yaliweka sharti la lazima kwa wanahabari kuwahabarisha na kutoa elimu ya uraia kwa wapigakura ili wafanye uamuzi sahihi wakati wa kupiga kura.
Uamuzi sahihi ni kwa wapigakura kuchagua viongozi bora na siyo bora viongozi kwa sababu tu amepandishwa chati na wanahabari wakati dhamira yake ni kwenda kuchuma na si kusaidia jamii.
Wakati tunajiandaa na chaguzi nilizozisema, tayari wapo wagombea ambao wamekuwa ‘mzigo’ lakini wanajiandaa kufanya kila njia ili waweze kurudi tena bungeni kwa kipindi kingine.
Kuna taarifa zisizo rasmi baadhi yao wametenga hadi Sh200 milioni na sehemu ya fedha hizo imetengwa kwa ajili ya wanahabari wasioheshimu maadili ili wawasafishie njia hata kama hawafai.
Wanahabari tunapaswa kuanza kujitafakari sasa kama tumefanya nini kulisaidia taifa kupata viongozi bora, wazalendo na wenye dhamira ya dhati ya kuwaletea Watanzania maendeleo.
Haiwezekani leo hii tuna rasilimali kibao kuanzia madini ya kila aina, vivutio vya utalii, nishati ya gesi, wingi wa misitu na mazao ya baharini lakini Tanzania inakuwa miongoni mwa nchi maskini.
Hapa ni lazima tutafakari kauli ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere kuwa ili nchi iendelee inahitaji vitu vinne navyo ni ardhi, watu, siasa safi na uongozi bora. Ninasema tutafakari ni kipi tunachokikosa kati ya vitu hivyo vinne hadi Watanzania waendelee kuwa maskini licha ya kuwa moja ya nchi zinazoongoza barani Afrika kwa kuwa na rasilimali nyingi.
Hakuna ubishi tuna tatizo la uongozi ndio maana hatufiki kule tunakotaka kwenda na wanahabari wanalo jukumu zito la kuirudisha nchi hii kwenye mstari.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa