Home » » FUNDI RADIO AFA BAADA YA KUZIDIWA GESTI

FUNDI RADIO AFA BAADA YA KUZIDIWA GESTI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

FUNDI radio maarufu mjini hapa, Daniel Mosha (53), amefariki dunia wakati akipatiwa matibabu katika hospitali ya Mkoa baada ya kuugua ghafla akiwa anafanya mapenzi na mwalimu mmoja katika nyumba ya kulala wageni iitwayo Cheyo.
Tukio hilo limetokea jana majira ya saa 11:00 alfajiri katika nyumba hiyo iitwayo Cheyo chumba namba nne, wakati fundi huyo akijivinjari na mpenzi wake huyo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Kamishna Msaidizi Mwandamizi (SACP), Geofrey Kamwela, alisema fundi huyo alifariki Oktoba 14 mwaka huu saa 10.30 jioni katika hospitali ya Mkoa alikokimbizwa baada ya kuzidiwa akiwa gesti.
Aidha, Kamanda Kamwela alisema kuwa Oktoba 13 mwaka huu majira ya jioni, marehemu akiwa nampenzi wake wa muda mrefu, Serafine Lucian (56), mwalimu wa shule ya Msingi Manguanjuki manispaa ya Singida, walipanga chumba namba nne kwa ajili ya mapumziko ya usiku mzima.
"Ilipofika alfajiri saa saa 11 Oktoba 14 mwaka huu, mwanaume huyo alianza kuugua ghafla huku akikoroma na ndipo mwalimu Serafine, aliamka na kumwita meneja wa nyumba hiyo na kumweleza juu ya hali ya mpenzi wake," alisema.
Alisema meneja pamoja na mwalimu huyo, walifanya juhudi za kumkimbiza hospitali ya Mkoa ili kuokoa maisha yake lakini mambo yaliendelea kuwa magumu.
Hata hivyo, Kamanda Kamwela, alisema uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa katika chumba walichopanga wapenzi hao, pamoja na vitu vingine zilikutwa paketi tupu za pombe kali aina ya viroba vilivyotumika.
"Tunaendelea na uchunguzi ili kujua kama kuna mtu au watu wanaohusika na kifo hicho cha fundi radio, lakini tunamshikilia mwalimu huyo kwa uchunguzi zaidi, ili pamoja na mambo mengine kuchunguza iwapo kuna mtu au watu waliohusika na kifo hicho,” alisema Kamwela.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa