Mkuu wa mkoa wa Singida aagiza waalimu wakuu wakajifunze matumizi ya fedha kwa mwalimu mkuu mwenzao





Mkuu wa mkoa wa Singida Dk.Parseko Kone akizungumza na baadhi ya walimu wa shule ya sekondari Mwanzi Manyoni mjini.Dk.Kone hakufurahishwa na hali duni ya ofisi ya mkuu wa shule hiyo wakati shule ikiwa na akiba ya zaidi ya shilingi milioni sita.(Picha na Nathaniel Limu).
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi mchanganyiko Ikungi wilaya ya Ikungi mkoani Singida, Olivary Kamili akiwa ofisini kwake akitekeleza majukumu yake. Mkuu wa mkoa wa Singida Dk.Parseko Kone ameagiza walimu wakuu wa shule za msingi na wakuu wa sekondari wafike shule ya msingi mchanganyiko Ikungi, ili wakajifunze juu ya matumizi bora ya fedha za Umma.(Picha na Nathaniel Limu).
Na Nathaniel Limu.
Mkuu wa  mkoa wa Singida Dkt. Parseko Kone amemwagiza mkurugenzi mtenadaji wa halmashauri ya wilaya ya Manyoni, achague walimu wakuu wanne wa shule za msingi na wakuu wa shule za sekondari wanne, awapeleke shule ya msingi mchanganyiko Ikungi, ili wakajifunze juu ya matumizi bora ya fedha za umma.
Akizungumza na walimu wa shule ya sekondari ya Mwanzi iliyopo mjini Manyoni pamoja na viongozi wa wilaya ya Manyoni Dkt. Kone amesema shule ya msingi mchanganyiko Ikungi wilaya ya Ikungi,ni shule ya mfano mkoani Singida kwa matumizi mazuri ya fedha za uuma.
Amesema Ofisi ya mkuu wa shule hiyo ni nzuri mno, pengine si rahisi kuifananisha na ofisi nyingi za wakuu wa wilaya. Ina samani za kisasa, tv, kompyuta, internet, jokofu na makochi ya hali ya juu na kuwa Ofisi kama ile inavutia na inachangia mhusika kubaki ofisini kipindi chote cha kazi.
Akifafanua zaidi, amesema majengo ya shule ya msingi mchanganyiko Ikungi pamoja na ujenzi wa uzio wa ukuta, yamekarabatiwa/kujengwa yana ubora unaofanana na thamani ya fedha zilizotumika.
Dkt. Kone amesema walimu wakuu wa shule za msingi na wakuu wa shule za sekondari, hawana budi kufika kwenye shule hiyo ili kujifunza mwenzao Olivary Kamilly (mwalimu mkuu wa shule ya msingi mchanganyiko Ikungi) anavyutumia fedha za umma vizuri.
Mkuu huyo wa mkoa, ametoa agizo hilo, baada ya kutokuridhishwa na hali duni ya ofisi ya mkuu wa shule ya sekondari Mwanzi mjini Manyoni, wakati shule hiyo benki ina zaidi ya shilingi milioni sita ambazo zimekaa kwa muda mrefu bila kutumiwa.
Katika hatua nyingine, Dkt. Kone amewaagiza watendaji wa halmashauri za wilaya na Manispaa, kujenga utamaduni wa kutembelea miradi mara kwa mara, ili miradi yote ya maendeleo iweze kutekelezwa kwa ubora unaofanana na fedha zilizotumika.
Amesema katika ziara yake wilayani Manyoni, amebaini baadhi ya miradi imetekelezwa chini ya kiwango na kitendo hicho kimechangiwa na viongozi kutokwenda vijijini  kutembelea miradi.
“Acheni tabia ya kukaa maofisini, jengeni utamaduni wa kusimamia kikamilifu miradi ya maendeleo, ili iwe na ubora unakusudiwa uweze kufikiwa”alisema Dk.Kone.
Aidha, amewataka kutunza vizuri miradi iliyomalizika na ile inayohitaji ukarabati, ifanyiwe ukarabati unaofanana na thamani ya fedha zitakazotumika.
Chanzo Mo Blog

Mbunge wa jimbo la Singida mjini Mohammed Dewji atoa msaada wa baiskeli kwa walemavu



Mbunge wa jimbo la Singida mjini Mh. Mohammed Gullam Dewji akizungumza na mmoja kati ya walemavu watano aliowakabidhi baiskeli za magurudumu matatu kwa ajili ya kuwasaidia kumudu maisha yao hivi karibuni.Pamoja na msaada wa baiskeli hizo, Dewji pia alitoa msaada wa Wheel Chair 24 kwa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Singida.Thamani ya msaada huo ni zaidi ya shilingi milioni 14.
Na Nathaniel Limu
Mbunge wa jimbo la Singida mjini, Mohammed Gullam Dewji ametoa msaada wa viti 24 maalum vya wagonjwa (wheel chairs) vyenye thamani ya zaidi ya shilingi 24 milioni, kwa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Singida.
Pamoja na viti hivyo mbunge huyo ametoa msaada wa baiskeli za magurudumu matatu kwa walemavu watano wa jimboni kwake.
Akizungumza kwenye makabidhiano ya msaada huo, Dewji amesema msaada huo ni mwendelezo wa misaada mbalimbali anayoitoa jimboni kwake, kwa ajili ya kusaidiana na serikali kuboresha huduma mbalimbali zikiwemo za sekta ya afya.
Alisema ana aimani kwamba viti hivyo vitasaidia wagonjwa katika hospitali hiyo hasa wale watakaokuwa hawawezi kutembea.
“Tunaochoomba tu ni kwamba viti hivi vitunzwe vizuri ili viweze kutumika kwa muda mrefu”,alisema mbunge huyo.
Awali mganga mfawidhi wa hospitali ya mkoa, Dk.Suleiman Muttani amepongeza mbunge Dewji kwa msaada huo ambao amedai umekuja kwa wakati muafaka.
Dk.Muttani amesema hospitali hiyo inayoendelea kujengwa ina mahitaji mengi na makubwa yakiwemo ya vitendea kazi ambavyo serikali ikiachiwa ifanye peke yake, itachukua muda mrefu kukidhi mahitaji ya hospitali hiyo ambayo itategemewa pia na mikoa jirani.
“Kwa kweli nakushukuru sana mbunge wetu kwa msaada huu wa viti.Tunakuomba usichoke kuisaidia vifaa hii hospitali ya rufaa.Tusaidie pia kuwahamasisha marafiki zako au taasisi mbalimbali ziweze/waweze kutusaidia vitendea kazi kwa kadri ya uwezo wao”,amesema Dk.Muttani.
Kwa mujibu wa Dk.Muttani, hospitali hiyo ya rufaa itakapokamilika itakuwa na majengo 47 yenye thamani ya zaidi ya shilingi 150 bilioni.
Serikali kila mwaka imekuwa ikitenga shilingi bilioni mbili kwa ajili ya ujenzi.Kwa utaratibu huo wa kutenga kiasi hicho cha fedha hospitali hiyo itachukua zaidi ya miaka 45 kukamilika kujengwa.
(Picha na Nathaniel Limu).
 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa