Mkuu  wa
 Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi amelishukuru Shirika la Nyumba 
 Taifa (NHC) kwa msaada wa mifuko ya saruji 10, kofia za bati 20, mabati
 90 ya geji 28 vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya shilingi 2.6 milioni 
ukiwa ni msaada kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa bweni la sekondari 
Mwanzi iliyoko Wilayani Manyoni Mkoani Singida.
Dkt.
 Nchimbi ametoa shukrani hizo juzi wakati akipokea masaada huo kutoka 
kwa Meneja wa NHC Mkoa wa Singida Ladislaus Bamanyisa na kutoa wito kwa 
mashirika, watu binafsi na taasisi zikiwemo mabenki, kuiga mfano mzuri 
wa NHC kusaidia serikali katika kuboresha sekta mbalimbali ikiwemo ya 
elimu.
“Mimi
 nitumie nafasi hii kuwaita au kuwaalika mabenki na taasisi zingine kuja
 mkoani Singida kutuunga mkono katika kutekeleza miradi mbalimbali ya 
maendeleo ya wananchi, pamoja na uboreshaji wa miundo mbinu ya shule za 
msingi na sekondari”,amesema.
Ameongeza
 kuwa benki, shirika au watu binafsi watakaojitokeza kuunga mkono 
kuuendeleza Mkoa wa Singida kwa kujenga jengo lo lote pamoja na majengo 
ya shule, huduma za afya na mengine yanayolenga kuwanufaisha wananchi, 
wataruhusiwa kupaka rangi na kuweka nembo zao ili kutangaza shughuli au 
huduma wanazotoa.
Amesema
 kwa njia hiyo benki, taasisi au watu binafsi watakuwa wamejitangaza na 
tangazo hilo litadumu kwa muda mrefu ikilinganishwa na matangazo 
mengine.
“Kwa
 upande wa wadau binafsi na wao wataruhusiwa kuweka picha za familia zao
 kwenye majengo au miradi husika. Kama ni mfugaji na ameuza sehemu ya 
mifugo yake kugharamia miradi wa umma, ataruhusiwa kuweka picha ya 
familia na ng’ombe zao”, amesema Dkt. Nchimbi.
Naye
 Meneja wa NHC Mkoa wa Singida Ladislaus Bamanyisa, amesema wataendelea 
kuiunga mkono serikali katika kuboresha sekta mbalimbali na huo mchango 
ni sehemu ndogo ambapo shirika bado linaendele ana jitihada za kukusanya
 michango mingine.
Wakati
 huo huo Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Nchimbi amezungumza na watumishi 
wa halmashauri ya Wilaya ya Manyoni na kuwaeleza kuwa halmashauri za 
wilaya na manispaa zimekuwa ni chanzo au viwanda vya kuzalisha mabango 
na kelele nyingi kwa wananchi kutokana na huduma zisizokidhi mahitaji na
 ubadhirifu wa fedha za umma.
Dkt.
 Nchimbi ameongeza kuwa ataelekeza nguvu zake kuanzisha na kufufua 
kilimo cha umwangiliaji na ufugaji wa samaki ili Mkoa uweze kunufaika 
kiuchumi na ujio wa makao makuu kuhamia mkoa jirani wa Dodoma.
“Sisi
 wakazi wa mkoa wa Singida sote ni lazima tujiandae kikamilifu kulisha 
makao makuu ya nchi yatakapokuwa Dodoma. Tuitumie fursa hiyo kumtokomeza
 adui umaskini”, amesisitiza.
Naye
 Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Geofrey Mwambe amesema wakati wanaendelea na 
ujenzi wa bweni halmashauri ya Manyoni imejipanga pia kujenga uzio 
katika shule hiyo ya sekondari ya Mwanzi ili kuboresha ulinzi katika 
shule hiyo.
Mwambe
 amesema kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wanamalizia ujenzi wa 
bweni moja na kuanza ujenzi wa bweni lingine huku akiwashukuru 
wafanyabiashara wa Wilaya ya Manyoni kwa kujitoa katika kusaidia 
maendeleo ya Wilaya hiyo.
 
0 comments:
Post a Comment