UFAULU DARASA LA SABA WAPANDA MKOA WA SINGIDA; ELFU KUMI NA NNE KUJIUNGA NA KIDATO CHA KWANZA 2017.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Kiwango cha ufaulu wa mitihani ya kumaliza elimu ya msingi Mkoani Singida kimepanda kutoka wastani wa asilimia 58.41 mpaka asilimia 69.25 ikiwa ni ongezeko la asilimia 11 huku wanafunzi 14,759 wakichaguliwa kujiunga na masomo ya sekondari kwa kidato cha kwanza kwa mwaka 2017.

Buhacha Baltazar Kichinda akiongoza kikao cha uteuzi wa wanafunzi wa kidato cha kwanza kwa mwaka 2017 kama Kaimu Katibu Tawala Mkoa na mwenyekiti wa kikao hicho amesema mkoa umefaulisha wavulana 6,852 na wasichana7,907 huku akiwapongeza waalimu wote kwa bidii ya ufundishaji iliyopelekea mkoa wa singida kushika nafasi ya 12 kati ya Mikao 26 ya tanzania bara.

Kichinda ameipongeza halmashauri ya Itigi kwa kushika nafasi ya kwanza kati ya halmasahuri saba za mkoa wa singida na ya 38 kitaifa kati ya halmashauri 186 za Tanzania bara huku ikifaulisha kwa asilimia 80.41. Aidha amewatia moyo halmasahuri ya Mkalama kwa ufaulu hafifu wa 57.51 na kuwa nafasi ya 155  kitaifa.

Kichinda ameongeza kuwa kwa sasa kila Mkurugenzi wa halmasahuri anapaswa kukaa na wadau wake wa elimu ili kupanga mikakati ya kuboresha zaidi elimu, amesema lengo kubwa kwa sasa ni kuhakikisha kila mwanafunzi aliyefaulu anajiunga na kidato cha kwanza na kumaliza elimu ya sekondari.

Amesema sekta ya elimu inachangamoto mbalimbali ikiwemo utoro wa walimu na wananfunzi, miundombinu ya vyumba vya madarasa kutotosheleza mahitaji halisi, upungufu wa waalimu, uhaba wa nyumba za walimu pamoja na waalimu wenyewe kuwa wachache tofauti na mahitaji halisi hivyo amewata wadau wa elimu kujipanga kutatua changamoto hizo na sio kusubiria serikali kuu kufanya kila kitu.

Aidha kichinda amesema kuwepo na utaratibu wa kuwapongeza waalimu hasa kwenye shule zilizofanya vizuri ili iwe motisha kwa kazi wanayoifanya huku akiitangaza shule ya msingi Utaho ya halmasahuri ya Ikungi kuwa ya kwanza kimkoa kwa shule zenye wananfunzi zaidi ya 40 na shule ya msingi Aghondi ya Itigi kuwa ya kwanza kimkoa kwa shule ambazo zina wanafunzi chini ya 40.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Singida Elias Tarimo amesema ili kuboresha elimu mkoani Singida msisitizo uwepo wa kuhakikisha wananfunzi wote wanapata chakula shuleni ili waweze kusikiliza kwa umakini mzuri.

Tarimo ameongeza kuwa wazazi wanapaswa kutambua kuwa elimu bila malipo haiwaondolei wajibu wao kama wazazi wa kuhakikisha wanafunzi wanakula, wanalala na kuvaa hivyo hivyo watakaposhirikishwa katika kuchangia chakula, ujenzi wa mabweni au shuguli za elimu wajitoe kwani wamiliki wa shule ni wazazi.

Amesema utaratibu wa kufanya ukaguzi ili kuwatambua waalimu watoro au wazembe ufanyike katika halmashauri zote na kwa viongozi wote wanaotembelea vijijini bila ya kusubiri ziara maalumu ya ukaguzi na kuongeza kuwa hali hiyo itawaongezea umakini waalimu katika kutekeleza majukumu yao lakini pia watendaji watabaini changamoto za waalimu na shule na kuzitatua kwa uharaka.

RC SINGIDA AHIMIZA WATUMISHI KUWAJIBIKA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mkuu wa mkoa wa Singida Mhandisi Mathew Mtigumwe, amewahimiza watumishi wa umma hasa wa ngazi ya Vijiji na Kata kuwajibika  na kutimiza vyema majukumu yao kwani wao wako karibu zaidi na Wananchi, ili kutimiza adhma ya Serikali ya awamu ya tano ya kumpunguzia kama si kumuondolea kabisa kero zinazozuilika Mwananchi wa kawaida.

WANANCHI WA KITARAKA SINGIDA WAOMBA MAENEO YA UKULIMA NA UFUGAJI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399

Wananchi wa Kata ya Kitaraka iliyopo katika Halmashauri ya Itigi, Wilaya ya Manyoni, Mkoani Singida, wamemuomba Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mh. William Ole Nasha, kuwapatia shamba linalomilikiwa na Serikali la Tanganyika Packers, ambalo Serikali imeacha kulitumia kwa zaidi ya miaka 20, ili walitumie kwa shughuli za Kilimo na Ufugaji.

Wananchi hao wamefikisha maombi hayo kwa Mh. Waziri alipotembelea shamba hilo lenye ukubwa wa ekari 45,000, na kuzungumza na Wananchi wa Kata hiyo waliolalamika kuwa hawana eneo la kulima wala kufuga ilihali shamba hilo halitumiki na linafaa kwa shughuli hizo.

Nae Mh. Waziri akizungumza na Wananchi hao amesema Serikali ya awamu ya tano ni Serikali inayosikiliza kero za Wananchi na kuzishughulikia kwani ipo karibu zaidi na Wananchi na ndio sababu ya yeye kufika Kijijini hapo ili kuona namna bora ya kutatua changamoto hiyo na kuweka utaratibu jinsi shamba hilo litakavyotumika.

"Wizara inalichukua suala hili ikalitolee maamuzi, Wananchi wavute subira wakingoja Serikali itoe ufafanuzi juu ya suala hili, ni marufuku mwananchi yeyote kuvamia na kufanya shughuli za kilimo ama ufugaji kwa sasa hadi hapo Serikali itakapotoa maelekezo mapya" alisema Mh. Nasha.

Mh. Waziri pia akatoa wito kwa wafugaji wa maeneo hayo kuacha tabia ya kukata miti hovyo, kwani kwa kufanya hivyo kwani wanaharibu mazingira na watapelekea eneo lake kuwa jangwa, akawasisitiza kufuga ufugaji wa kisasa kwa kufuga madume ya kisasa, kupunguza wingi wa mifugo ili uendane na malisho waliyonayo, ukubwa wa eneo na kuendana na mabadiliko ya tabia nchi, kuitumia mifugo yao kujiendeleza kiuchumi kama kuwasaidia kujenga makazi bora na kushiriki kuchangia shughuli za maendeleo.


MKUU WA MKOA AELEKEZA HALMASHAURI YA SINGIDA KUHAMIA ILONGERO NDANI YA KIPINDI CHA MIEZI SITA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Mhandisi Mathew John Mtigumwe amemtaka Mkuu wa Wilaya ya Singida kusimamia utekelezaji wa maamuzi ya kuhamishia makao makuu ya halmashauri ya Singida katika mji mdogo wa Ilongero ndani ya kipindi cha miezi sita  ili kusogeza huduma karibu na wananchi wa halmashauri hiyo.
Mheshimiwa Mhandisi Mtigumwe amefikia uamuzi huo kutokana na taarifa za kuwepo watu wachache wanaotaka kufanya mabadiliko ya makao makuu bila ya kusikiliza mawazo ya wananchi wengi huku wananchi wakipendelea makao makuu ya halmashauri hiyo kuwa katika mji mdogo wa Ilongero.
Ameongeza kuwa baraza la madiwani la halmashauri ya Singida linapaswa kuketi tena na kufanya maamuzi sahihi kwa maslahi ya wananchi wengi huku akiongeza kuwa endapo wanataka kufanya mabadiliko wayafanye wakiwa tayari wameshahamia katika halmashauri yao tofauti na sasa ambapo bado ofisi zipo manispaa ya Singida.
Mheshimiwa Mhandisi Mtigumwe amesema wananchi wanataka kupatiwa huduma kwa ukaribu hivyo halmashauri kuhamishiwa Ilongero itasaidia kusogeza Huduma ambapo zitatolewa kwa ufanisi huku akimshauri Mkurugenzi wa halmashauri hiyo kujipanga ndani ya kipindi hicho waanze kutumia ofisi chache zilizopo.
Aidha Mheshimiwa Mhandisi Mtigumwe amewataka wananchi wa halmashauri na Mkoa mzima wa Singida kujituma na kufanya kazi kwa bidii, wakulima wajiandae FEMA kwa msimu huu wa kilimo na kujitahidi kutunza vyakula ili kujiepusha na njaa na wafanyabiashara watumie fursa mbalimbali kujiongezea kipato.
Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Singida Martha Mlata amesema chama hicho mkono mapendekezo ya wananchi yakutaka makao makuu kuwa katika mji mdogo wa Ilongero na kuahidi kufuatilia na kusimamia utekelezaji wake.
Katika kuunga mkono mapendekezo ya wananchi Mbunge wa jumbo la Singida kaskazini la kaskazini Mhe. Lazaro Nyalandu amesema kufikia mwezi Januari ataweka ofisi za Mbunge katika mji wa  I'll wananchi wapate Huduma na kumfikishia kero kwa ukaribu zaidi.

Uongozi bora na matumizi bora ya fedha vimeiletea Tanzania maendeleo

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.



Na. Lilian Lundo – MAELEZO

Dar es Salaam

28.11.2016

IMEELEZWA kuwa Uongozi bora na matumizi bora katika usimamizi wa fedha za Serikali ni miongoni mwa sababu zilizoiletea Tanzania maendeleo tangu ilipopata uhuru mwaka 1961.

Hayo yamebainishwa leo Jijini Dar es Salaam na Spika Mstaafu, Pius Msekwa wakati wa mahojiano maalum na mwandishi wa habari hii kuhusiana na hatua ambazo Tanzania imepiga tangu ipate uhuru mwaka 1961.

Msekwa alisema kuwa uongozi bora pamoja matumizi bora ya fedha ndizo nguzo kuu zilizoiletea Tanzania maendeleo yanayoonekana leo ambapo takribani sekta zote zimepiga hatua kubwa ukilinganisha na kipindi cha uhuru mwaka 1961.

“Wakati tunapata uhuru mwaka 1961 tulirithi vitu vichache kutoka kwa wakoloni ambavyo ni shule hospitali ya Muhimbili iliyokuwa ikijulikana kama Princess Magreth ambayo kwa sasa imepiga hatua na kuweza kufanya upasuaji wa moyo ambao haukuwahi kufanyika kwa miaka ya nyuma,” alifafanua Msekwa.

Alisema kuwa maendeleo yote hayo yametoka na juhudi za marais waliopita na aliyepo, katika uongozi wao ambapo wamekuwa wakipambana na maadui watatu wa maendeleo ambao ni ujinga, maradhi na umasikini.

Aidha alisema kuwa viongozi hao wamekuwa wakipambana na maadui hao kulingana na fedha ambazo zimekuwa zikipatikana katika kipindi cha uongozi wao.

Msekwa aliwataka Watanzania kuendelea kumuenzi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kutokana na misingi aliyoiacha ambayo imeweza kutumiwa na viongozi wa nchi na kuendelea kuleta maendeleo ambayo Tanzania inajivunia hadi sasa.

SINGIDA YATEKELEZA AGIZO LA RAIS LA USAFI WA MAZINGIRA KIKAMILIFU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.



Na Evelyn Mkokoi – Singida
Katika kutekeleza agizo la Serikali la usafi wa mazingira kila Jumamosi ya Mwisho wa Mwezi, wananchi wa Mkoa wa Singida wamejitokeza kwa kwingi katika zoezi hilo lililofanyika kitaifa mwezi huu mkoani humo.
Akishiriki zoezi hilo  Mkoani Singida kitaifa, Naibu waziri Ofisi ya Makamu w Rais Muungano na Mazingira Mhe. Luhaga Mpina, ameupongeza uongozi wa Mkoa wa Singida na wana  singida kwa ujumla kwa jitihada walizoonyesha kwani kila eneo la Singida Jumamosi ya leo Limeonekana kuwa nadhifu kabla hata ya muda wa kuanza kufanya usafi tofauti na mikoa mingine ambayo amewahi kushiriki zoeZi hilo.
Akiongea na Hadhara iliyojitokeza katika siku ya usafi Mjini Singida Leo, Mpina alisema kuwa usafi wa mazingira  unapunguza magonjwa yatokanayo na uchafu akitolea mfano ugonjwa wa kipindu pindu na hivyo taifa likiwa safi litaweza kuokoa ngumukazi yake, na kupunguza gharama ambazo zingetumika kutibu maradhi hayo.
“Ukiona Msichana mzuri barabarani ujue kagharamiwa ukiona kijana mtanashati vilevile ujue kagharamiwa Mkiona taifa zuri na safi ujue limegharamiwa na wananchi wake wamejipanga vizuri, hivyo wana singida Muendelee kujitahidi katika suala zima la usafiwa mazingira.” Alisisitiza Mpina.
Zoezi la usafi wa Mazingira Mkoani Singida lilienda sambamba na zoezi la upandaji miti ambapo, Naibu Waziri Mpina Pia alishiriki  na wananchi katika zoezi la kupanda miti mkoani Singida ambapo alipanda mti aina ya mpararachichi katika eneo la stand mpya ya Misuna.

WAMILIKI WA LESENI ZA UCHIMBAJI MDOGO WA MADINI MKOANI SINGIDA WAMETOZWA FAINI YA SHILINGI MILIONI 20 KWA UHARIBIFU WA MAZINGIRA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 





Na Evelyn Mkokoi-Singida
Wamilki wa Leseni za uchimaji mdogo wa madini wa Joshua Mine na Sekeknke one mine wa Sekenke Mkoani Singida, wametozwa faini ya shilingi milioni 10 kila moja kwa kosa la uchafuzi wa mazingira wa kutumia vibaya madini ya zebaki, hivyo kuhatarisha maisha ya viumbe hai.
Baraza la taifa la Hifadhi na usimamizi wa Mazingira limeitoza faini hiyo kupitia mratibuwa wa Barazakanda a Ziwa Bw. Jamali Baruti na kiwataka wamiliki hao kulipa faini hiyo ndani ya siku 14.
Adhabu hiyo inatokana na makelele katika eneo la uchimbaji, kusambaa kwa vumbi lisilovumilika, kukosekana kwa vyoo pia na matumizi mabaya ya miti katika uchimbaji wao ambao huenda sambamba na uharifu wa misitu.
Aidha Baraza limewataka wachimbaji hao kuwa na vyeti vya tathmini ya athari ya mazingira pamoja na leseni ya uchimbaji.
Kwa Upande wake Mkuu wa Wiaya ya Mkalama Injinia Joakim Masakala  akimuwaklisha mkuu wawiaya ya Iramba, alisema kuwa ni vizuri wakazi wa maeneo hayo wanavyojibidisha katika kazi lakini ni muhimu sana kuzingatia afya kwani uchimbaji wa kutumia madini aina ya zebaki bila vifaa salama kazini unaweza kuleta maradhi hususan ya saratani kwani madini hayo upenya kirahisi katika mwili wa binadamu.
Awali Katika Kikao na uongozi wa Mkoa pamoja na wadau wa Mazingira Naibu Waziri Mpina alitolea ufafanuzi masuala mbalimbali ya Mazingira ikiwemo matumizi ya Mifuko ya plastic na kuwashauri wakazi wa singida kutunza mazingira akitolea mfano wa ziwa Kitangiri lililoo Hatarini kutoweka kabisa.
 

WAFANYABIASHARA MKOANI SINGIDA WAJIPATIA BILIONI 1.8 KWA MAUZO YA KUKU.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Na Nathaniel Limu-Singida
Wafanyabiashara wa kuku wa asili/kienyeji mkoani Singida wamejipatia mapato ya zaidi ya shilingi bilioni 1.8, baada ya kuuza kuku 151,242 katika kipindi cha mwaka jana hadi sasa.
 
Hayo yamesemwa juzi na kaimu Katibu Tawala Msaidizi Uchumi na Uzalishaji Beatus Choaji wakati akitoa taarifa ya uendelezaji wa kuku wa asili, kwenye kikao cha kamati ya ushauri mkoa (RCC) kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano uliopo kwenye jengo la ofisi ya mkuu wa mkoa mjini hapa.
 
Chowaji amesema mapato hayo yamepatikana baada ya kuku hao 151,242 kusafirishwa  na kuuzwa nje ya mkoa ikiwemo jijini Dar-es-salaam.
 
“Kuku wa asili wakifungwa vizuri kwa kudhibiti ugonjwa wa mdondo na kuzingatia kanuni za ufugaji bora wanaweza kuleta mabadiliko makubwa na ya haraka ya kipato. Kuku wa asili pia ni lishe bora hususani kwa watoto na akina mama”, ameongeza Choaji.
 
Ili kuimarisha ufugaji kuku wa asili amesema imependekezwa halmashauri zote zitekeleze mkakati wa kuchanja kuku kwa wakati moja mara tatu kwa mwaka kwa kutumia watoa chanjo wasiokuwa wataalam wa mifugo.
 
Akisisitiza amesema “Mkakati huu unatarajiwa kuanza mara halmashauri zitakazokamilisha utoaji wa mafunzo kwa watoa chanjo hao. Halmashauri zimesisitizwa kushiriki kikamilifu kutekeleza mkakati huo ili kuinua kipato cha wananchi kwa haraka zaidi”.
 
Mapema Mkuu wa Mkoa wa Singida na mwenyekiti wa kikao hicho, Mhandisi Mathew John Mtigumwe, akifungua kikao hicho ameagiza kuwa wananchi wahamasishwe, ili wasiendelee kuuza chakula walichovuna msimu uliopita kiweze kuwafikisha msimu ujao wa mavuno.
 
Mhandisi Mitugumwe amesema kwa mujibu wa mamlaka ya hali ya hewa nchini (TMA) mvua za msimu huu zinatarajiwa kunyesha kwa kiwango cha chini ya wastani.
 
“Hivyo ni jukumu letu sote kuhimiza na kushauri wananchi kufuata kanuni bora za kilimo na kupanda mazo ya kipaumbele yanayostahimili ukame, na yanayokomaa mwa muda mfupi.
 
Wakati huo huo Mkuu huyo wa mkoa, ametumia fursa hiyo kutoa shukrani zake za dhati kwa wananchi wadau wa elimu, wafanyabiashara, kampuni za simu za viganjani na mashirika ya umma na binafsi, kwa kushiriki kutekeleza agizo la rais Magufuli la kumaliza uhaba wa madawati mashuleni.

WAZIRI MWIGULLU AWAONYA MADEREVA WANAOACHA MITI NA MAWE BARABARANI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Na Nathaniel Limu- Singida
Waziri wa mambo ya ndani Mhe. Mwigullu Lameck Nchemba (mb), ameliagiza jeshi la polisi nchini,kuwakamata na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria  madereva wanaoacha mawe na matawi ya miti barabarani.

Nchemba ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Iramba mkoani Singida, ametoa agizo hilo wakati akizungumza kwenye kikao cha 38 cha bodi ya barabara mkoa kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa mkoa mjini hapa.
 
Amesema baadhi ya madereva wa magari na hasa yale makubwa,hutumia mawe kuzuia magari yao kutembea wakati wakiyafanyia matengenezo ya dharura.
 
“Wakiisha maliza kuyafanyia matengenezo magari yao, madereva hao huyaacha barabarani mawe na matawi ya miti ambayo hutumika kutoa tahadhari kwa vyombo vingine vya moto. Kitendo hicho kinahatarisha maisha na mali za watumiaji wengine wa barabara kwa vile yanaweza kusababisha ajali”, amesema Mwigullu.
 
Kwa hali hiyo amesema jeshi la polisi linapaswa kuimarisha mawasiliano ili waweze kuwathibiti na kuwakamata madereva wanaoacha mawe na matawi ya miti barabarani.
 
Katika hatua nyingine, waziri huyo amesema upo umuhimu mkubwa wa wananchi na hasa wale wanaoishi kando kando ya barabara kuelimishwa juu ya matumizi bora ya barabara zinazojengwa kwa fedha nyingi ili waweze kuacha kupitisha mifugo yao na mikokoteni barabarani.
 
Kwa upande wake mwenyekiti wa bodi ya barabara na Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhandisi Mathew John Mtigumwe ameagiza kuwa fedha zinazotolewa na serikali na wafadhili mbalimbali wa miradi ya barabara matumizi yake yasimamiwe kikamilifu, ili zitumike kwa miradi iliyokusudiwa.
 
“Ujenzi wa miradi hiyo ya barabara ufanane na thamani halisi ya fedha zilizotumika. Pia kazi za ujenzi wa barabara za ngazi zote wapewe wakandarasi bora na wenye uwezo wa kutekeleza miradi ikakamilika kwa wakati. Nasisitiza kuimarishwa kwa usimamizi na ukaguzi wa mara kwa mara wa miradi ya barabara ili ziwe za kiwango kinachokusudiwa”,amesema.
 
Wakati huo huo, mhandisi Mtigumwe ambaye kabla ya kuteuliwa kuwa mkuu wa mkoa alikuwa meneja TANROADS mkoa, ametumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa TANROADS mkoa wa Singida chini ya meneja wake Mhandisi Leonard Kapongo kwa kazi nzuri ya usimamizi na ukaguzi uliopelekea miradi ya barabara kujengwa kwa ubora unaofafana na fedha zilizotumika.

ANNE MAKINDA AZITAKA HOSPITALI ZA SERIKALI ZIBORESHE HUDUMA ILI ZIPATE WATEJA WENGI WA BIMA YA AFYA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Mwenyekiti wa bodi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Anne Makinda amezishauri hospitali, vituo vya afya na zahanati za serikali kuboresha huduma za afya ili wananchi waliojiunga katika mifuko ya afya ya jamii (CHF) na mfuko wa bima ya afya washawishike kutumia huduma katika hospitali zao.

Makinda ametoa rai hiyo alipotembelea hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida kujionea huduma za Bima ya afya zinavyotolewa na changamoto zilizopo ili kwa ushirikiano wa mfuko wa bima ya afya na wadau wake waweze kuzitatua.

Amesema hospitali na vituo binafsi au vya mashirika mbalimbali wamekuwa wanufaikaji wakubwa wa kupata wateja wengi wa bima ya afya na mifuko ya afya ya jamii kutokana na kusifiwa kuwa wanatoa huduma bora tofauti na hospitali za serikali ambazo hupata wateja wachache na hivyo kupata faida kidogo.

Makinda amesema hamasa anayoitoa ya kuboresha huduma kwa vituo vya serikali haimaanishi mfuko wa taifa wa bima ya afya hauthamini vituo na hospitali binafsi bali inataka hospitali za serikali kuboresha huduma na kuingia katika ushindani.

Ameongeza kuwa changamoto ya ukosefu wa dawa na vifaa tiba inawakatisha tamaa watumiaji wa bima ya afya pamoja na watu wengine kujiunga hata hivyo mfuko wa bima ya afya na hospitali za serikali zimejipanga kuziondoa changamoto hizo.

Aidha Makinda ameupongeza Mkoa wa Singida kwa kufanya vizuri katika mfuko wa afya jamii na bima ya afya huku akisisitiza kuendelea kuboresha ili Mkoa wa Singida uwe mfano kwa mikoa mingine ya Tanzania.

Akitembelea majengo mapya ya hospitali rufaa iliyopo eneo la Mandewa Makinda amevutiwa sana na majengo hayo huku akiutaka uongozi wa Mkoa kwa kushirikia na wadau wengine hasa mfuko wa bima ya afya kutafuta pesa za ukamilishaji wa majengo muhimu ili huduma zianze kutolewa katika hospitali hiyo kwakuwa itakuwa msaada hata kwa kanda nzima ya kati.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Mhandisi Mathew J Mtigumwe amemshukuru Anne Makinda kwa kuutembelea mkoa wa Singida ili kujionea huduma za Bima ya afya zinavyotolewa.

Mheshimiwa Mhandisi Mtigumwe amemuahidi Makinda kuwa Mkoa utaendeleza ushirikiano mzuri na Mfuko huo na kuomba waendelee kutoa ushirikiano wa vifaa tiba na ukarabati wa miundombinu ya hospitali na vituo vya afya vya serikali ili kuboresha huduma za afya Mkoani Singida.

Ameongeza kuwa Mkoa utaendelea kuhamasisha wananchi kujiunga na mfuko wa afya ya jamii na bima ya afya ili wapate huduma bora hata wakati wakiwa na upungufu wa fedha kwani bima huokoa maisha.

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa