Mvua zaathiri hekta 2,000 za zao la Pamba Mkoani Singida


DSC05358
Mkuu wa wilaya ya Ikungi mkoani Singida, Gishuli Charles (kulia) akitoa maelekezo juu ya mikakati ya kuboresha kilimo cha pamba mbele ya wajumbe wa kikao cha kazi cha kutathimini zao la pamba msimu huu kilichohudhuriwa na wajumbe kutoka bodi ya pamba na wadau wa zao hilo. Dc Charles alikuwa mwenyekiti wa kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa mkoa mjini hapa. Kushoto ni kaimu katibu tawala mkoa wa Singida,Mumba.
DSC05355
Baadhi ya wajumbe wa kikao cha kazi cha kutathimini kilimo cha pamba cha msimu huu kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa mkoa mjini Singida.(Picha na Nathaniel Limu).
Na Nathaniel Limu, Singida
MVUA zilizonyesha kwa mtawanyiko usioridhisha msimu huu na kusababisha ukame mkali,zimeathiri zaidi ya hekta 2,000 za zao la pamba na mavuno yanatarajiwa kuwa hafifu;imeelezwa.
Hayo yamesemwa na mkuu wa mkoa wa Singida,Dk.Parseko Kone,wakati akifungua kikao cha kazi cha wadau wa zao la pamba mkoani hapa, kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa mkoa mjini hapa.
Alisema kwa kuzingatia hilo,mkoa wa Singida kwa kushirikiana na bodi ya pamba umeona umuhimu wa kukutanisha wadau wa zao la pamba ili kujadili maendeleo ya kilimo cha pamba cha mkataba ambacho kina tija zaidi.
Aidha, Dk.Kone alisema kukutana huko pia zitatolewa taarifa  za mafanikio na changamoto mbalimbali zilizojitokeza msimu wa 2014/2015,na kuweka mikakati ya kufanikisha masuala ya soko la pamba katika msimu huu.
“Napenda tuelewe kuwa mkutano huu ni fursa nzuri ya kuwakutanisha viongozi na wataalam wa ngazi ya wizara,mkoa,halmashauri na wakulima,ili kujadiliana mafanikio yaliyopatikana,changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya kuhakikisha juhudi za kuongeza tija na faida katika uzalishaji wa zao la pamba, zinaendelezwa”,alifafanua.
Katika hatua nyingine,Dk.Kone alisema katika msimu huu jumla ya wakulima 821 wa zao la pamba,wamepewa mafunzo ya kilimo bora cha pamba.
Aidha, alisema katika msimu huu jumla ya hekta 6,757 za pamba zimelimwa,chupa 11,346 za viuatilifu na mabomba 35 ya kunyunyizia pamba,yalisambazwa na kampuni pekee inayoshughulkia zao la pamba mkoani hapa ya Biosustain ya jijini Dar-es-salaam.
“Nitumie fursa hii kuipongeza kampuni ya Biosustain kwa kazi nzuri inayojishughulisha na kilimo cha mkataba mkoani mwetu.Kampuni hii imeweza kufufua zao la pamba kwa kuanzisha kiwanda cha kuchambua pamba.Mfumo wa kilimo cha mkataba umeweza kunufaisha wakulima 2,500”,alisema Dk.Kone.
Zao la pamba ni miongoni mwa mazao makuu manne ya biashara yanayozalishwa hapa nchini na linachukua nafasi ya nne kwa kuchangia uchumi wa taifa.Wastani wa faifa wa uzalishaji, ni kilo 300 kwa ekari ikilinganishwa na lengo lililowekwa la kufikia uzalishaji wa kilo 1,500 kwa ekari ifikapo mwaka huu wa 2015.
Kwa mkoa wa Singida,hali ya uzalishaji wa pamba imekuwa ikibadilika kwa kiasi kikubwa ikilinganishwa na mazao mengine ya biashara, kutokana na kuyumba kwa bei ya zao hilo mwaka hadi mwaka.
Baadhi ya mikakati ya kuimarisha kilimo cha pamba mkoani hapa ambayo imewekwa na kikao hicho,ni pamoja na kuhamasisha kila kaya inalima si chini ya ekari mbili kila msimu.
Mikakati mingine ni halmashauri kushirikiana na wataalamu wa vipimo kuhakikisha matumizi sahihi ya vipimo yanatumika wakati wa kuuza pamba,kuhimiza kilimo cha mkataba na kila mdau wa kilimo cha pamba,atimize wajibu wake.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

CHIKAWE ATOA HOFU UCHAGUZI WA 2015

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

 Kuanza kufuta vyama Jumatatu Vipo vya kiraia, dini.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe.
 Serikali imetishia kuchukua hatua kali kwa watu binafsi, vyama vya siasa, kijamii na vya kidini vitakavyobainika kuvuruga usalama na utulivu wa nchi katika kipindi cha Kura ya maoni kwa Katiba inayopendekezwa na uchaguzi mkuu, huku ikitishia kufuta asasi kadhaa kuanzia wiki ijayo.
 
Imetangaza kwamba kuanzia wiki ijayo itavifuta katika daftari la usajili vyama vya kijamii na vya kidini ambavyo vitakiuka katiba za kuanzishwa kwake.
 
Hatua hiyo ilitangazwa jana jijini Dar es Salaam na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mustakabali wa nchi kuelekea Kura ya Maoni kwa Katiba inayopendekezwa na Uchaguzi Mkuu.
 
VYAMA KUFUTWA JUMATATU
Waziri Chikawe alisema kuanzia Jumatatu ijayo, wizara hiyo itaanza kuvifuta vyama vyote vilivyosajiliwa chini ya Sheria ya Vyama, Sura 337, ambavyo havifuati matakwa ya kisheria ya kuwasilisha taarifa zao za mwaka za ukaguzi wa hesabu na kulipa ada kisheria.
 
Alisema kazi hiyo itaanza kwa vyama vilivyopo jijini Dar es Salaam na itaendelea nchi nzima na kwamba vyama hivyo havitaruhusiwa kuendelea na shughuli zake.
 
“Serikali inapenda kuwataka wananchi mmoja mmoja au vikundi, zikiwamo taasisi za dini kuepuka kushiriki katika vitendo ambavyo vinaashiria kuvuruga amani na utulivu nchini na itachukua hatua za kisheria kudhibiti hali hiyo,” alisema Waziri Chikawe.
 
Waziri Chikawe alisema kwa siku za hivi karibuni kumekuwa na matukio ambapo baadhi ya viongozi wa taasisi za dini wanatoa matamko yanayoashiria kuingilia masuala ya kisiasa kinyume cha sheria na katiba zinazosimamia uendeshaji wa taasisi hizo.
 
Mathalani, alisema viongozi wa dini wanapokutana na kutoa matamko yanayolenga kuwashawishi waumini wao wafuate maelekezo yao kuhusiana na masuala ya Katiba inayopendekezwa au kuhusu Uchaguzi Mkuu ujao, matamshi hayo yanakiuka sheria za usajili wa taasisi hizo.
 
“Ni kweli kuwa viongozi wa taasisi za dini wana haki ya kushiriki katika masuala ya kisiasa kama watu binafsi ila ni kinyume cha sheria kutumia uongozi wao kushawishi waumini wao watekeleze matakwa yao ya kisiasa,” alisema.
 
Alisema serikali inatambua kuwa waumini wa dini mbalimbali wana haki ya kuamini mafundisho ya dini zao, lakini wanapaswa kutekeleza masuala yao ya kisiasa na kijamii kwa utashi wao wenyewe bila ya kushawishiwa na mtu yeyote kama sheria za nchi zinavyosema.
 
“Mfano mwingine ni pale kiongozi au viongozi wa dini wanapochangisha fedha na kuandamana au kukutana na wanasiasa kwa kile kinachoelezwa kuwa ni kuwashawishi kugombea nafasi mbalimbali za uongozi…hii siyo kazi ya taasisi za dini na ni kinyume cha sheria,” alifafanua.
 
Hata hivyo, hakutaja viongozi wa dini waliokwenda kumshawishi mgombea wa urais, lakini mwezi uliopita, kundi la watu wanaodaiwa kuwa ni Masheikh kutoka Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani, lilikwenda mjini Dodoma kumshawishi Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, achukue fomu kugombea urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
 
Pia kundi la Wachungaji wa Makanisa ya Pentekoste kutoka maeneo kadhaa nchini, yalikwenda Dodoma kumshawishi Lowassa kugombea nafasi hiyo.
 
Chikawe alisema uzoefu unaonyesha kuwa kila inapofikia wakati wa kuelekea katika chaguzi mbalimbali, hutokea matukio ambayo mengine yakiashiria uvunjifu wa usalama na utulivu wa nchi.
 
Alisema matukio hayo yanasababisha hamasa za kisiasa au baadhi ya watu kutumia muda kutekeleza ajenda zao za kihalifu kwa kisingizio cha vuguvugu la kisiasa.
 
Waziri huyo alikumbushia matukio ya hivi karibuni Visiwani Zanzibar kulikuwa na matukio ya baadhi ya ofisi za vyama vya kisiasa kuchomwa moto na watu wasiojulikana pamoja na wanachama wa vyama hivyo kuvamiwa na kujeruhiwa wakati wakitoka katika mikutano ya kisiasa.
 
“Kwa vyovyote vile matukio kama haya yanaashiria uvunjifu wa amani na utulivu na ni lazima serikali ichukue hatua kuhakikisha kuwa yanadhibitiwa ili kila mwananchi awe huru kufanya shughuli zake za kisiasa, kijamii na kiuchumi bila hofu ya kufanyiwa uhalifu,” alisisitiza.
 
Aidha, alivishauri vyama vya siasa kuepuka kufanya ushabiki wa kubeba wanachama wao kutoka sehemu moja kwenda nyingine wanapoandaa mikutano na badala yake washirikishe wanachama waliopo sehemu husika kufanya mkutano.
 
Alisema utekelezaji wa jambo hilo utapunguza ushabiki wa kisiasa na tatizo la uvamizi wa wanachama wanapokuwa wanatoka kwenye mikutano ya mbali na maeneo yao pamoja na kupunguza mzigo wa ulinzi kwa askari.
 
MATAMKO YA VIONGOZI WA DINI NA JUKWAA
Tamko la serikali limekuja siku chache baada ya Kiongozi Mkuu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Askofu Josephat Gwajima, kutakiwa kupeleka vielelezo 10 Polisi, ikiwamo hati ya usajili wa kanisa hilo, nyaraka za idadi ya makanisa anayomiliki, muundo wa uongozi wa kanisa lake na nyaraka za helikopta anayomiliki.
 
Vingine ni idadi ya nyumba na mali ambazo Kanisa linamiliki, muundo wa Bodi ya Wadhamini wa Kanisa pamoja na majina yao na makusanyo ya Kanisa.
 
Machi, mwaka huu, Jukwaa la Wakrsto Tanzania, lilitoa tamko la kuwataka waumini wake kujiandikisha kwa wingi katika Daftari la Kudumu la Wapigakura, kuisoma Katiba inayopendekezwa na kujitokeza kuikataa kwa kupiga kura ya hapana. Jukwaa hilo linaundwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (Tec), Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) na Kanisa la Pentekoste Tanzania (CPCT).
 
Pia, Taasisi za Kiislamu nchini zimetoa matamko mbalimbali ya kuwataka waumini kutoshiriki kura ya maoni kutokana na serikali kutopeleka bungeni Muswada wa Mahakama ya Kadhi.
 
Kwa sasa Tanzania ina vyama vya siasa 22 vyenye usajili wa kudumu na kimoja chenye usajili wa muda huku chama tawala ni CCM na vyama vikuu vya upinzani ni Chadema, CUF na NCCR- Mageuzi, ambavyo wakati wa Bunge Maalum la Katiba, waliunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
 
UGAIDI 
Waziri Chikawe alisema serikali imejizatiti kiusalama katika kupambana na vitisho vya ugaidi kwa kuweka maofisa usalama hasa nyumba za ibada, ikiwa ni pamoja na kutumia mashine za kielektroniki zenye uwezo wa kutambua watu waliobeba vitu vya kusababisha milipuko.
 
Aidha, aliwatoa hofu Watanzania kuwa ulinzi umeimarishwa, hivyo waendelee na shughuli zao za kila siku.
 
Kauli ya Waziri Chikawe inakuja huku kukiwa na taarifa zilizosambaa kwenye mitandao ya kijamii kuwa kikundi cha kigaidi cha Al Shaabab kinalenga kushambulia mikoa ya Arusha, Mbeya, Mwanza na Dar es Salaam na baadhi ya vyuo vikuu.
 
Kuhusu kukamatwa kwa raia wa Tanzania, Rashid Mberesero, kwa tuhuma za kuhusika na tukio la mashambulizi katika Chuo Kikuu cha Garissa, nchini Kenya, alisema anachojua ni kuwa amefikishwa mahakamani, lakini serikali haijapewa taarifa rasmi.
 
Chikawe alisema ugaidi ni tatizo la kidunia na kuwaomba wazazi kuwa karibu na watoto wao ili wasijiingize katika makundi au kushawishiwa kwa namna moja au nyingine kuingia katika makundi mabaya hasa kupitia mitandao ya kijamii. Aidha, akijibu maswali ya waandishi wa habari waliotaka kujua hatua zinazochukuliwa dhidi ya wageni wanaodaiwa kuingia kwa wingi nchini, alisema kila mgeni anayeingia nchini wizara hiyo ina taarifa zake na wanaoingia kinyume cha sheria hurudishwa nchini kwao.
CHANZO: NIPASHE

WAAHIDI KUCHAGUA VIONGOZI WATAKAOCHOCHEA KILIMO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.


WAKULIMA na wafanyabiashara wa mkoani Iringa wameahidi kuchagua viongozi watakaokuja na sera itakayoleta ufumbuzi wa haraka utakaoshawishi uzalishaji wa kilimo chenye tija kitakachotoa pia fursa kwa vijana wanaomaliza vyuo vikuu kujiajiri katika sekta hiyo. 

Wakishiriki mjadala wa kilimo na mnyororo wa thamani uliofanyika juzi katika Ukumbi wa Chuo Kikuu Huria mjini Iringa, wadau hao walisema wanashindwa kuamini kama mazingira ya sasa ya kilimo na biashara yake yanategemewa na asilimia 80 ya Watanzania.
 
Mjadala huo uliohusisha pia wawakilishi wa baadhi ya vyombo vya habari wa mjini Iringa, vyama vya wataalamu na wawekezaji wa kilimo, mifugo na wafanyabiashara uliandaliwa na East Africa Business and Media Training Institute kupitia mradi wake wa Best Dialogue Radio Project.

Mwenyekiti wa mradi huo, Rosemary Mwakitwange alisema mijadala hiyo inafanywa katika Mikoa ya Mbeya, Ruvuma, Iringa, Njombe, Rukwa na Morogoro inayotekeleza Mradi wa Ukanda wa Kilimo wa Kusini mwa Tanzania (SAGGOT).
 
“Lengo ni kuamsha mjadala utakaokifanya kilimo kiwe ni kazi ya faida na ya kudumu kwa wananchi kama sera ya kilimo inayoelekeza kuwa sekta ya kilimo inatakiwa kutoa mchango mkubwa katika kutengeneza ajira kwa vijana, na hivyo kutoa matumaini mapya kwa vijana waliomaliza shule,” alisema.

Mwenyekiti wa Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo (TCCIA) mkoani Iringa, Lucas Mwakabungu alisema wakulima wanajitahidi sana kuongeza tija lakini serikali imeshindwa kuboresha miundombinu itakayowahakikishia soko pamoja bei elekezi.
 

Mwakabungu alitoa mfano wa jinsi serikali inavyoshindwa kuwashirikisha wadau wake kukabiliana na tatizo la vipimo batili vya uuzaji mazao ya kilimo (lumbesa) vinavyoathiri na kunyong’onyeza nguvu kazi ya mkulima.
 
Urasimu, rushwa,gharama kubwa za pembejeo, ukosefu wa mikopo na usimamizi na ushiriki mdogo wa wataalamu wa sekta ya kilimo ni baadhi ya mambo yanayofanya biashara ya kilimo iwe ngumu na kufuta matumaini ya Watanzania wakiwemo vijana kuiona kama moja kati ya sekta muhimu zinazoweza kutoa ajira kwo,” alisema. 

Mfanyabiashara wa bidhaa za kilimo, Enock Ndondole alikosoa utaratibu wa serikali wa kuanzisha mambo mengi ya kuikuza sekta ya kilimo; mambo yanayoendelea kushindwa kumuinua mkulima wa kawaida.
 
Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Iringa (IUCo), Jackson Michael alisema shughuli ya kilimo haiwavutii vijana walio wengi kwa sababu ya changamoto zake na akawasihi vijana wenzake kushiriki Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu kwa kuwachagua viongozi watakonesha dhamira ya dhati ya kuikomboa sekta hiyo ili itoe ajira kubwa kwa Watanzania.
 
“Tunaambiwa asilimia 80 ya Watanzania wanategemea kilimo, kuna maswali ya kujiuliza kama kweli Watanzania hao wanalima au wanataka kulima na kama wanalima wanafanya hivyo ili iwe nini?...Maana tunashuhudia baadhi yao wanapewa pembejeo bure na badala ya kuzitumia mashambani mwao wanauza,” alisema.
Chanzo:Majira

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa