Mwenyekiti
 wa bodi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Anne Makinda 
amezishauri hospitali, vituo vya afya na zahanati za serikali kuboresha 
huduma za afya ili wananchi waliojiunga katika mifuko ya afya ya jamii 
(CHF) na mfuko wa bima ya afya washawishike kutumia huduma katika 
hospitali zao.
Makinda
 ametoa rai hiyo alipotembelea hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida 
kujionea huduma za Bima ya afya zinavyotolewa na changamoto zilizopo ili
 kwa ushirikiano wa mfuko wa bima ya afya na wadau wake waweze 
kuzitatua.
Amesema
 hospitali na vituo binafsi au vya mashirika mbalimbali wamekuwa 
wanufaikaji wakubwa wa kupata wateja wengi wa bima ya afya na mifuko ya 
afya ya jamii kutokana na kusifiwa kuwa wanatoa huduma bora tofauti na 
hospitali za serikali ambazo hupata wateja wachache na hivyo kupata 
faida kidogo.
Makinda
 amesema hamasa anayoitoa ya kuboresha huduma kwa vituo vya serikali 
haimaanishi mfuko wa taifa wa bima ya afya hauthamini vituo na hospitali
 binafsi bali inataka hospitali za serikali kuboresha huduma na kuingia 
katika ushindani.
Ameongeza
 kuwa changamoto ya ukosefu wa dawa na vifaa tiba inawakatisha tamaa 
watumiaji wa bima ya afya pamoja na watu wengine kujiunga hata hivyo 
mfuko wa bima ya afya na hospitali za serikali zimejipanga kuziondoa 
changamoto hizo.
Aidha
 Makinda ameupongeza Mkoa wa Singida kwa kufanya vizuri katika mfuko wa 
afya jamii na bima ya afya huku akisisitiza kuendelea kuboresha ili Mkoa
 wa Singida uwe mfano kwa mikoa mingine ya Tanzania.
Akitembelea
 majengo mapya ya hospitali rufaa iliyopo eneo la Mandewa Makinda 
amevutiwa sana na majengo hayo huku akiutaka uongozi wa Mkoa kwa 
kushirikia na wadau wengine hasa mfuko wa bima ya afya kutafuta pesa za 
ukamilishaji wa majengo muhimu ili huduma zianze kutolewa katika 
hospitali hiyo kwakuwa itakuwa msaada hata kwa kanda nzima ya kati.
Naye
 Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Mhandisi Mathew J Mtigumwe 
amemshukuru Anne Makinda kwa kuutembelea mkoa wa Singida ili kujionea 
huduma za Bima ya afya zinavyotolewa.
Mheshimiwa
 Mhandisi Mtigumwe amemuahidi Makinda kuwa Mkoa utaendeleza ushirikiano 
mzuri na Mfuko huo na kuomba waendelee kutoa ushirikiano wa vifaa tiba 
na ukarabati wa miundombinu ya hospitali na vituo vya afya vya serikali 
ili kuboresha huduma za afya Mkoani Singida.
Ameongeza
 kuwa Mkoa utaendelea kuhamasisha wananchi kujiunga na mfuko wa afya ya 
jamii na bima ya afya ili wapate huduma bora hata wakati wakiwa na 
upungufu wa fedha kwani bima huokoa maisha.
0 comments:
Post a Comment