KAIMU Mkuu wa Wilaya ya Iramba, mkoani Singida, Christopher 
Ngubiagai, ameagiza kusimamishwa kazi na kuwafikisha kwenye vyombo vya 
sheria watumishi watatu wa halmashauri hiyo kwa tuhuma mbalimbali, 
ikiwamo matumizi mabaya ya madaraka.
Ngubiagai ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Mkalama, mkoani humo 
alitaja tuhuma nyingine kuwa ni kushindwa kutoa ushauri makini na 
kusababisha upotevu wa fedha na nguvu za wananchi katika ujenzi wa bweni
 la wasichana la shule ya sekondari Kinyangiri wilayani Mkalama.
Aliwataja watumishi hao kuwa ni David Malegi, Mhandisi Msaidizi 
Ujenzi, Hashim Ndwata (Fundi Sanifu) na aliyekuwa Mratibu wa Mradi huo, 
Jeremiah Lubeleje ambaye kwa sasa amehamishiwa wilaya ya Masasi mkoani 
Mtwara.
Alieleza kuwa mradi huo wa ujenzi wa bweni la wasichana ulianza 
Septemba 6, mwaka 2011 wakati wilaya ya Mkalama ikiwa haijagawanywa 
kutoka wilaya mama ya Iramba.
Ngubiagai alisema wafadhili wa mradi huo, Ubalozi wa Japan walitoa 
hundi ya Sh milioni 133.7 kwa ajili ya ujenzi wa bweni hilo ambapo 
halmashauri ilipewa jukumu la kusimamia, kutoa ushauri wa kitaalamu, 
kununua na kuweka vitanda na magodoro ujenzi utakapokamilika.
“Ujenzi wa hosteli hiyo ulikuwa ukamilike Aprili 18, mwaka 2012 
lakini hadi hivi leo ( zaidi ya miaka minne) haujakamilika na jengo 
limekaa bila kutumika, huku wasichana waliopaswa kulitumia wakitembea 
kilometa 14 kwenda na kurudi hali inayowaathiri kitaaluma,” alisema 
Ngubiagai.
Mkuu huyo wa Wilaya alisema kuwa licha ya ujenzi huo kutokamilika 
kama ambavyo mkataba ulielekeza, uongozi wa halmashauri ya Iramba pia 
umeshindwa kukabidhi bweni hilo kwa halmashauri ya wilaya ya Mkalama.
Kutokana na hali hiyo, alisema njia pekee ni kuwasimamisha kazi 
wahusika wa mradi huo ili uchunguzi wa kina ufanyike na ikithibitika 
wamehusika na tuhuma hizo hatua za ukiukwaji maadili ya utumishi wa umma
 zichukue mkondo wake.
Kusimamishwa kwa watumishi hao watatu kunafanya idadi ya 
waliosimamishwa katika halmashauri hiyo hadi sasa kufikia tisa. Februari
 mwaka huu watumishi sita wa Idara ya Afya nao walisimamishwa kwa tuhuma
 ya upotevu wa zaidi ya Sh milioni 145.2 za Mfuko wa Afya ya Jamii 
(CHF).
CHANZO: HABARI LEO 

0 comments:
Post a Comment