Home » » APENDEKEZA MAGARI 10 TU MSAFARA WA RAIS

APENDEKEZA MAGARI 10 TU MSAFARA WA RAIS



Fidelis Butahe, Manyoni
MKAZI wa Kata ya Kintinku, Wilaya ya Manyoni, Hadija Ismail (58) amependekeza Katiba Mpya iwe na kifungu kinachosema misafara yote ya viongozi hususan Rais  iwe na magari yasiyozidi  10 ili kupunguza gharama za uendeshaji.

 Hadija alisema kuwa fedha zinazotumika kugharimia magari zaidi ya 30 yanayokuwa katika msafara mmoja wa Rais, zinaweza kujenga madarasa na kuwalipa fedha ya ziada walimu wanaoishi vijijini.

 
Akizungumza wakati akitoa maoni juu ya Katiba Mpya juzi, Hadija alisema  Katiba Mpya inatakiwa kueleza wazi suala hilo, kwa kuwa fedha za walipa kodi ndiyo zinazotumika kuendeshea magari hayo.
“Rais msafara wake unatakiwa kuwa na magari 10 tu, msafara wa Waziri Mkuu na Makamu wa Rais unatakiwa kuwa na magari matano matano,” alisema Hadija.
Alisema kuwa ni ajabu kwa viongozi wa Serikali kutumia magari mengi katika shughuli zao za kila siku wakati kuna baadhi ya vijiji, wananchi wanatumia jembe la mkono katika shughuli za kilimo.

“Mfano msafara mmoja unakuwa na magari 30, ukipiga hesabu ya gharama ya mafuta kwa magari 20, labda kutoka Dodoma mpaka Singida, zinatosha kabisa kununulia trekta la kilimo” alisema Hadija.
Pia Hadija alisema kuwa viongozi wote wanaochaguliwa na wananchi wanatakiwa kukaa madarakani kwa vipindi viwili tu na siyo kama ilivyo sasa ambapo wapo wabunge wenye miaka zaidi ya 30 bungeni.
“Diwani na mbunge nao wanatakiwa kuwa na vipindi viwili tu vya kugombea kama ilivyo kwa Rais” alisema.

Chanzo: Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa