Mkuu
 wa Mkoa wa Singida Mhandisi Mathew J. Mtigumwe amezindua huduma tembezi
 za madaktari bingwa humo na kuwasihi wananchi kujitokeza kwa wingi 
kupata huduma hizo za kibingwa.
Huduma
 zilizozinduliwa Wilayani Iramba katika hospitali ya Kiomboi zitahusisha
 huduma za za upasuaji, meno, macho, upasuaji wa mifupa, huduma za 
kibingwa za magonjwa ya watoto, wanawake na huduma za mionzi.
Mhandisi
 Mtigumwe amesema matarajio ya mkoa huo ni kuwa huduma tembezi za 
kibingwa zitasaidia kutambua na kutibu magonjwa mbalimbali kabla 
hayajafikia hatua ya usugu na kupunguza gharama za rufaa za wagonjwa 
kwenda nje ya mkoa.
“Huduma
 tembezi za kibingwa zitawasaidia wananchi kutambua uwepo wa huduma za 
kibingwa katika mkoa wa singida na kupata matibabu kwa gharama nafuu” 
alisema Mhandisi Mtigumwe.
Naye
 Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt. John Mwombeki akisoma taarifa ya hali ya afya 
Mkoa wa Singida amesema wazo la kuanzisha huduma tembezi za kibingwa 
limetokana na idadi kubwa ya operesheni zilizofanyika kwa mwaka 
2015/2016 na pia mkutano wa wadau wa afya mkoani hapa kuafiki wazo la 
kuanzisha huduma hiyo.
"Kwa
 kipindi cha mwaka 2015/2016  jumla ya operesheni kubwa na ndogo 4,836 
zimefanyika katika hospitali mbalimbali mkoani hapa, aidha Idara ya 
macho katika hospitali ya Mkoa imefanya jumla ya operesheni kubwa na 
ndogo 2,020" ameongeza Dkt. Mwombeki.
Dkt.
 Mwombeki amesema uwepo wa madaktari bingwa 11 mkoani Singida pia 
umekuwa chachu ya utekelezaji wa huduma hiyo huku Mkoa ukifanya jitihada
 za kuazima madaktari wengine katika mikoa jirani ya Dodoma na Manyara.
Baadhi
 ya wagonjwa waliohudhuria katika siku ya kwanza ya zoezi hilo huku 
huduma hiyo ikitarajiwa kufanyika kwa muda wa siku tano wilayani hapo 
wameeleza shauku na furaha yao ya kusogezewa huduma za kibingwa katika 
halmashauri zao.
"Nilikuwa
 naumwa jino ambalo limeota vibaya, niliambiwa nitaweza kufanyiwa 
operesheni katika hospitali kubwa kama Muhimbili lakini hawa madaktari 
wametusaidia , nimepata huduma haraka na kwa gharama nafuu, nawasihi 
wenzangu waje kwa wingi" amesema Bi Neema Josseph Mkazi wa Kijiji cha 
Kizaga Wilayani Iramba.
 Naye
 Mzazi wa mtoto Jonas Masaka amesema huduma za kibingwa zitamsaidia 
mtoto wake mwenye matatizo ya macho na hiyo kumpunguzia gharama ya 
kumpeleke katika hospitali kubwa kutibu tatizo la macho linalomsababisha
 mtoto huyo kushindwa kusoma vizuri.
Huduma 
 ya tembezi za kibingwa Mkoani Singida zitafanyika katika Wilaya zote 
tano za Mkoa nwa Singida na hvyo kupunguza wagonjwa wa rufaa 
watakaopelekwa hospitali za Bugando, KCMC na Muhimbili.

0 comments:
Post a Comment