Home » » BWANA HARUSI AFARIKI, MKEWE AJERUHIWA AJALINI WAKITOKA KUFUNGA NDOA

BWANA HARUSI AFARIKI, MKEWE AJERUHIWA AJALINI WAKITOKA KUFUNGA NDOA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Imeandikwa na Abby Nkungu, Singida.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Debora Magiligimba
WATU 12 wamekufa na wengine 22 kujeruhiwa katika ajali iliyotokea kijiji cha Ighuka wilayani Ikungi kwenye Barabara Kuu ya Singida – Manyoni baada ya Toyota Hiace walimokuwa wakisafiria kutoka kumchukua bibi harusi kugongana uso kwa uso na Toyota Noah iliyokuwa imepakia watu kutoka msibani.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Debora Magiligimba alisema kuwa ajali hiyo ilitokea juzi saa mbili usiku kwa kulihusisha gari lenye namba za usajili T 581 BBV iliyokuwa ikitokea Singida kwenda Manyoni na T 423 CFF iliyokuwa ikitokea Manyoni kwenda Singida.
Alisema kuwa ingawa uchunguzi wa kina juu ya chanzo cha ajali hiyo bado unaendelea, taarifa za awali zinaonesha kuwa sababu kuu ni mwendo kasi na uzembe wa madereva.
“Baadhi ya majeruhi walituambia dereva wa Toyota Hiace aliyekuwa anatoka Singida mjini alihama kutoka upande wake na kwenda upande wa pili wa barabara ambako aligongana uso kwa uso na Noah iliyokuwa imebeba watu waliokuwa wakitoka msibani na kusababisha vifo vya abiria 10 hapo hapo na majeruhi 24,” alisema.
Mganga Mfawidhi Hospitali ya Rufaa mkoa wa Singida, Dk Ng’hungu Kusenza alisema kuwa majeruhi wawili waliofikishwa Hospitali ya Misheni Puma kwa ajili ya matibabu pia walikufa hivyo kufanya idadi ya watu waliokufa kuwa 12.
Aliwataja waliokufa ambao miili yao imehifadhiwa Hospitali ya mkoa kuwa ni John Duma, Jasson Nsunza, Abubakar Omari, Mary Kinku, Mwanaidi Juma na Husna Juma, Wengine ambao miili yao imehifadhiwa Hospitali ya Misheni Puma wilayani Ikungi ni Ezekiel Joseph, Mussa Daniel, Namtaki Daniel, Hamis Omari, Jumanne Mganga na Wansola Shalua. Habari ambazo hazijathibitishwa zinadai kuwa Bwanaharusi na madereva wa magari yote mawili ni miongoni mwa watu waliopoteza maisha katika ajali hiyo.
CHANZO HABARI LEO 

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa