Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi (katikati) akimkabidhi 
mmoja kati ya wa wakulima wa Pamba wa kijiji cha Kinyangiri Wilayani 
Mkalama kilo kumi za mbegu za zao la pamba zilizotolewa bure na Serikali
 kwa wakulima hao. Kushoto kwa Mkuu wa Mkoa ni Mkurugenzi Mkuu wa 
Mamlaka ya Bodi ya Pamba nchini, Marco Mtunga.
Mkulima wa Pamba Bi Johari kutoka kijiji cha Kinyagiri Wilayani 
Mkalama akibeba mbegu za Pamba kilo kumi alizokabidhiwa na Mkuu wa Mkoa 
wa Singida Dkt Rehema Nchimbi, mbegu hizo zimetolewa bure kwa wakulima 
wa Pamba Mkoa wa Singida.
Mama Devid Mkulima wa Pamba wa Kijiji cha Kinyangiri Wilayani Mkalama
 akijifunza kwa vitendo namna ya kuandaa kamba inayotumika kuonyesha 
vipimo vya upana na urefu katika kupanda pamba badala ya kilimo cha 
mazoea cha kumwaga mbegu bila kufuata kipimo chochote.
Wakulima wa Pamba wa Kijiji cha Lyelembo Wilayani Mkalama 
wakiwasikiliza Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi na Mkurugenzi 
Mkuu wa Mamlaka ya Bodi ya Pamba nchini Marco Mtunga (hawapo pichani) 
kabla ya kupewa mbegu za pamba zilizotolewz bure.
Wakulima wa pamba wa kijiji cha Kinyangiri Wilayani Mkalama 
wakimfuatilia kwa makini mtaalam kutoka Bodi ya Pamba Nchini 
akiwaelekeza namna ya kupuliza dawa ya kuuwa wadudu waharibifu wa pamba,
 viuatilifu hivyo vitatolewa bure na serikali kwa wakulima wote wa pamba
 Mkoani Singida.
Serikali
 imeahidi kutoa bure pembejeo za kilimo kwa wakulima mbali mbali wa zao 
la pamba mkoani Singida kuanzia msimu huu wa kilimo ikiwa ni moja ya 
juhudi za kuhamasisha na kufufua kilimo hicho mkoani hapa.  
Mkurugenzi
 Mkuu wa Mamlaka ya Bodi ya Pamba nchini, Marco Mtunga ameeleza hayo 
juzi katika vijiji vya Kinyangiri na Lyelembo wilayani Mkalama katika 
siku ya kwanza ya ziara yake ya siku mbili kuhimiza Kilimo cha pamba 
mkoani Singida. 
Kwa 
mujibu wa Mkurugenzi huyo, Kampuni ya Biosustain iliyopo mjini hapa 
imepewa jukumu la kuleta na kusambaza mbegu na madawa yote yahusuyo 
kilimo cha pamba bure na kwamba gharama ya pembejeo hizo italipwa na 
Serikali. 
Kutokana
 na hilo, Mkurugenzi huyo amewataka Wakulima kutumia vyema fursa hiyo 
kwa kulima mashamba makubwa zaidi lakini pia kwa kuzingatia tija na 
ubora wa pamba. 
Amesema
 kuwa Wakulima wataweza kufanya hivyo tu iwapo pia watawatumia 
kikamilifu wataalamu wao wa kilimo na kufuata Kanuni na Taratibu za 
kilimo bora. 
“Mmepewa
 upendeleo maalum, kazi yenu sasa ni kulima tu, malipo ya mbegu na 
viuatilifu vyote italipwa na Serikali. Hapa hakuna kisingizio cha 
kushindwa kulima”, amesema Mtunga na kuongeza;
“Pandeni
 vizuri ili wakati mnatumia dawa, kiwango kikubwa cha dawa kisipotee 
bure maana kama hukupanda kwa mstari lazima kutakuwa na ugumu wa 
kupulizia mimea yako. Jengeni utamaduni wa kuwatumia wataalamu wa kilimo
 kama ilivyo kwa wafugaji mifugo yao inapopatwa na maradhi”.  
Aidha, 
amewataka wakulima wa zao hilo kuhakikisha wanang'oa masalia yote ya 
misitu ya pamba na kuichoma moto kwa kuwa, kwa kuacha kufanya hivyo 
wanaruhusu wadudu waliomo kwenye masalia kuendelea kunenepeana na hivyo 
kuhatarisha mazao mapya yanayopandwa.  
Mkurugenzi
 huyo amewasihi wakulima kuacha kuchanganya kilimo cha pamba na mazao 
mengine akisema kuwa tafiti zinaonesha pamba iliyochanganywa na mazao 
mengine hutoa vitumba vitatu tu ikilinganishwa na vitumba 10 kwa kilimo 
cha pamba iliyolimwa peke yake. 
Wakulima
 wa zao hilo wamemueleza Mkurugenzi huyo kuwa, moja ya sababu za kushuka
 kwa uzalishaji pamba kwenye maeneo yao ni pamoja na bei kuwa ndogo kwa 
kisingizio cha Soko la Kimatafa kushuka na kuchezewa mizani wanazotumia 
kupima mazao yao, hali inayowapunja kimapato.  
Hata 
hivyo, wamejibiwa kuwa suluhisho la kuchezewa mizani lipo mikononi mwao 
ili mradi tu wajenge tabia ya kuhoji mara moja wanapoona mambo yanaenda 
isivyo badala ya kusubiri hadi siku ya vikao.
Wakati 
huohuo Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi amewataka watendaji 
wote wa serikali na Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoani Singida kulima 
ekari moja ya pamba kila mmoja ili kuamsha hamasa kwa wananchi wengine.
Dkt 
Nchimbi ameongeza kwa kuwataka watendaji hao kuliweka zao la pamba kama 
ajenga katika vikao vyao, huku akiwataka viongozi wa dini na vikundi vya
 kwaya kuonyesha mfano kwa kulima vizuri pamba.
Ameongeza
 kuwa vijana wanaocheza vijiweni ‘pooltable’ waache mara moja na 
kujikita katika kilimo cha pamba kwa kuwa ni chanzo kikubwa na cha 
uhakika cha kujipatia fedha na hivyo kuchangia kukuza uchumi.
Aidha 
amewataka wakulima wa pamba kuwasikiliza wataalamu na sio kupanda kwa 
mazoea huku akishauri kuwa mikutano yote inayohusu kilimo cha pamba 
ifanyike katika mashamba ya wakulima.
Dkt Nchimbi ameeleza kuwa kauli mbiu mpya ya kilimo cha pamba kwa Mkoa wa Singida ni, ‘Singida Mpya, kwa Pamba yenye Tija’.
0 comments:
Post a Comment