Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
BAADHI ya madiwani katika Halmashauri ya Wilaya Kondoa, wamejitokeza
 kupinga uamuzi uliofikiwa na Baraza la Madiwani wa kulifukuza Shirika 
la Sikika wilayani humo.
Wakizungumza na gazeti hili hivi karibuni, madiwani hao walisema 
uamuzi huo hauna afya kwa maendeleo ya wilaya hiyo, kwani shirika hilo 
lilikuwa likisaidia kuonyesha udhaifu uliopo katika idara ya afya.
Kwa mujibu wa madiwani hao, uamuzi wa shirika hilo kufukuzwa ulianza 
kutengenezewa mazingira kwa madiwani wa CCM kufungwa na msimamo wa 
kichama juu ya shirika hilo.
Diwani wa Kata ya Kondoa Mjini, Hamza Mafita (CCM), alisema Sikika ni
 jicho la pili ambalo kama lingetumiwa vizuri lingeweza kuwasaidia 
madiwani kuona uchafu mahala ambapo wameshindwa kuufikia.
“Kuhusu Sikika mimi nilijua shirika hili litafukuzwa tu kwa sababu ya
 viongozi wetu kupenda kulinda ufisadi. Katika bajeti ya mwaka 2012/2013
 miradi ya afya shughuli namba 12 ilitengewa bajeti ya sh milioni 17 kwa
 ajili ya kukarabati vizimba vya kuchomea takataka.
“Ilikuwa ni kwa ajili ya vituo vya afya vya Hamai na Mrijo. Kizimba 
cha Hamai kilijengwa chini ya kiwango thamani yake hata milioni mbili 
hakifiki, Mrijo kule hicho kizimba chenyewe hakipo,” alisema.
Diwani wa Viti Maalumu, Hija Suru (CCM), alisema uamuzi wa shirika 
hilo kufukuzwa ulikuwa na msukumo ndani yake wenye sura inayotiliwa 
shaka dhidi ya madiwani.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Suruke, Jafari Ganga (CUF) alisema
 uamuzi huo ulifanywa na madiwani wa CCM lakini madiwani wa upinzani 
walipiga kura ya kukataa shirika hilo kufukuzwa.
“Kikao  cha Julai 26 kilihudhuriwa na madiwani 36 madiwani 26 wa CCM 
walishikizwa kupiga kura ya kuiondoa Sikika madiwani 10 wa upinzani 
tulikataa,” alisema.
Wakijibu madai hayo, Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Hisdory Mwalongo
 na Mwenyekiti wa halmashauri, Khamis Mwenda walitetea msimamo wao na 
kusema kuwa hatua zilizochuliwa dhidi ya shirika hilo ni sahihi.
Chanzo;Tanzania Daima  
0 comments:
Post a Comment