Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Hakuna ubishi waandishi wa habari wana nafasi kubwa sana ya 
kuipatia jamii viongozi bora na sio bora viongozi, kama wataweka mbele 
uzalendo na kuacha kuchukua hongo kutoka kwa wagombea kwenye Uchaguzi 
Mkuu wa 2015.
Nafahamu wapo waandishi wengi wenye uadilifu, 
lakini kwa sababu kwenye msafara wa mamba na kenge wamo, si ajabu kukuta
 ambao njaa yao ya muda mfupi inatupatia viongozi wabovu.
Kipindi cha uchaguzi ni wakati ambapo baadhi yetu 
tunajulikana thamani zetu. Wapo wa Sh20,000, wengine Sh50,000, pia wa 
Sh100,000 na wale wanaopewa hongo zaidi ya kiasi hicho.
Hongo hizi wanazopokea ili kumpamba mgombea kuliko
 uhalisia wake, zimekuwa na athari kubwa kiuchumi, kisiasa na kijamii 
ikiwamo kupata viongozi wasiofaa na wanaotanguliza masilahi yao binafsi 
mbele.
Sote tunafahamu Uchaguzi Mkuu wa 2005 na 2010 
namna ambavyo tuliwapamba baadhi ya wagombea wakiwamo wa ubunge, 
tukawaaminisha wapigakura wakawachagua, lakini leo wanajuta. Natamani 
utaratibu ule wa zamani urejee, kwamba kama wananchi walikuwa na hitaji 
la kiongozi walimtafuta wenyewe na kumuomba ili agombee, leo mtu 
anagombea tena kwa kuhonga wapigakura.
Mwaka huu huenda tukawa na uchaguzi wa Serikali za
 mitaa, lakini mwakani tukawa na uchaguzi mkuu wa Rais, wabunge na 
madiwani watakaotuongoza kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.
Ni kipindi ambacho thamani ya waandishi wa habari 
hupanda kwa kipindi kifupi sana na kisha wanasiasa wakishaingia 
madarakani, huwatelekeza kama mafundi wanavyotumia karai la zege.
Nafahamu asilimia 75 ya wanahabari wote nchini ni 
wa kujitegemea ambao kimsingi wanalipwa kulingana na habari ama makala 
zitakazochapwa au kutangazwa na vyombo vya habari.
Ni ukweli malipo haya ni kidogo, lakini hiyo 
haiwezi kuhalalisha baadhi yetu kujiingiza katika vitendo vya kupokea 
hongo kutoka kwa wagombea ili tu wawaandike vizuri hata kama hawafai.
Maadili ya Uchaguzi Mkuu 2010 kwa wanahabari 
yaliweka sharti la lazima kwa wanahabari kuwahabarisha na kutoa elimu ya
 uraia kwa wapigakura ili wafanye uamuzi sahihi wakati wa kupiga kura.
Uamuzi sahihi ni kwa wapigakura kuchagua viongozi 
bora na siyo bora viongozi kwa sababu tu amepandishwa chati na 
wanahabari wakati dhamira yake ni kwenda kuchuma na si kusaidia jamii.
Wakati tunajiandaa na chaguzi nilizozisema, tayari
 wapo wagombea ambao wamekuwa ‘mzigo’ lakini wanajiandaa kufanya kila 
njia ili waweze kurudi tena bungeni kwa kipindi kingine.
Kuna taarifa zisizo rasmi baadhi yao wametenga hadi Sh200 
milioni na sehemu ya fedha hizo imetengwa kwa ajili ya wanahabari 
wasioheshimu maadili ili wawasafishie njia hata kama hawafai.
Wanahabari tunapaswa kuanza kujitafakari sasa kama
 tumefanya nini kulisaidia taifa kupata viongozi bora, wazalendo na 
wenye dhamira ya dhati ya kuwaletea Watanzania maendeleo.
Haiwezekani leo hii tuna rasilimali kibao kuanzia 
madini ya kila aina, vivutio vya utalii, nishati ya gesi, wingi wa 
misitu na mazao ya baharini lakini Tanzania inakuwa miongoni mwa nchi 
maskini.
Hapa ni lazima tutafakari kauli ya Baba wa Taifa, 
Hayati Mwalimu Julius Nyerere kuwa ili nchi iendelee inahitaji vitu 
vinne navyo ni ardhi, watu, siasa safi na uongozi bora. Ninasema 
tutafakari ni kipi tunachokikosa kati ya vitu hivyo vinne hadi 
Watanzania waendelee kuwa maskini licha ya kuwa moja ya nchi 
zinazoongoza barani Afrika kwa kuwa na rasilimali nyingi.
Hakuna ubishi tuna tatizo la uongozi ndio maana 
hatufiki kule tunakotaka kwenda na wanahabari wanalo jukumu zito la 
kuirudisha nchi hii kwenye mstari.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment