Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
ZAIDI ya wanawake 9,000 mkoani Singida wamegundulika kuwa wamekeketwa katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Daktari Bingwa wa Ushauri wa magonjwa ya Wanawake na Uzazi mkoani 
hapa, Suleiman Mutani aliyasema hayo kwenye Jukwaa la Kitaifa la 
kuadhimisha Siku ya kupinga ukeketaji lililofanyika mjini hapa.
Dk Mutani alisema, idadi hiyo ya waliokeketwa ni sawa na asilimia 
20.8 ya wanawake wote waliokwenda kujifungua kwenye vituo mbalimbali vya
 kutolea tiba mkoani humu, kati ya Januari 2013 na Desemba mwaka jana.
“Wanawake 9,386 walibainika kufanyiwa ukeketaji, jambo ambalo ni 
kinyume cha sheria na ni ukiukwaji wa misingi ya haki za binadamu, licha
 ya kuwa na madhara makubwa ya kiafya” alisema Dk Mutani.
Alitaja madhara yatokanayo na ukeketaji kuwa ni pamoja na kuwa na 
uzazi pingamizi wakati wa kujifungua, wanawake kupata shida wakati wa 
hedhi, uwezekano wa kupata fistula, kuugua maradhi ya kujamiiana na 
kuhisi maumivu makali wakati wa tendo la ndoa.
Dk Mutani alisema pia kuwa madhara hayo ni matokeo hasi yasababishwayo na jamii husika kuendelea kukumbatia mila hiyo potofu .
Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake 
(Tamwa), Edda Sanga alisema, madhumuni ya jukwaa hilo ni kutoa fursa kwa
 wadau kujadili kwa kina utekelezaji wa maazimio ya miaka iliyopita na 
kupanga mikakati na njia bora zaidi za kukabiliana na mbinu mpya za 
ukeketaji.
Alitaja mikoa ambayo ni vinara wa ukeketaji na asilimia kwenye mabano
 kuwa ni Manyara (71), Dodoma (64), Arusha (59), Singida (51) na Mara 
(40).
Mikoa mingine ambayo pia inahusishwa na ukeketaji kutokana na watu wa
 makabila yanayoendesha vitendo hivyo kuhamia, ni Dar es Salaam, Pwani 
na Morogoro.
Hata hivyo, wadau waliohudhuria kikao hicho walisema kuwa, pamoja na 
mikakati mbalimbali, mbinu bora zaidi ni kuwawezesha ngariba kuwa na 
miradi ya kipato mbadala ili waache biashara ya kukeketa.
Aidha, walishauri wazee wa kimila katika maeneo husika wahusishwe 
kikamilifu katika vita dhidi ya ukeketaji kwa sababu wanaheshimika zaidi
 na wana ushawishi mkubwa kwa jamii.
Jukwaa hilo la siku mbili lililoandaliwa na Tamwa, limefadhiliwa na 
Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya Watu (UNFPA). 
Lilihudhuriwa na wadau kutoka mikoa minane ambayo baadhi ya makabila 
yake yanaendesha ukeketaji.
CHANZO: HABARI LEO. 

0 comments:
Post a Comment