Home » » DKT NCHIMBI ASHAURI WAHADZABE WAPEWE AJIRA ZA MUDA KUPITIA TASAF.

DKT NCHIMBI ASHAURI WAHADZABE WAPEWE AJIRA ZA MUDA KUPITIA TASAF.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi ameshauri Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini (TASAF) uanzishe kazi za ajira za muda, kwa walengwa wa Mpango huo kutoka jamii ya Wahadzabe waliopo Wilayani Mkalama ili uwasaidie kuinua uchumi wao.
Dkt Nchimbi ametoa ushauri huo mara baada ya kutembela kijiji cha Singa Wilayani Mkalama na kuona bwawa litakalotumika kuhifandhi maji ya mvua kwa ajili ya shughuli mbalimbali lililojengwa na walengwa wa Tasaf Kijijini hapo kisha kutembelea kijiji cha Munguli Kata ya Mwangeza Wilayani  humo aliposhuhudia malipo ya walengwa wa kihadzabe wa Mpango wa Tasaf.
Ameeleza kuwa jamii ya wahadzabe hawana mradi unaohusisha kazi za ajira za muda ambazo zimekuwa zikisaidia katika kuongeza kipato, kuwafundisha thamani ya kazi pamoja na kutekeleza miradi ambayo imekuwa ikisaidia jamii nzima kama vile mabwawa na  barabara.
“Nashauri TASAF kabla ya msimu huu wa mvua kuisha muwaletee na hawa wahadzabe mradi wa ajira za muda kama ambavyo walengwa wa vijiji vingine wamekuwa wakifanya kazi hizo na zimekuwa zikichangia maendeleo kwa vijiji vyao”, ameeleza na kuongeza kuwa,
“Miradi ya ajira za muda zitawafundisha Wahadzabe kujituma kufanya kazi ambazo zinachangia maendeleo ya jamii huku kazi hizi zikiwa kama darasa la wao kujifunza kwa vitendo kuwa kama anaweza kwa mfano kushiriki kujenga bwawa basi anaweza kufanya jambo kubwa katika familia au maisha yake”, amesisitiza Dkt Nchimbi.
Aidha ametoa tahadhari kwa walengwa hao wa kihadzabe kuwa wasitumie pesa wanayopewa kwa kunywa pombe badala yake pesa hiyo itumike sawasawa na maelekezo ya mpango huo na hatua zichukuliwe kwa wale watakaokaidi.
Kwa upande wake Afisa Ufuatiliaji Kutoka Tasaf Makao Makuu Anna Njau ambaye aliambatana na Mkuu wa Mkoa Dkt Nchimbi katika ziara yake ameeleza kuwa ushauri huo ni mzuri na una lengo la kuwasaidia wananchi kama ambavyo Tasaf imekuwa na lengo la kuinua jamii hasa kaya masikini hivyo wazo hilo ataliwasilisha makao makuu kwa ajili ya utekelezaji.
Baadhi ya wahadzabe waliofika kupokea fedha za Mpango wa Tasaf wameeleza kuwa fedha hizo zimewasaidia kuwainua kiuchumi kwa kuhakikisha wana chakula cha kutosha, watoto wameenda shule, watoto wadogo wamepelekwa kliniki huku wakijiendeleza zaidi kiuchumi kwa ufugaji mdogo wa kuku na mbuzi pamoja na kuboresha makazi yao.
Jamii ya Wahadzabe waliopo Kijiji cha Munguli na hasa kitongoji cha Kipamba Wilayani Mkalama wamekuwa wakiishi kwa kutegemea uwindaji wa wanyama pori, kula asali, ubuyu, matunda na mizizi mbalimbali ambapo juhudi za Serikali kupitia Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini (Tasaf) umesaidia jamii hiyo kuanza kupeleka watoto shule, kuanzisha shughuli za uzalishaji mali kama vile kilimo na ufugaji.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa