Picha/habari na Nathanieli Limu-Singida
Waziri
 Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassimu Majaliwa Kassim amesema
 kuna haja ya kuangalia upya mfumo wa elimu ya juu nchini ili kuuboresha
 uweze kusaidia kutayarisha haraka rasilimali watu walioelimika  zaidi, 
watakaoliwezesha  taifa kuwa na maendeleo na kufikia uchumi wa kati 
ifikapo mwaka 2025. 
Waziri
 Mkuu Majaliwa ameyasema huyo jana wakati akizungumza kwenye kilele cha 
mahafali ya 33 ya Chuo Kikuu huria cha Tanzania yaliyofanyika kwenye 
viwanja vya Kanisa Katoliki mjini Singida. 
“Kwa
 kuzingatia malengo ya dira ya taifa ya maendeleo na mwelekeo wa 
serikali ya awamu ya tano, napenda nisisitize kuwa dira ya utendaji wenu
 ijikite katika maeneo yaliyoainishwa chini ya mwamvuli wa kauli mbiu ya
 chuo-elimu bora na nafuu kwa wote”, amesema.  
Amesisitiza
 kwa kusema kwa uchumi wa kati na wa viwanda, hauwezi kufikiwa au kuwa 
endelevu pasipo kuwa na kiwango cha udahili katika elimu ya juu cha 
angalau asilimia 23.  
“Hivi
 sasa kiwango cha Tanzania cha udahili katika elimu ya juu ni aslimia 
nne (4). Kiwango hiki ni kidogo hata kuliko nchi kama Jamhuri ya 
Kidemokrasia ya Kongo ambao licha ya hali ya vita nchini mwao kwa muda 
mrefu,wamefikia asilimia saba (7)”,amefafanua.
Waziri
 Mkuu Majaliwa amefafanua zaidi kwa kusema kuwa takwimu zinaonyesha 
kwamba karibu nchi zote washiriki katika jumuiya ya Afrika mashariki, 
ukiacha Burundi, zina viwango vya juu zaidi vya udahili katika elimu ya 
juu ikilinganishwa na kiwango cha Tanzania.  
Amesema
 kwa mujibu wa sera ya elimu ya mwaka 2014 mfumo wa elimu na mafunzo 
umetawaliwa na muundo wa kitaaluma wenye dhana ya kuchuja wahitimu kwa 
kila ngazi ili kupata wachache wenye uwezo mkubwa katika taaluma. 
“Hali
 hii inatokana na nafasi za elimu na mafunzo ngazi za juu kuwa chache 
kadri wanafunzi wanavyohitimu kuanzia ngazi ya elimu ya msingi 
na kuendelea. Kwa uhaba wa nafasi za elimu ya juu na ufinyu wa bajeti 
ndio unaosababisha kutumia muundo wa kuchuja badala ule wa kutoa 
fursa kulingana na uwezo, vipaji na vipawa”, amesema na kuongeza; 
“Huu
 ndio mfumo ambao unahitaji kuhuishwa na mfumo wa elimu huria na masafa 
kama alivyoeleza Waziri wa Elimu, Sayansi na Tekinolojia Profesa Joyce 
Ndalichako kwamba mazingira, vigezo na masharti ya mchakato huu 
vimeainishwa katika sera ya elimu na mafunzo 2014’.  
Wakati
 huo huo, Waziri Mkuu Majaliwa amesema serikali inaunga mkono azma ya 
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ya kuanzisha dawati maalum kwa 
ajili ya kuimarisha mfumo wa elimu huria na masafa. 
“Kupitia
 hafla hii, ninaagiza dawati kama hili lianzishwe pia katika Tume ya 
vyuo vikuu (TCU) na Baraza la elimu ya ufundi (NACTE), kwa lengo la 
kuhakikisha kuwa taratibu zao za ithibati zinazingatia na kukidhi 
matakwa ya viwango vya mfumo wa elimu huria na masafa”, amesema. 
Katika
 Mahafali hayo Mkuu wa Chuo Kikuu Huria na Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo 
Peter Pinda amemtunuku shahada ya heshima ya uzamivu Balozi Nicolous 
Kuhanga ambaye mchango wake umetajwa kuwa mkubwa hasa wakati wa 
kuanzishwa kwa chuo hicho.
Zaidi
 ya wahitimu 2200 wamehitimu katika Chuo Kikuu hicho na kutunikiwa 
shahada mbalimbali ambapo mke wa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Mama Mary 
Majaliwa, amekuwa miongoni mwa wahitimu akitunukiwa shahada ya uzamili 
katika Elimu ya Utawala, Mipango na Sera.
0 comments:
Post a Comment