Picha juu na chini ni Mbunge wa jimbo
 la Singida mjini, Mh. Mohammed Gullam Dewji akihutubia wananchi kwenye 
mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye kituo cha mabasi cha zamani mjini 
Singida.
Baadhi ya wananchi waliohudhuria 
mkutano wa hadhara ulioitishwa kwa ajili ya mbunge wa jimbo la Singida 
mjini Mh. Mohammed Gullam Dewji kuzungumza na wananchi wa jimbo lake.
Mbunge wa jimbo la Singida mjini, Mh.
 Mohammed Gullam Dewji, akiwa anasalimiana na Wana CCM na wananchi wa 
Singida mjini kwenye kituo cha mabasi cha zamani mjini Singida.
Na Nathaniel Limu.
Mbunge wa Singida mjini (CCM) Mh. 
Mohammed Gullam Dewji amemwaga misaada mbalimbali ikiwemo kuwaongezea 
mitaji wauza kahawa chungu, ambayo haijawahi kutolewa jimboni humo na 
mbunge au mfadhili yeyote kwa wakati mmoja, kabla na baada ya Tanzania 
kupata uhuru.
Misaada hiyo yenye thamani ya zaidi 
ya shilingi milioni 87.9, ni pamoja na mabati 100 na mifuko ya saruji 
100, kwa kila shule 17 za sekondari jimboni humo.
Misaada mingine ni vyereheni viwili kwa kila kata 19  na cherehani moja kwa kila tawi la CCM jimboni humo.
Pia vikundi 16 vya wajasiriamali 
vikiwemo vya kung’arisha viatu, mafundi baiskeli, wapiga debe wa vituo 
vya mabasi, wasukuma matoroli, wakereketwa wa mashina ya CCM, 
watengeneza viatu vya kienyeji na baba, mama lishe, kila kimoja 
kimeongezewa mtaji wa shilingi 500,000 taslimu.
Vifaa hivyo na mitaji ya biashara, 
vimetolewa kwenye mkutano  wa hadhara uliofanyika kwenye kituo cha 
zamani cha mabasi mjini Singida.
Akizungumza kwenye mkutano huo wa 
hadhara uliohudhuriwa na maelfu ya wana-CCM na wananchi kwa ujumla, Mh. 
Dewji amesema msaada huo ni mwendelezo wa misaada yake anayoitoa kwa 
ajili ya kuiunga mkono serikali katika kuwatumikia wananchi.
Amesema pia kuwa misaada hiyo ni 
sehemu yake ya utekelezaji wa ilani ya CCM  katika kuwatumikia wananchi 
wa jimbo la Singida mjini.
Amesema “Tunatakiwa tujitume usiku na
 mchana, ili tuhakikishe  kila tuliyoyaahidi kwenye ilani yetu, yote 
tumeyakamilisha, vinginevyo wananchi hawatatuelewa. Wananchi wanahitaji 
utimilifu wa ahadi na sio uhodari wa  kujieleza kwenye majukwaa”.
Katika hatua nyingine, Mh. Dewji 
ametumia fursa hiyo kuwaomba viongozi na watendaji kuendelea na moyo 
safi wa kuwatumikia wananchi bila kuchoka.
Amesema pia wawe waaminifu na 
waadilifu kwa wananchi na waongozwe kwa dhamira iliyo njema, yenye 
uzalendo wa kuipenda nchi yetu na watu wake.
Mbunge Dewji amesema “Tuendelee 
kuhubiri amani na utulivu kwenye majukwaa, wakati wote tuwaelekeze 
wananchi kwenye kujiletea maendeleo endelevu ya wakati huu na wakati 
ujao”.
0 comments:
Post a Comment