Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Ukibahatika kuutembelea Mkoa wa Singida na kurejesha kumbukumbu 
zako miaka 10 nyuma unaweza usiamini yanayotokea hivi sasa kwenye mkoa 
huo. Unaweza kushangaa na kujiuliza maswali mengi jinsi mkoa huo 
unavyobadilika na kuvutia watu wengi sasa.
                
              
Singida sasa wamejenga nyumba za kisasa, barabara 
za lami na wakazi wake wameongeza uzalishaji wa zao la alizeti, karanga 
na vitunguu na hivyo kuinua kipato cha mtu mmoja mmoja.
                
              
Uzalishaji wa mazao ya biashara; alizeti, pamba na
 vutungu umeongezeka kwa kasi ukilinganisha na miaka minane iliyopita 
kwa mfano, mwaka 2007 Mkoa wa Singida ulivuna tani 28, 000 za alizeti 
wakati mwaka 2012 Singida ilivuna tani 202,000 za zao hilo.
                
              
Ukuaji na kuwapo kwa mabadiliko ya kiuchumi katika
 mkoa huo hasa kuongezeka kwa pato la mtu mmoja mmoja kunachangiwa na 
shughuli za kilimo, ufugaji na ujenzi wa barabara ya lami ambayo 
imekamilika mwaka 2007.
                
              
“Pato la mtu mmoja, mkoani Singida, kabla ya mwaka
 2007 lilikuwa Sh280,000 kwa mwaka, sasa ni Sh650,000 kwa mwaka,” 
anasema Liana Hassan, Katibu Tawala wa mkoa huo.
                
              
Mabadiliko yalivyotokea
                
              
Mabadiliko hayo hajatokea kirahisi kwenye mkoa huo
 bali mambo mengi yamebalika kutokana na juhudi za Mkuu wa Mkoa wa 
Singida, Dk. Parseko Kone na Benki ya Dunia (WB) ambayo imetoa mkopo wa 
Sh44.506 bilioni kwa Serikali ya Mkoa wa Singida.
                
              
Mradi wa ujenzi wa kilometa 109 ya barabara 
kuanzia Singida mpaka Shelui kupitia Mlima wa Sekenke, uko chini ya 
Central Transport Corridor Project (CTCP). Wakala wa Barabara nchini 
(Tanroads), Mhandisi Yustaki Kangolle anasema Barabara ya Singida hadi 
Shelui imejengwa katika awamu tatu; kuanzia Singida hadi Iguguno, awamu 
ya pili Iguguno hadi Sekenke na Sekenke hadi Shelui.
                
              
Ujenzi wa barabara hiyo umewavutia wakazi wa mkoa 
huo kuongeza bidii katika kilimo cha alizeti na kununua na kuanzisha 
viwanda vidogo vya kukamua mafuta kutokana na fursa ya kusafirisha kwa 
wingi mafuta hayo jijini Dar es Salaam, Arusha na mkoani Kilimanjaro.
                
              
Mwitikio wa wananchi wa Singida kupenda kulima na 
kutekeleza maagizo ya Serikali ya Mkoa wa Singida chini Dk. Kone 
wameleta mabadiliko kilimo cha alizeti na kusababisha kuongezeka kwa 
viwanda vya kukamua mafuta.
                
              
Kutokana na juhudi za wakulima, Ofisa Mtendaji wa 
TCCIA wa mkoa huo, Calvent Nkulu anabainisha kuwa miaka saba iliyopita 
kulikuwa na viwanda 50 vya kukamua mafuta, lakini sasa kuna viwanda 120 
mkoani Singida.
                
              
“Kutokana na kipato cha wananchi kuongezeka, 
tumewahamasisha wajenge nyumba za kisasa badala ya nyumba za tembe. 
Wananchi wanapata urahisi wa kusafirisha vifaa vya ujenzi kutoka Singida
 mjini hadi vijijini,” anaeleza mkuu wa mkoa huo.
Mazao ya biashara yanasafirishwa hadi nchi za jirani; Rwanda, 
Kenya, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na mazao ya 
chakula kwa mfano, samaki, maparachichi yanasafirishwa na kuuzwa jijini 
Dar es Salaam kutoka mkoani Mwanza na Rwanda.
“Biashara imekua hapa Singida, wafanyabiashara 
wanatoka Kenya kwa ajili ya kununua vitungu na kuku, Singida ya leo siyo
 ile ya zamani,” anasema Julius Madebwe ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa 
Kitengo cha Biashara mkoani Singida.
Mkoa huo sasa umekuwa na maendeleo makubwa ya 
shughuli za ujenzi wa nyumba za kisasa kutokana na kuwapo kwa barabara 
hiyo na kukua kwa shughuli za kilimo baada ya kuwapo kwa mvua za 
kutosha.
Biashara ya mafuta ya alizeti imepata soko kubwa 
nchini na kuwavutia watu wengi kuifanya akiwamo Mhandisi Mstaafu wa 
Wakala wa Barabara nchini, John Shailla ambaye ananunua mbegu za alizeti
 Wilaya ya Bariadi na kuzikamua kwenye mashine yake na kuuza kwa walaji.
Jambo kubwa la kujivunia kwa wakazi wa Singida ni 
bidhaa mbalimbali zinazosafirishwa kutoka nchini Rwanda kwa mfano, 
maparachichi na maharagwe hivi sasa yanauzwa sokoni mkoani Singida 
tofauti na awali magari ya mizigo yalikuwa yakikwama njiani.
Baada ya kukamilika kwa barabara hiyo, mkazi wa 
Shelui katika mkoa huo, Mohamed Hassani anasema kuwa ajali zimeongezeka 
kwenye Mlima wa Sekenke na baadhi ya wananchi wameiomba Serikali 
iwaruhusu madereva watumie barabara ya zamani wakati wa kuteremka mlima 
huo.
Baadhi ya wakazi wa Kata ya Iguguno, Misigiri, 
Ulemo na Kijiji cha Kyengege akiwamo dereva wa malori ya mizigo, Henry 
Michael na mkulima wa Kata ya Iguguno, Hatibu Sambai wanapendekeza 
kuwekwa kwa alama za barabarani katika maeneo muhimu ya pembezoni mwa 
barabara ambako kuna shule, hospitali na miji midogo ili kupunguza 
ajali.
Wakazi wa wengi wa kata hizo wameshangazwa na 
barabara hiyo kuharibika mapema na kuwa mashimo mengi huku wakiitupia 
lawama Tanroads kwa kuitengeneza barabara hiyo chini ya kiwango na 
kutoweka mitaro ya kupitisha maji wala barabara za waendesha baiskeli, 
pikipiki na barabara ya waenda kwa miguu.
“Matatizo ni mengi kwenye barabara hii, haina 
mitaro ya kupitisha maji na matokeo yake maji yanaingia kwenye makazi ya
 watu,” anabainisha Nikodemmonti Maigai, mkazi wa Kijiji Kyengege.
Hata hivyo mkazi wa kijiji hicho, Josephat Mginza 
anawalaumu Tanroads kwa kuwa hawawashirikishi wakazi wa Singida wakati 
wa kutengeneza barabara na matokeo yake kusababisha wananchi wengi 
kulalamika kutokana na kupoteza fursa za biashara zilizokuwapo pembezoni
 mwa barabara.
Kutokana na kuwapo kwa kasoro hizo Meneja wa 
Tanroads mkoani Singida, Mhandisi Kangole alikiri kwamba barabara hiyo 
imejengwa chini ya kiwango kwa kuwa fedha walizopata hazikutosheleza 
kujenga barabara ya kiwango cha juu.
“Barabara hii imejengwa kwa kiwango cha TLC 10- ni
 aina ya barabara ya kiwango cha chini. Sasa tunafikiria kuweka lami juu
 ya hii ya sasa na kilometa moja ya barabara ya milimita 50 inaweza 
kugharimu Sh600 mpaka Sh800 milioni,” anabainisha Mhandisi Kangole.
Kutowekwa kwa alama za barabarani na vibao, Mhandisi Yonennes 
Mbegalo anabainisha kwamba ni tatizo linalosababishwa na baadhi wananchi
 ambao wanaviiba na hivyo amewataka kuvilinda vibao hivyo.
Wakati Mhandisi Kangole akisema hayo Mhandisi 
Masige Matari anatoa sababu za kuharibika kwa barabara hiyo kwamba wingi
 wa magari ya mizigo umesababisha kuwapo mashimo.
“Kabla ya Barabara ya Singida hadi Shelui kuwekwa 
lami, malori ya mizigo 117 yalikuwa yakitumia barabara hii kwa siku, leo
 yanapita malori 1,135 kwa siku kwenda Rwanda, DRC, Kagera na Mwanza.
Baadhi ya wananchi wanapongeza jitihada hizo 
wakisema kuwa ikiwa harakati za maendeleo zitaendelea mkoa huo unaweza 
kuwa na maendeleo ya kasi zaidi.
Chanzo;mwananchi