Home » » MAJI YAWANUFAISHA NG'ANG'ULI

MAJI YAWANUFAISHA NG'ANG'ULI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
WANANCHI zaidi ya 3,000 wa Kijiji cha Ng’ang’uli, Kata ya Ulemo, wilayani Iramba, Mkoa wa Singida,  wamenufaika na huduma ya maji safi na salama baada ya mradi wa maji ya bomba kukamilika kujengwa na kuanza kutumika.
Mjumbe wa Kamati ya Mradi wa Maji ya Kijiji hicho, Paulo Saida, aliyasema hayo hivi karibuni katika taarifa ya utekelezaji wa mradi huo wakati wa uzinduzi wa bomba la maji uliofanyika katika kijiji hicho.
Alisema lengo la mradi huo ulioanza kutekelezwa Agosti 15, 2013 na kukamilika Februari 15, mwaka huu, ni kuboresha afya za wananchi 3,669 kwa kuwapatia huduma ya maji safi na salama karibu na maeneo wanayoishi na kwa njia endelevu.
Saida alisema historia ya mradi huo ilitokana na wananchi wa kijiji hicho kuuchagua mpango huo uwe kipaumbele chao kutokana na shida ya maji iliyokuwa ikiwakabili.
Kwa mujibu wa mjumbe huyo, gharama za mradi huo wa bomba la maji ni sh 312,945,550; zikiwemo fedha za nje sh 307,245,550 na michango ya wananchi sh 5,700,000.
“Shughuli zilizofanyika kutokana na fedha hizo ni pamoja na kujenga tenki lenye ujazo wa lita 45,000, kujenga nyumba moja ya mtambo wa kusukuma maji, kujenga vituo 11 vya kuchotea maji, kujenga malambo mawili ya kunyweshea maji mifugo, kujenga choo bora kimoja, kujenga tenki la kuvuna maji ya mvua lenye ujazo wa lita 5,000 na kufyatua mtungi wa kuvuna maji ya mvua wenye ujazo wa lita 1,000.
“Pia zimetumika kujenga tenki la lita 3,000, kuchimba mitaro na kufunga bomba lenye urefu wa mita 11,487, kununua na kufunga mtambo wa kusukuma maji, kuwapatia semina na mafunzo wananchi kuunda na kusajili vikundi vya watumia maji kwenye vituo na jumuiya ya watumiaji wa maji (Juhudi Cowsco),” alifafanua mjumbe huyo.
Akizungumzia faida za mradi huo, alisema ni  kupungua kwa magonjwa yanayotokana na maji yasiyo salama, muda wa shughuli za kiuchumi utaongezeka na hatimaye kipato kitaongezeka kwa wakazi wa kijiji hicho.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba,  Halima Mpeta, katika taarifa yake ya utekelezaji wa Programu ya Maji na Usafi wa Mazingira, alisema lengo la programu hiyo ni kusambaza huduma ya maji safi na salama kwa wakazi 77,015 wakiwemo 45,470 wa Wilaya ya Mkalama na 31,545 wa Iramba ifikapo mwaka 2015.
Utekelezji wa Programu ya Maji na Usafi wa Mazingira awamu ya kwanza katika Halmashauri ya Wilaya ya Iramba ulianza mwaka 2008/2009 ambapo vijiji 13 vya Iramba na Mkalama viliingia, wakati huo ilikuwa ikitambulika kama Wilaya moja ya Iramba.
Chanzo:Tanzani Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa