Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
WANANCHI zaidi ya 3,000 wa Kijiji cha Ng’ang’uli, Kata ya Ulemo,  
wilayani Iramba, Mkoa wa Singida,   wamenufaika na huduma ya maji safi 
na salama baada ya mradi wa maji ya  bomba kukamilika kujengwa na kuanza
 kutumika.
  Mjumbe wa Kamati ya Mradi wa Maji ya Kijiji hicho, Paulo Saida,  
aliyasema hayo hivi karibuni katika taarifa ya utekelezaji wa mradi huo 
wakati  wa uzinduzi wa bomba la maji uliofanyika katika kijiji hicho.
  Alisema lengo la mradi huo ulioanza kutekelezwa Agosti 15, 2013 na  
kukamilika Februari 15, mwaka huu, ni kuboresha afya za wananchi 3,669 
kwa  kuwapatia huduma ya maji safi na salama karibu na maeneo wanayoishi
 na kwa njia  endelevu.
  Saida alisema historia ya mradi huo ilitokana na wananchi wa kijiji  
hicho kuuchagua mpango huo uwe kipaumbele chao kutokana na shida ya maji
  iliyokuwa ikiwakabili.
  Kwa mujibu wa mjumbe huyo, gharama za mradi huo wa bomba la maji ni  
sh 312,945,550; zikiwemo fedha za nje sh 307,245,550 na michango ya 
wananchi sh  5,700,000.
  “Shughuli zilizofanyika  kutokana na fedha hizo ni pamoja na kujenga 
tenki lenye ujazo wa lita 45,000,  kujenga nyumba moja ya mtambo wa 
kusukuma maji, kujenga vituo 11 vya kuchotea  maji, kujenga malambo 
mawili ya kunyweshea maji mifugo, kujenga choo bora  kimoja, kujenga 
tenki la kuvuna maji ya mvua lenye ujazo wa lita 5,000 na  kufyatua 
mtungi wa kuvuna maji ya mvua wenye ujazo wa lita 1,000.
  “Pia zimetumika kujenga tenki  la lita 3,000, kuchimba mitaro na 
kufunga bomba lenye urefu wa mita 11,487,  kununua na kufunga mtambo wa 
kusukuma maji, kuwapatia semina na mafunzo  wananchi kuunda na kusajili 
vikundi vya watumia maji kwenye vituo na jumuiya ya  watumiaji wa maji 
(Juhudi Cowsco),” alifafanua mjumbe huyo.
  Akizungumzia faida za mradi huo, alisema ni  kupungua kwa magonjwa 
yanayotokana na maji  yasiyo salama, muda wa shughuli za kiuchumi 
utaongezeka na hatimaye kipato  kitaongezeka kwa wakazi wa kijiji hicho.
  Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba,  Halima Mpeta,
 katika taarifa yake ya  utekelezaji wa Programu ya Maji na Usafi wa 
Mazingira, alisema lengo la  programu hiyo ni kusambaza huduma ya maji 
safi na salama kwa wakazi 77,015  wakiwemo 45,470 wa Wilaya ya Mkalama 
na 31,545 wa Iramba ifikapo mwaka 2015.
  Utekelezji wa Programu ya Maji na Usafi wa Mazingira awamu ya kwanza  
katika Halmashauri ya Wilaya ya Iramba ulianza mwaka 2008/2009 ambapo 
vijiji 13  vya Iramba na Mkalama viliingia, wakati huo ilikuwa 
ikitambulika kama Wilaya  moja ya Iramba.
Chanzo:Tanzani Daima 
0 comments:
Post a Comment