Home » » WAZEE WA KIMILA WAHUSISHWE VITA DHIDI YA UKEKETAJI.

WAZEE WA KIMILA WAHUSISHWE VITA DHIDI YA UKEKETAJI.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

ZAIDI ya wanawake 9,000 mkoani Singida wamegundulika kuwa wamekeketwa katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

Daktari Bingwa wa Ushauri wa magonjwa ya Wanawake na Uzazi mkoani hapa, Suleiman Mutani aliyasema hayo kwenye Jukwaa la Kitaifa la kuadhimisha Siku ya kupinga ukeketaji lililofanyika mjini hapa.

Dk Mutani alisema, idadi hiyo ya waliokeketwa ni sawa na asilimia 20.8 ya wanawake wote waliokwenda kujifungua kwenye vituo mbalimbali vya kutolea tiba mkoani humu, kati ya Januari 2013 na Desemba mwaka jana.
“Wanawake 9,386 walibainika kufanyiwa ukeketaji, jambo ambalo ni kinyume cha sheria na ni ukiukwaji wa misingi ya haki za binadamu, licha ya kuwa na madhara makubwa ya kiafya” alisema Dk Mutani.

Alitaja madhara yatokanayo na ukeketaji kuwa ni pamoja na kuwa na uzazi pingamizi wakati wa kujifungua, wanawake kupata shida wakati wa hedhi, uwezekano wa kupata fistula, kuugua maradhi ya kujamiiana na kuhisi maumivu makali wakati wa tendo la ndoa.

Dk Mutani alisema pia kuwa madhara hayo ni matokeo hasi yasababishwayo na jamii husika kuendelea kukumbatia mila hiyo potofu .
Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (Tamwa), Edda Sanga alisema, madhumuni ya jukwaa hilo ni kutoa fursa kwa wadau kujadili kwa kina utekelezaji wa maazimio ya miaka iliyopita na kupanga mikakati na njia bora zaidi za kukabiliana na mbinu mpya za ukeketaji.

Alitaja mikoa ambayo ni vinara wa ukeketaji na asilimia kwenye mabano kuwa ni Manyara (71), Dodoma (64), Arusha (59), Singida (51) na Mara (40).
Mikoa mingine ambayo pia inahusishwa na ukeketaji kutokana na watu wa makabila yanayoendesha vitendo hivyo kuhamia, ni Dar es Salaam, Pwani na Morogoro.

Hata hivyo, wadau waliohudhuria kikao hicho walisema kuwa, pamoja na mikakati mbalimbali, mbinu bora zaidi ni kuwawezesha ngariba kuwa na miradi ya kipato mbadala ili waache biashara ya kukeketa.

Aidha, walishauri wazee wa kimila katika maeneo husika wahusishwe kikamilifu katika vita dhidi ya ukeketaji kwa sababu wanaheshimika zaidi na wana ushawishi mkubwa kwa jamii.

Jukwaa hilo la siku mbili lililoandaliwa na Tamwa, limefadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya Watu (UNFPA). Lilihudhuriwa na wadau kutoka mikoa minane ambayo baadhi ya makabila yake yanaendesha ukeketaji.
CHANZO: HABARI LEO.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa