Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
  MFUGAJI na mkulima  wa Kijiji cha Ufana, Kata ya Mgungira, Tarafa ya 
Sepuka, wilayani hapa mkoani  Singida, Sawaka Kujelwa, ametishia 
kuwafungulia mashtaka mahakamani viongozi  wawili wa Chama Cha Mapinduzi
 (CCM), kata hiyo kwa madai ya kuuza zaidi ya  ekari 500 anazozitegemea 
kwa ajili ya makazi, kilimo na malisho.
  Kujelwa, aliwataja  viongozi hao kuwa ni Mwenyekiti wa CCM wa Kata, 
Nhende Shija na Diwani Mussa  Ng’imba, ambao alidai waliamua kuvamia 
maeneo yake baada ya yeye kuugua ugonjwa  wa kushindwa kwenda haja 
ndogo, Desemba 21, 2009.
  Alisema baada ya  kuugua ndipo alilazimika kwenda kwenye matibabu 
ambako alipita hospitali ya  misheni ya Mtakatifu Gasper mjini Itigi, 
Makiungu, Puma na hatimaye hospitali  ya Rufaa ya KCMC Moshi, mkoani 
Kilimanjaro mwaka 2010 alikopona.
  “Baada ya kupata  matibabu KCMC, madaktari walinishauri kukaa karibu 
na hospitali hiyo kwa  uchunguzi zaidi, ambapo nilikaa hadi mwaka 2012 
ndipo niliporudi nyumbani,  lakini nikilazimika kufuata masharti ya 
madaktari ya kutofanya kazi ngumu,”  alisema.
  Aliongeza kuwa wakati akiwa kwenye matibabu  Moshi KCMC, ndipo diwani 
kwa kushirikiana na mwenyekiti wa chama wa kata,  walipoanza kuyavamia 
maeneo yake aliyokuwa akiyategemea kwa kilimo na malisho  ya mifugo, na 
mwaka jana wakati anaendelea na mapumziko ya matibabu, watu  walizidi 
kuvamia.
  Alisema kuwa baada  ya kuona hali hiyo, aliandika barua kwa Kaimu 
Ofisa Mtendaji wa Kijiji hicho,  kumjulisha, lakini bila mafanikio na 
ndipo mwaka jana alimwandikia mwenyekiti  wa kijiji kumfahamisha juu ya 
uvamizi huo.
  Mwenyekiti wa  Kitongoji cha Matinje, Elius Milekwa na Mwenyekiti wa 
Kijiji cha Ufana, Machiya  Nyorobi, walipotakiwa kuzungumzia malalamiko 
hayo, walikiri eneo lililovamiwa  ni la Kujelwa na kwamba wanaoendesha 
shughuli za kilimo na malisho kwa sasa ni  wavamizi na hawataki 
kuyaachia.
  Mwenyekiti wa CCM  Kata ya Mgungira, Nhende Shija alipoulizwa sababu 
za kuvamia maeneo hayo,  alidai hakuvamia bali ni mali  yake.
  Diwani Ng’imba  alisema kuwa, malalamiko hayo hayana ukweli wowote ila
 ni mali yake na mwenyekiti huyo, na  kwamba Sawaka ni tapeli tu.
 Chanzo;Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment