Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
WATU sita wakazi wa wilayani ya Manyoni mkoani Singida,  
wanashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kukutwa na nyara za 
serikali  zenye thamani ya zaidi ya sh. milioni 200.
  Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Mkuu wa Wilaya  
hiyo, Fatma Toufiq, bila kuwataja watuhumiwa hao, alisema kuwa tukio 
hilo  lilitokea Julai 8, mwaka huu, kwenye nyumba ya kulala wageni 
iitwayo Matunda.
   Alizitaja nyara hizo kuwa ni vipande 28 vya meno ya tembo  ambavyo ni
 sawa na tembo wanane, singa za tembo bando sita, ngozi ya simba  moja, 
mkia wa pofu, kucha nne za simba, silaha aina ya SMG mbili, risasi 48 na
  magazine tatu.
  Toufiq alisema nyara hizo zote zina thamani ya sh. 202,560,000 na  
kwamba Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi ambapo ukikamilika 
watuhumiwa  hao watapelekwa mahakamani.
  Katika hatua nyingine, Toufiq alisema baada ya Operesheni Tokomeza  
matukio ya ujangili wa tembo yaliendelea kwenye maeneo mbalimbali ya 
Ikolojia.
  Alisema kuwa katika matukio matatu, askari wa Kikosi cha Kuzuia  
Ujangili Kanda ya Kati (KDU) na polisi Manyoni waliwakamata watuhumiwa 
wanne  wakiwa na meno ya tembo sita na vipande 37 ambavyo ni sawa na 
tembo 15.
  Kwa mujibu wa Toufiq watuhumiwa hao ni George James maarufu kama  
Maige aliyekamatwa Februari 12, mwaka huu, katika Kijiji cha Mgandu, 
akiwa na  vipande 21 vyenye uzito wa kilo 39.5 ambavyo thamani yake ni 
sh. 34,760,000.
  Mtuhumiwa mwingine ni Ally Hamadi aliyekamatwa Februari 16, mwaka  
huu, katika Kijiji cha Mgandu, akiwa na vipande 16 vyenye uzito wa kilo 
19.4  vyenye thamani ya sh. 17,072,000.
  Wengine kwa mujibu wa mkuu wa wilaya, ni David Makasi  na Joseph 
Malima waliokamatwa Machi 29, mwaka huu, wakiwa na nyara  mbalimbali 
zenye kilo 31.1 ambazo thamani yake ni sh. 27,368,000 na kwamba  nyara 
zote hizo zina thamani ya sh. 79,200,000.
  Alifafanua kuwa tembo wote waliuawa kwenye mapori ya akiba ya  
Rungwa/Kizigo/Mhesi na kwamba Ikolojia ya Rungwa–Ruaha bado ina tembo 
wengi  ambao huzunguka kwenye mapori ya akiba ya Rungwa/Kizigo/Muhesi, 
Swagaswaga na  Mkungunero.
  Toufiq aliongeza kuwa mapori mengine ni hifadhi za taifa za Ruaha,  
Tarangire, Mikumi na Manyara na hujumuisha pia na mapori ya wazi ya 
Mgori,  Itiso, Pawaga, Pwaga Rumuma, Mtera, Chaya, Mwamagembe, Shelui na
  Sambaru/Londoni.
  Kwa kutambua changamoto hiyo, mkuu huyo wa wilaya alibainisha kuwa  
ofisi ya Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori ilifanya mawasiliano na 
wakuu wa  taasisi za Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) na Mamlaka 
ya Hifadhi za  Taifa (Tanapa).
   Alisema mawasiliano hayo yalifanyika ili kuwezesha wakuu wa  kanda 
dhidi ya ujangili (KDU-Arusha na Manyoni) katika kupambana na ujangili  
kushirikiana na kikosi kazi cha Ikolojia ya Ngorongoro, Manyara-Tarangie
  ambacho kimekuwa kinafuatilia mitandao ya ujangili sehemu mbalimbali 
na tayari  wanayo kanzi data (Data Base).
Chanzo:Tanzania Daima 
0 comments:
Post a Comment