Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
 
             
                
KAMATI 
ya Usalama na Maadili ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Agosti mwaka huu, 
itafanya mapitio ya mwenendo wa wanachama wake waliopewa onyo kwa kosa 
la kuanza kampeni za kutafuta kuteuliwa kugombea urais katika Uchaguzi 
Mkuu 2015, kabla ya wakati kinyume na Kanuni za Uongozi na Maadili ya 
CCM, toleo la Februari 2010, Ibara 6(7)(i).
 
Katibu wa NEC, Itikadi 
na Uenezi wa CCM, Bw. Nape Nnauye, aliyasema hayo Dar es Salaam jana 
wakati akizungumza na waandishi wa habari juu ya kile kilichozungumzwa 
kwenye kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM iliyofanya kikao 
cha siku moja jijini Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake, Rais Jakaya
 Kikwete.
 
Alisema pamoja na mambo
 mengine, kikao hicho kilipokea taarifa ya mazungumzo yanayoendelea kati
 ya CCM kwa upande mmoja na vyama vingine vya siasa ambavyo ni CHADEMA, 
NCCR-Mageuzi na CUF ambayo yanasimamiwa na Msajili wa Vyama vya Siasa 
nchini Jaji Francis Mutungi.
Bw. Nnauye alisema, 
lengo la mazungumzo yaliyokutanisha vyama hivyo ni kuangalia kwa kina 
sababu za baadhi ya wajumbe wachache wa Bunge Maalumu la Katiba, kususia
 na kutoka nje katika awamu ya kwanza ya vikao vya Bunge hilo.
Lengo lingine ni 
kuangalia namna ambavyo wajumbe hao watarudi bungeni ili kukamilisha 
mchakato wa mabadiliko ya Katiba ambapo Kamati Kuu ya CCM, imeridhishwa 
na mwenendo wa mazungumzo hayo, kupongeza juhudi zinazofanywa na Jaji 
Mutungi pamoja na vyama husika vinavyoshiriki mazungumzo.
 
"Kamati Kuu pia 
ilipokea taarifa za harakati za baadhi ya wanachama wa CCM walioonesha 
nia ya kuomba ridhaa ya chama kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu 
2015...baada ya kutafakari kwa kina, Kamati hii inapenda kuwakumbusha 
wote kuwa ili wasipoteze sifa za kugombea ni muhimu wakazingatia katiba,
 kanuni na taratibu za chama.
"Wanachama waliopewa 
adhabu na Kamati Kuu kutokana na kukiuka taratibu za chama katika suala 
hili, Kamati ya Usalama na Maadili ya chama itafanya mapitio ya mwenendo
 wao na utekelezaji wa adhabu hiyo Agosti mwaka huu.
"Ikibainika 
hawatekelezi ipasavyo masharti ya adhabu zao, itapendekeza kwa Kamati 
Kuu iongeze adhabu kwa kuzingatia taratibu za chama," alisema Bw. 
Nnauye.
Aliongeza kuwa ni 
muhimu wanachama wote wakatambua kuwa, chama ni pamoja na Katiba, kanuni
 na taratibu zake hivyo kutoziheshimu na kuzifuata ni kuvuruga jambo 
ambalo haliwezi kuvumilika.
Alisema dhamira ya CCM 
kusimamia Katiba, kanuni na taratibu za chama ni kuhakikisha chama hicho
 kinakuwa na umoja, mshikamano ambao ni wa muhimu sana hasa wanapokwenda
 kukamilisha kazi ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2010/15.
Februari mwaka huu, CCM
 ilifanya vikao vya kitaifa ambavyo vilishughulikia suala la maadili 
ndani ya chama vikihusisha Kamati Ndogo ya Udhibiti, Tume ya Udhibiti na
 Nidhamu na Kamati Kuu.
Vikao hivyo viliwahoji 
baadhi ya wanachama wa chama hicho ambao ni Bw. Frederick Sumaye, Bw. 
Edward Lowasa, Bw. Bernard Membe, Bw. Stephen Wassira, Bw. January 
Makamba na Bw. William Ngeleja.
Baada ya wanachama 
waliohojiwa, ilithibitika kuwa baadhi ya tuhuma dhidi yao ni za kweli 
hivyo kamati zilipendekeza adhabu na mapendekezo hayo yalipelekwa kwenye
 Tume ya Udhibiti na Nidhamu na hatimaye Kamati Kuu ya CCM ambayo ilitoa
 adhabu kwa wahusika.
Ilithibitika wanachama 
hao walifanya makosa mawili, mosi la kuanza kampeni za kutafuta 
kuteuliwa kugombea Urais kabla ya wakati kinyume na Kanuni za Uongozi na
 Maadili za CCM, Toleo la Februari 2010, Ibara 6(7)(i).
Kosa la pili ni kufanya
 vitendo vinavyokiuka maadili ndani ya chama na baadhi yao kufanya 
vitendo vinavyokiuka maadili ndani ya jamii kinyume na Kanuni za Uongozi
 na Maadili za CCM, Toleo la Februari 2010, Ibara kadhaa za kanuni hizo.
Kwa mujibu wa Bw. 
Nnauye ambaye alitoa tamko la CCM Februari 18 mwaka huu juu ya adhabu 
zilizochukuliwa kwa wanachama hao, alisema Kamati Kuu baada ya 
kuthibitisha makosa hayo imewapa watu hao adhabu ya onyo kali na 
kuwataka wajiepushe na vitendo vinavyokiuka maadili na iwapo wataendelea
 na vitendo hivyo, chama kitawachukulia hatua kali zaidi.
Alisema tafsiri ya 
adhabu ya onyo kali kwa mujibu wa Kanuni za Uongozi na Maadili za CCM, 
Toleo la Februari 2010, Ibara ya 8(ii) (b) ni mwanachama aliyepewa 
adhabu ya onyo kali, atakuwa katika hali ya kuchunguzwa kwa muda 
usiopungua miezi 12, ili kumsaidia katika jitihada zake za 
kujirekebisha.
Aliongeza kuwa, Kamati 
Kuu iliitaka Kamati Ndogo ya Udhibiti kuwachunguza na kuchukua hatua kwa
 wote waliohusika kwa namna moja au nyingine (mawakala na wapambe) 
kufanyika kwa vitendo hivyo ambavyo vilivunja kanuni za chama.
Pia Kamati Kuu 
iliwaonya vikali viongozi na watendaji wa chama ikiwataka wajiepushe 
kujihusisha na matendo ya wanaowania urais yanayovunja na kukiuka 
maadili ya chama badala yake wazingatie kanuni na taratibu za chama.
Chanzo:Majira 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment