Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Nani atabisha kwamba hakuna jambo linalogusa Wabongo kama elimu?
 Au labda tuseme hakuna jambo linalogusa Wabongo kama matokeo ya 
mitihani. Ndiyo maana sikushangaa kupokea mapepe kibao wiki hii. Hebu 
niwaonyeshe mbili tu.
Yes, Serikali yetu bunifu. Kwa nini tuhangaike 
kuinua uwezo wakati tunaweza kushusha viwango? Achana na hawa 
wanaharakati wote, ambao kazi yao ni kupinga tu utadhani wanaamka na 
kula malimau tu kila asubuhi. Mimi nasema, hongera sana wote waliofaulu 
mwaka huu. Hongera kwa kuzaliwa mwaka mwafaka, mwaka wa neema, mwaka wa 
mafanikio. Hongera zaidi kwa wizara yetu ya shule pamoja na Baraza la 
Vyakihuni kwa kuonyesha njia. Kwa njia hii tunajua Bongo yetu itasonga 
mbele kwa kasi sana.
Kwanza kwenye mpira. Miaka mingapi tumelalamika 
kuhusu kiwango cha mpira hapa petu? Uongozi mbovu huzaa mpira mbovu. Na 
kutokana na ubovu huo, tumepata matatizo sana ya uhaba wa magoli mara 
kwa mara. Tunajitahidi kuwafundisha washambuliaji wetu jinsi ya kufunga,
 lakini ukweli ni kwamba magoli ni madogo mno. Hivyo, kuanzia msimu ujao
 wa ligi kuu na ligi zote chini yake, magoli yatapanuliwa kwa mita tano 
zaidi. Nadhani kwa njia hiyo tutaweza kushangilia magoli mengi, potelea 
mbali iwapo kwenye mashindano ya kimataifa goli itakuwa dogo, lazima 
wajue kwamba mabadiliko ni sisi, sisi ni wabongo na tutabonga na 
kuboronga kwa njia zetu wenyewe.
Haya, upande wa fedha pia. Hawa watu wa Hazina 
watumie ubunifu badala ya ubanifu. Kama pesa hazitoshi, chapa pesa 
nyingi zaidi. Kwa njia hiyo, kila mtu atajisikia akibeba marundo ya 
manoti. Hata kama haina thamani ni lazima tushindane na wenzetu wa 
Zimbabwe, ambao hatimaye walitumia dola zao milioni moja kwa ajili ya 
kununua kilo moja ya sukari. Kila mtu milionea au hata bilionea, wataka 
nini zaidi?
Kwa kweli katika sayansi inaitwa sheria ya 
utapiamlo ni sheria ya Mungu kabisa. Mlo ukipungua kwa mtoto, tumbo 
linaongezeka, linatuna, linang’aa. Na elimu inaweza kuwa vivyo hivyo.
Tena ingawa tunafanya kwa mtindo wetu mwenyewe, 
tunaendeleza vizuri sana umoja wa Afrika. Wale wenye sifa ya uaminifu na
 kutokomeza utapeli walionyesha njia siku nyingi, yaani Nigeria lakini 
wapumbavu wa vyuo vikuu mwisho walikataa kuamini matokeo hayo, hivyo 
waliotaka kuingia vyuo vikuu vyao walilazimika kufanya mtihani wa ziada.
 Kufuru kabisa na ole wake profesa atakayejaribu huo upuuzi hapa. Kama 
mtu amepata cheti, wao ni nani kukihoji?
Baraza la Vihuni juuuuuu! Viwango ziiiiii, kidumu na kudumu.
Duh! Barua hii ilinishtua kidogo, lakini kabla sijaweza kuachana na mshangao wangu, ikaja nyingine.
We Makengeza,
Mimi sijui nifurahie ya mwaka huu au niomboleze ya
 mwaka jana. Yaani, baada ya kuletwa hapa kwenye shule ya walimu wawili 
na kitabu kimoja, nimejitahidi kwa nguvu zangu zote kuwapatia vijana 
wetu angalau misingi michache ya elimu, lakini haiwezekani. Wanapata 
kitu labda, lakini mbele ya mitihani lazima wafeli kwa sababu hatuna 
uwezo wa kuwapatia zaidi. Sasa mwaka huu, tupo walimu walewale na kitabu
 kilekile na hata notisi zilezile, maana utapata wapi zingine lakini 
ghafla shule nzima imefaulu. Haiyumkiniki. Sijaongeza juhudi wala 
maarifa, maana tangu niombe ualimu nimejitahidi vilevile. Na sioni 
kwamba wanafunzi wangu wamebadilika pia. Tena wa mwaka huu walikuwa na 
hasira zaidi wakijua watapigwa muhuri wa ujinga tu. Je, wanastahili 
kusonga mbele? Labda kwa kuwa na akili, ambayo ikikutana na mazingira ya
 kweli ya elimu, lakini kwa hayo waliyoyapata kutoka kwangu na 
mwenzangu, mmmmh! Tunaelekea wapi?
Basi kutokana na hayo, nikajikuta natafakari kwa 
kina wakati nimefunikwa na giza nene ya eneo letu. Wakati asilimia 
sitini ya shule za Kenya zina umeme, kwetu ni asilimia mbili tu ya shule
 za vijijini. Ndiyo maana elimu iko hoi kwa koroboi. Lakini angalau tuna
 nafasi ya kutafakari.
Sasa, uzee wako lazima unakumbuka enzi zile za 
kupiga deki resepsheni. Sijui inaitwaje siku hizi, lakini nimegundua 
kwamba tabia za mtu mmoja mmoja zinaakisi tabia za wakubwa wetu na 
mifumo yao ya kutufuma bila sisi kuwafumania. Angalia watoto wanavyohaha
 barabarani kutafuta wafadhili kwa ajili ya timu yao ya mpira au 
mahafali wa darasa la saba. Nani kawafundisha kwamba dunia ni kuombaomba
 siyo kufanya kazi? Elimu ya Kujitegemea siyo kujiegemea iliishia wapi? 
Hata ule mpango wa maskauti wa kufanya kazi ndogondogo ili walipwe kwa 
ajili ya mipango yao iliishia wapi? Nani kawatonya umatonya?
Haya, hata katika elimu mambo hayo ya kuwangia viwango yalianza 
leo? Tangu zamani sote tumethamini sura ya elimu, badala ya elimu 
yenyewe. Zamani ilitosha kunawa vizuri kwa uso wa kawaida, yaani kusoma 
kwa bidii chini ya uangalizi wa walimu wanaofundisha kwa bidii ndani ya 
mazingira wezeshi. Nakumbuka, maana hata mimi nilisoma wakati ule. 
Lakini hata wakati ule, bado wanafunzi wengi walijali sura ya elimu tu, 
siyo elimu yenyewe maana lengo lilikuwa cheti siyo zaidi ya hapo.
Haya, sura ya elimu ikaanza kuota vipele kutokana 
na sababu mbalimbali. Maarifa ikapungua na wengi walikosa vyeti ndipo 
ilibidi kutafuta sabuni za kuua vijidudu vilivyoanza kujitokeza. Badala 
ya kuoga vizuri, watu walitegemea sabuni itafanya kazi peke yake. Sabuni
 hii kwa lugha ya kitaalamu iliitwa sabuni twisheni. Na wengine walibuni
 sabuni kali zaidi iliyoitwa sabuni akademiki. Ndiyo maana tulisikia 
kwamba watu wengine walipata fasticlasi ya vidato, kisha wakala disko 
baada ya mwaka mmoja chuoni kutokana na kukosa sabuni hiyo (ingawa 
nasikia hata kule siku hizi sabuni hizi zimetapakaa).
Kutokana na sabuni hizo pia, Serikali yetu kufuru 
iliweza kubuni mpango wa viwango panuka, badala ya viwango pandisha. 
Kila mtu alitakiwa kuoga hata maji yakiwa machafu namna gani au hata 
kukosekana kabisa, ili mradi wanakubali kununua sabuni twisheni na wao. 
Wasipokuwa na uwezo wa kupata hiyo sabuni potelea mbali. Wenye sabuni 
ndiyo wenye zabuni za kujaza nafasi za juu.
Lakini mambo siyo rahisi kivile. Wasio na sabuni 
walianza kuwashwa sana, ngozi zao zikaharibika hadi wakaanza kudai elimu
 ya kweli na wao. Ndipo hapo tumekuja na mikorogo kabisa. Mtu anaweza 
kuwa hana maji, hana sabuni, hana chakula bora, lakini ili mradi 
resepsheni inapigwa deki. Nani atajua na ataweza kwenda kujinadi popote?
 Cheti ni mkorogo, ndiyo maana unaona watu wana sura ya Mirinda, lakini 
akili ya Pepsi.
Ndiyo maana nawahurumia wanafunzi wangu wa huko 
nyuma. Kama suala ni mkorogo tu, kwa nini pepa zao zisisahihishe upya 
ili na wao waingie katika ufalme wa mbingu.
Lakini mwisho, nawapa pole wanafunzi wa mwaka huu 
pia. Muwe mmebebwa na daladala ya ‘T111BRN’ au la, mustakabali wa nchi 
yetu uko mikononi mwenu.
Ndiyo. Siyo tu kwa sababu ambazo tumezizoea kwamba
 sura ya elimu itajenga sura ya ghorofa au daraja au kutibu sura ya 
magonjwa. Bali vizazi vitakavyofuata vitaweza kupata au kukosa nafasi 
kutokana na maisha yenu. Kwa matokeo kama haya, wengi mtaweza hata 
kuomba masomo ya nje. Iwapo nyinyi na Fasticlasi yenu (siyo First Class)
 mtaonekana katika vipimo vingine kwamba hamjui, mitihani ya Bongo 
itadharauliwa moja kwa moja. Na hata humu, nani atawaajiri mkorogo 
ukitambulika?
Mwalimu mkereketwa.
Na mimi pia nikabaki natafakari ndani ya giza 
nene. Twafunga goli au twajifunga? Kupanua goli ndiyo suluhisho. 
Tukichapa pesa nyingi, mwisho si itaonekana feki? Sura ya Mirinda 
itaficha daima akili ya Pepsi?
Chanzo:Mwananchi
Chanzo:Mwananchi
0 comments:
Post a Comment