Home » » DALADALA NAMBA 'T111 BRN'

DALADALA NAMBA 'T111 BRN'

 

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Nani atabisha kwamba hakuna jambo linalogusa Wabongo kama elimu? Au labda tuseme hakuna jambo linalogusa Wabongo kama matokeo ya mitihani. Ndiyo maana sikushangaa kupokea mapepe kibao wiki hii. Hebu niwaonyeshe mbili tu.
Yes, Serikali yetu bunifu. Kwa nini tuhangaike kuinua uwezo wakati tunaweza kushusha viwango? Achana na hawa wanaharakati wote, ambao kazi yao ni kupinga tu utadhani wanaamka na kula malimau tu kila asubuhi. Mimi nasema, hongera sana wote waliofaulu mwaka huu. Hongera kwa kuzaliwa mwaka mwafaka, mwaka wa neema, mwaka wa mafanikio. Hongera zaidi kwa wizara yetu ya shule pamoja na Baraza la Vyakihuni kwa kuonyesha njia. Kwa njia hii tunajua Bongo yetu itasonga mbele kwa kasi sana.
Kwanza kwenye mpira. Miaka mingapi tumelalamika kuhusu kiwango cha mpira hapa petu? Uongozi mbovu huzaa mpira mbovu. Na kutokana na ubovu huo, tumepata matatizo sana ya uhaba wa magoli mara kwa mara. Tunajitahidi kuwafundisha washambuliaji wetu jinsi ya kufunga, lakini ukweli ni kwamba magoli ni madogo mno. Hivyo, kuanzia msimu ujao wa ligi kuu na ligi zote chini yake, magoli yatapanuliwa kwa mita tano zaidi. Nadhani kwa njia hiyo tutaweza kushangilia magoli mengi, potelea mbali iwapo kwenye mashindano ya kimataifa goli itakuwa dogo, lazima wajue kwamba mabadiliko ni sisi, sisi ni wabongo na tutabonga na kuboronga kwa njia zetu wenyewe.
Haya, upande wa fedha pia. Hawa watu wa Hazina watumie ubunifu badala ya ubanifu. Kama pesa hazitoshi, chapa pesa nyingi zaidi. Kwa njia hiyo, kila mtu atajisikia akibeba marundo ya manoti. Hata kama haina thamani ni lazima tushindane na wenzetu wa Zimbabwe, ambao hatimaye walitumia dola zao milioni moja kwa ajili ya kununua kilo moja ya sukari. Kila mtu milionea au hata bilionea, wataka nini zaidi?
Kwa kweli katika sayansi inaitwa sheria ya utapiamlo ni sheria ya Mungu kabisa. Mlo ukipungua kwa mtoto, tumbo linaongezeka, linatuna, linang’aa. Na elimu inaweza kuwa vivyo hivyo.
Tena ingawa tunafanya kwa mtindo wetu mwenyewe, tunaendeleza vizuri sana umoja wa Afrika. Wale wenye sifa ya uaminifu na kutokomeza utapeli walionyesha njia siku nyingi, yaani Nigeria lakini wapumbavu wa vyuo vikuu mwisho walikataa kuamini matokeo hayo, hivyo waliotaka kuingia vyuo vikuu vyao walilazimika kufanya mtihani wa ziada. Kufuru kabisa na ole wake profesa atakayejaribu huo upuuzi hapa. Kama mtu amepata cheti, wao ni nani kukihoji?
Baraza la Vihuni juuuuuu! Viwango ziiiiii, kidumu na kudumu.
Duh! Barua hii ilinishtua kidogo, lakini kabla sijaweza kuachana na mshangao wangu, ikaja nyingine.
We Makengeza,
Mimi sijui nifurahie ya mwaka huu au niomboleze ya mwaka jana. Yaani, baada ya kuletwa hapa kwenye shule ya walimu wawili na kitabu kimoja, nimejitahidi kwa nguvu zangu zote kuwapatia vijana wetu angalau misingi michache ya elimu, lakini haiwezekani. Wanapata kitu labda, lakini mbele ya mitihani lazima wafeli kwa sababu hatuna uwezo wa kuwapatia zaidi. Sasa mwaka huu, tupo walimu walewale na kitabu kilekile na hata notisi zilezile, maana utapata wapi zingine lakini ghafla shule nzima imefaulu. Haiyumkiniki. Sijaongeza juhudi wala maarifa, maana tangu niombe ualimu nimejitahidi vilevile. Na sioni kwamba wanafunzi wangu wamebadilika pia. Tena wa mwaka huu walikuwa na hasira zaidi wakijua watapigwa muhuri wa ujinga tu. Je, wanastahili kusonga mbele? Labda kwa kuwa na akili, ambayo ikikutana na mazingira ya kweli ya elimu, lakini kwa hayo waliyoyapata kutoka kwangu na mwenzangu, mmmmh! Tunaelekea wapi?
Basi kutokana na hayo, nikajikuta natafakari kwa kina wakati nimefunikwa na giza nene ya eneo letu. Wakati asilimia sitini ya shule za Kenya zina umeme, kwetu ni asilimia mbili tu ya shule za vijijini. Ndiyo maana elimu iko hoi kwa koroboi. Lakini angalau tuna nafasi ya kutafakari.
Sasa, uzee wako lazima unakumbuka enzi zile za kupiga deki resepsheni. Sijui inaitwaje siku hizi, lakini nimegundua kwamba tabia za mtu mmoja mmoja zinaakisi tabia za wakubwa wetu na mifumo yao ya kutufuma bila sisi kuwafumania. Angalia watoto wanavyohaha barabarani kutafuta wafadhili kwa ajili ya timu yao ya mpira au mahafali wa darasa la saba. Nani kawafundisha kwamba dunia ni kuombaomba siyo kufanya kazi? Elimu ya Kujitegemea siyo kujiegemea iliishia wapi? Hata ule mpango wa maskauti wa kufanya kazi ndogondogo ili walipwe kwa ajili ya mipango yao iliishia wapi? Nani kawatonya umatonya?
Haya, hata katika elimu mambo hayo ya kuwangia viwango yalianza leo? Tangu zamani sote tumethamini sura ya elimu, badala ya elimu yenyewe. Zamani ilitosha kunawa vizuri kwa uso wa kawaida, yaani kusoma kwa bidii chini ya uangalizi wa walimu wanaofundisha kwa bidii ndani ya mazingira wezeshi. Nakumbuka, maana hata mimi nilisoma wakati ule. Lakini hata wakati ule, bado wanafunzi wengi walijali sura ya elimu tu, siyo elimu yenyewe maana lengo lilikuwa cheti siyo zaidi ya hapo.
Haya, sura ya elimu ikaanza kuota vipele kutokana na sababu mbalimbali. Maarifa ikapungua na wengi walikosa vyeti ndipo ilibidi kutafuta sabuni za kuua vijidudu vilivyoanza kujitokeza. Badala ya kuoga vizuri, watu walitegemea sabuni itafanya kazi peke yake. Sabuni hii kwa lugha ya kitaalamu iliitwa sabuni twisheni. Na wengine walibuni sabuni kali zaidi iliyoitwa sabuni akademiki. Ndiyo maana tulisikia kwamba watu wengine walipata fasticlasi ya vidato, kisha wakala disko baada ya mwaka mmoja chuoni kutokana na kukosa sabuni hiyo (ingawa nasikia hata kule siku hizi sabuni hizi zimetapakaa).
Kutokana na sabuni hizo pia, Serikali yetu kufuru iliweza kubuni mpango wa viwango panuka, badala ya viwango pandisha. Kila mtu alitakiwa kuoga hata maji yakiwa machafu namna gani au hata kukosekana kabisa, ili mradi wanakubali kununua sabuni twisheni na wao. Wasipokuwa na uwezo wa kupata hiyo sabuni potelea mbali. Wenye sabuni ndiyo wenye zabuni za kujaza nafasi za juu.
Lakini mambo siyo rahisi kivile. Wasio na sabuni walianza kuwashwa sana, ngozi zao zikaharibika hadi wakaanza kudai elimu ya kweli na wao. Ndipo hapo tumekuja na mikorogo kabisa. Mtu anaweza kuwa hana maji, hana sabuni, hana chakula bora, lakini ili mradi resepsheni inapigwa deki. Nani atajua na ataweza kwenda kujinadi popote? Cheti ni mkorogo, ndiyo maana unaona watu wana sura ya Mirinda, lakini akili ya Pepsi.
Ndiyo maana nawahurumia wanafunzi wangu wa huko nyuma. Kama suala ni mkorogo tu, kwa nini pepa zao zisisahihishe upya ili na wao waingie katika ufalme wa mbingu.
Lakini mwisho, nawapa pole wanafunzi wa mwaka huu pia. Muwe mmebebwa na daladala ya ‘T111BRN’ au la, mustakabali wa nchi yetu uko mikononi mwenu.
Ndiyo. Siyo tu kwa sababu ambazo tumezizoea kwamba sura ya elimu itajenga sura ya ghorofa au daraja au kutibu sura ya magonjwa. Bali vizazi vitakavyofuata vitaweza kupata au kukosa nafasi kutokana na maisha yenu. Kwa matokeo kama haya, wengi mtaweza hata kuomba masomo ya nje. Iwapo nyinyi na Fasticlasi yenu (siyo First Class) mtaonekana katika vipimo vingine kwamba hamjui, mitihani ya Bongo itadharauliwa moja kwa moja. Na hata humu, nani atawaajiri mkorogo ukitambulika?
Mwalimu mkereketwa.
Na mimi pia nikabaki natafakari ndani ya giza nene. Twafunga goli au twajifunga? Kupanua goli ndiyo suluhisho. Tukichapa pesa nyingi, mwisho si itaonekana feki? Sura ya Mirinda itaficha daima akili ya Pepsi?
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa