Home » » Kung’olewa kwa Zitto, Mkumbo: Chadema mikoani watofautiana

Kung’olewa kwa Zitto, Mkumbo: Chadema mikoani watofautiana

Wanachama wa Chadema mikoa mbalimbali nchini pamoja na wananchi wametoa maoni tofauti kuhusu uamuzi wa Kamati Kuu ya chama hicho wa juzi kuwavua uongozi viongozi wake watatu; Naibu Katibu Mkuu wake Zitto Kabwe na Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk Kitila Mkumbo na mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba.
Singida
Kutoka mkoani Singida, uongozi wa chama hicho  jana ulifanya kikao cha faragha kujadili uamuzi wa chama hicho, huku baadhi ya wananchi wakiuelezea uamuzi  huo kuwa umetokana na pupa na kushindwa kuvumiliana, wengine wakitishia kujitoa katika chama hicho.
Kwa zaidi za saa 5 uongozi huo ulikuwa ukijadili hatua hiyo huku ukiahidi kutoa taarifa yake baada ya kikao hicho kilichokuwa kikiendelea hadi baada ya saa 7 mchana.
Habari zaidi kutoka Wilaya ya Iramba mkoani humo zinasema kuwa wanachama wa Chadema wilayani humo wametishia kurudisha kadi za chama hicho kilichokuwa kimeanza kujizolea umaarufu wakisema watafanya hivyo ikiwa Chadema ‘watalitosa jembe’ lao.
Baadhi ya wananchi waliozungumza na gazeti hili walisema kuwa hatua hiyo inaweza kuipunguzia umaarufu Chadema na kwamba ustawi wa vyama vingi vya siasa unaponzwa na pupa, jazba hata kukosa uvumilivu.
“Kikundi hiki cha viongozi kinasababisha Chadema kumeguka kama tulivyosikia juzi. Kwa maoni yangu kabla hakijawavua uongozi Zitto, Dk Mkumbo na Mwigamba, kilikuwa kinashabikiwa na asilimia 90, hapa Singida, lakini baada ya tukio la juzi la kuwavua uongozi baadhi ya viongozi, nina hakika kinashabikiwa na asilimia 30 ya wananchi,” alisema Juma Mdida.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TLP Wilaya ya Singida, Athumani Nkii, alisema kuwa ustawi  wa vyama vingi vya siasa unaponzwa na vitendo vya pupa, jazba na ubinafsi wa baadhi ya viongozi wake baada ya majina yao kupata umaarufu,wakisahau kuwa umaarufu huo unachangiwa na chama husika.
“Kwa upande wa Kabwe Zitto, nadhani safari zake za nje ya nchi na suala la mapesa ya Uswisi, zitakuwa hazina baraka za Chadema. Kuhusu Dk Kitila Mkumbo, sina kabisa fununu ya madhambi yake,”alisema.
Rukwa
Barua ya kujiuzulu nafasi ya Makamu Mwenyekiti Chadema Tanzania Bara, Said Amour Arfi ambaye pia ni Mbunge wa Mpanda imesambazwa  kwa wapiga kura wake na wananchi wa jimbo hilo ili  wafahamu sababu za msingi za yeye kujiondoa katika nafasi yake.
Katibu wa mbunge huyo, Joseph Mona, alipata taarifa za uamuzi huo wa ghafla, aliosema kuwa ni sahihi.
Chanzo;Mwananchi


0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa