Wanachama wa Chadema mikoa mbalimbali nchini pamoja na wananchi 
wametoa maoni tofauti kuhusu uamuzi wa Kamati Kuu ya chama hicho wa juzi
 kuwavua uongozi viongozi wake watatu; Naibu Katibu Mkuu wake Zitto 
Kabwe na Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk Kitila Mkumbo na mwenyekiti wa chama 
hicho Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba.
Singida
Kutoka mkoani Singida, uongozi wa chama hicho  
jana ulifanya kikao cha faragha kujadili uamuzi wa chama hicho, huku 
baadhi ya wananchi wakiuelezea uamuzi  huo kuwa umetokana na pupa na 
kushindwa kuvumiliana, wengine wakitishia kujitoa katika chama hicho.
Kwa zaidi za saa 5 uongozi huo ulikuwa ukijadili 
hatua hiyo huku ukiahidi kutoa taarifa yake baada ya kikao hicho 
kilichokuwa kikiendelea hadi baada ya saa 7 mchana.
Habari zaidi kutoka Wilaya ya Iramba mkoani humo 
zinasema kuwa wanachama wa Chadema wilayani humo wametishia kurudisha 
kadi za chama hicho kilichokuwa kimeanza kujizolea umaarufu wakisema 
watafanya hivyo ikiwa Chadema ‘watalitosa jembe’ lao.
Baadhi ya wananchi waliozungumza na gazeti hili 
walisema kuwa hatua hiyo inaweza kuipunguzia umaarufu Chadema na kwamba 
ustawi wa vyama vingi vya siasa unaponzwa na pupa, jazba hata kukosa 
uvumilivu.
“Kikundi hiki cha viongozi kinasababisha Chadema 
kumeguka kama tulivyosikia juzi. Kwa maoni yangu kabla hakijawavua 
uongozi Zitto, Dk Mkumbo na Mwigamba, kilikuwa kinashabikiwa na asilimia
 90, hapa Singida, lakini baada ya tukio la juzi la kuwavua uongozi 
baadhi ya viongozi, nina hakika kinashabikiwa na asilimia 30 ya 
wananchi,” alisema Juma Mdida.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TLP Wilaya ya 
Singida, Athumani Nkii, alisema kuwa ustawi  wa vyama vingi vya siasa 
unaponzwa na vitendo vya pupa, jazba na ubinafsi wa baadhi ya viongozi 
wake baada ya majina yao kupata umaarufu,wakisahau kuwa umaarufu huo 
unachangiwa na chama husika.
“Kwa upande wa Kabwe Zitto, nadhani safari zake za
 nje ya nchi na suala la mapesa ya Uswisi, zitakuwa hazina baraka za 
Chadema. Kuhusu Dk Kitila Mkumbo, sina kabisa fununu ya madhambi 
yake,”alisema.
Rukwa 
Barua ya kujiuzulu nafasi ya Makamu Mwenyekiti 
Chadema Tanzania Bara, Said Amour Arfi ambaye pia ni Mbunge wa Mpanda 
imesambazwa  kwa wapiga kura wake na wananchi wa jimbo hilo ili  
wafahamu sababu za msingi za yeye kujiondoa katika nafasi yake.
                
              Katibu wa mbunge huyo, Joseph Mona, alipata taarifa za uamuzi huo wa ghafla, aliosema kuwa ni sahihi.
Chanzo;Mwananchi 
0 comments:
Post a Comment