SINGIDA
 ni moja kati ya mikoa ambayo ilikuwa inafanya vizuri katika mchezo wa 
riadha miaka ya 1980 na kutoa wanariadha mahiri ambao waliiwakilisha 
Tanzania katika mashindano mbalimbali ya kimataifa.
Mkoa huo ni wenye mandhari nzuri yenye mawe mawe pamoja na mto upande wa kushoto na kulia hususan pale unapofika mkoani hapo.
Hakika
 mkoa huu ni wenye vitu vingi, lakini kikubwa zaidi ni wakimbiaji wa 
riadha hususan maeneo ya Singida Vijijini ambako kama wakimbiaji hao 
wataweza kupewa vifaa maalumu kwa ajili ya kukimbia na wadau wa riadha 
wakajitokeza na kuchangia zaidi katika riadha, Tanzania itakuwa na 
medali nyingi na kupata heshima katika nchi mbalimbali duniani.
Nasema
 hivyo kwa sababu hivi karibuni Mbunge wa Singida Vijijini ambaye pia ni
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu aliandaa 
mashindano ya riadha hususan vijijini kwa ajili ya kuibua vipaji kwa 
kushirikiana na Mkurugenzi wa Shrika la African Wildlife Trust (AWT), 
Pratic Patel.
Mbio
 hizo zilizojulikana kwa jina la Singida Marathon za kilometa 21, 
zilianza rasmi Novemba 9, mwaka huu kwa kushirikisha wakimbiaji zaidi ya
 400 kutoka Singida Mjini na Singida Vijijini na zilianzia Kijiji cha 
Mitula, Kata ya Kinyagigi na kuishia Viwanja vya Shule ya Msingu Ntunduu
 (W) Singida Vijijini.
Mbio
 hizo zilikuwa za kilometa 21 ambazo ni nusu marathoni na kilometa 5 na 
mwisho kabisa ni kilometa 2.5 ambazo ziliwashirikisha watoto wa kiume na
 wa kike. Wakimbiaji walikuwa wamejiandaa wenyewe na walijiandikisha, 
lakini baadhi yao pamoja na kukabiliwa na ukosefu wa viatu, lakini 
waliweza kumudu hali hiyo kutokana na mazingira waliyokua nayo na 
kuonesha vipaji vyao vilivyowashangaza wengi.
Inawezekana
 kukimbia bila viatu ni jambo lisiloruhusiwa, lakini kutokana na 
mazingira yenyewe ya vijijini hali hiyo haikuwa kikwazo kwa wakimbiaji 
hao kukimbia bila viatu ila walionesha kuwa wana moyo na nia ya dhati 
kuonesha vipaji vyao hakika ilikuwa faraja kubwa kwao kwani mwisho wa 
siku waliweza kuibuka washindi na wengine wakapata kifuta jasho.
Washindi
 hao ni Paulo Itambi ambaye aliibuka mshindi wa kwanza kwa upande wa 
wanaume ambaye alipewa zawadi ya Sh 300,000, Emmanuel Samson wa pili (Sh
 200,000) na Samwel Ikungi wa tatu (Sh 100,000). Kwa upande wa wanawake,
 mshindi wa kwanza Fabiola William (Sh 300,000), Zakia Abdallah (Sh 
200,000) na Winfrida Hassani (Sh 100,000).
Mbio
 za kilometa tano, washindi ni Gabriel Garado (Sh 200,000), Deo Lazaro 
(Sh 100,000) na Jonas John (Sh 50,000) huku wanawake ni Neema Kisuda (Sh
 200,000), Pascalina Silvesta (Sh 100,000) na Christina Yuda (Sh 50,000)
 ambao washindi wa kilometa 2.5 wakiwa ni Julita Antony (Sh 100,000), 
Editha Gabriel (Sh 50,000) na Magreth Bernado (Sh 25,000).
Wanaume
 walikuwa ni Petro Pascal mshindi wa kwanza na kupewa Sh 100,000, Baraka
 Sebastian (Sh 50,000), Haji Swalehe (Sh 25,000) huku washindi wengine 
400 kila mmoja akipewa Sh 10,000. Baada ya washindi hao kukabidhiwa 
zawadi zao, Patel ambaye alikuwa mgeni rasmi kwa niaba ya Naibu Waziri 
Nyalandu, alikabidhi pia medali mbalimbali kwa washindi hao.
Aidha,
 alitoa changamoto kwa wananchi hao kuacha tabia ya kuua tembo, bali 
wanastahili kulindwa na kuhifadhiwa ili kukuza uchumi na kufungua 
milango ya ajira.
Hata
 hivyo, baadhi ya washindi walimshukuru Nyalandu kwa kuamua kuanzisha 
mashindano hayo maeneo ya vijijini ili kuibua vipaji na kutoa rai kwa 
wadau wa riadha mkoani humo pamoja na sehemu mbalimbali kuanzisha klabu 
za michezo ya riadha ili kuendeleza vipaji na kuibuavipaji vipya.
Fabiola
 ambaye ni mkimbiaji mashuhuri wa riadha na aliyeiletea sifa Tanzania, 
alisema awali alikuwa akikimbia mkoani Kilimanjaro, lakini hivi sasa 
yupo Singida ambako alihamia Singida Vijijini kwenye Jimbo la Nyalandu, 
ndio kwao alipozaliwa na anaona fahari kubwa kuona wilaya hiyo ina 
wakimbiaji wengi na ni wazuri, lakini bado wanakabiliwa na changamoto ya
 ukosefu wa vifaa kwa ajili ya kufanyia mazoezi.
Fabiola
 na wadau wengine wamemwomba Naibu Waziri pamoja na wadau wengine 
kushirikiana kwa pamoja ili kuanzisha klabu za michezo ya riadha ili 
kuibua vipaji vya wakimbiaji waliopo maeneo ya vijijini.
Alisema
 mkoa huo una wanamichezo wengi, lakini hakuna klabu za michezo hali 
inayosababisha baadhi ya wanariadha kufanya mazoezi bila ya kuwa na 
vifaa maalumu, lakini walimpongeza Nyalandu kwa kuanzisha mashindano 
hayo maeneo ya vijijini ili kuibua wanamichezo wengi watakaoweza 
kuutangaza mkoa huo pamoja na Tanzania kwa ujumla pale yanapotokea 
mashindano ya riadha ya ndani na nje ya nchi.
Chanzo;Habari Leo 
0 comments:
Post a Comment