Home » » Walimu mbaroni wizi wa mitihani

Walimu mbaroni wizi wa mitihani

Shukuru Kawambwa
 
Jeshi  la Polisi mkoani Singida linawashikilia walimu wawili wa shule ya sekondari, katika Tarafa ya Kirumi, Wilaya ya Mkalama, kwa kujihusisha na wizi wa mitihani ya kidato cha nne inayoendelea nchini kote.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Geofrey Kamwela, alisema tukio hilo lilitokea kati ya saa 3:00 na saa 3:30 juzi, katika Shule ya Sekondari Nkinto, iliyopo Tarafa ya Kirumi, wilayani humo.

Alisema walimu hao wanashikiliwa kwa tuhuma za udanganyifu wa mitihani hiyo iliyohusisha masomo ya Kiswahili na Fizikia.

Aliwataja walimu wanaoshikiliwa kuwa ni Mkuu wa Shule ya Nkinto, Monica Sebastian (30), na Agaloslo Otieno (32), ambao wote ni walimu wa shule hiyo.

Alisema mwalimu Otieno alikuwa msimamizi wa  mitihani kwenye Shule ya Sekondari ya Mwangeza, lakini alitumia simu yake ya kiganjani kuandika maswali na kumtumia mwalimu wake mkuu aliyemwacha katika kituo chake cha kazi (Nkinto).

Kamwela alisema baada ya Mwalimu Monica kupokea maswali hayo, alianza kuyapatia majibu kisha anapiga kambi kwenye moja ya choo cha shule yake.

Alisema baadhi ya wanafunzi waliomba ruhusa kwa wasimamizi kwenda kujisaidia chooni na kwamba, walipokuwa wakifika walipewa majibu sahihi ya somo husika.

Kamwela alisema polisi walipata taarifa hizo kutoka kwa raia wema na kuandaa mtego, ambao ulimnasa Monica.
Alisema simu yake ilipochunguzwa, ilionekana kuwa na maswali hayo yaliyotumwa kutoka katika simu ya Mwalimu Otieno, aliyekuwa msimamizi wa mitihani kwenye shule nyingine.

Kutokana na hali hiyo, Kamwela alisema walimu hao watapandishwa kizimbani wakati wowote baada ya upelelezi kukamilika.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa