JESHI la Polisi mkoani Singida limewaua kwa kuwapiga  risasi 
majambazi wawili waliokuwa wakijiandaa kufanya uhalifu katika Kijiji cha
  Manga nje kidogo ya mji wa Singida.
  Kamanda wa Polisi mkoani Singida, Godfrey Kamwela  alisema tukio hilo 
limetokea juzi, saa 12:00 jioni baada ya polisi kupata  taarifa za siri 
kutoka kwa raia wema.
  Kamwela alisema majambazi hayo yalikuwa na bunduki moja  aina ya SMG 
yenye namba 34555 ikiwa na risasi saba kwenye magazine, huku wakitumia  
pikipiki T 634 BTW Sanlg.
  Aidha, Kamanda Kamwela alisema askari polisi walifika  katika eneo 
hilo, na watu hao walistuka kwa kuwa wanafuatiliwa na askari na  hivyo 
kuanza kukimbia kuelekea Kijiji cha Uhamaka kwa kutumia pikipiki hiyo.
  Hata hivyo, alisema walipoona polisi wanawakaribia  waliitelekeza 
pikipiki hiyo na kuanza kukimbia porini kwa miguu, lakini hali  
ilipokuwa ngumu zaidi walianza kuwarushia polisi risasi, hivyo polisi 
nao  walilazimika kujibu.
  “Majibizano hayo ya risasi yalipelekea majambazi wawili  kujeruhiwa 
huku mmoja akifanikiwa kukimbia. Majeruhi hao walifariki dunia  wakati 
wakikimbizwa hospitali ya mkoa kwa matibabu. Maiti zimehifadhiwa  
hospitalini hapo kwa ajili ya kutambuliwa na ndugu zao,” alisema 
Kamwela.
  Alisema kwenye eneo la tukio ilipatikana bunduki moja  aina ya SMG 
ikiwa na risasi saba na pikipiki iliyokuwa wakiitumia kukimbia.  Polisi 
wanaendelea na uchunguzi   ili  kubaini kama kuna mtandao wa majambazi 
pamoja na kumsaka mtuhumiwa aliyekimbia.
  Wakati huohuo, polisi mkoani hapa inawashikilia watu  wanne akiwemo 
mhudumu wa nyumba ya kulala wageni ya Lake Hill Singida Motel  kuhusiana
 na tukio la ujambazi lililotokea kwenye hoteli hiyo.
  Kamanda Kamwela alisema wizi huo ulitokea juzi, saa  9:30 usiku, 
ambapo watu ambao idadi bado haijajulikana wakiwa na bunduki  walivamia 
hoteli hiyo na kuwapora wapangaji vitu mbalimbali.
  Alisema watu hao walipofika katika hoteli hiyo  walifyatua risasi 
hewani kwa lengo la kuwatisha wapangaji na walinzi na  kufanikiwa 
kuwafunga kamba walinzi wote watatu na kuingia katika vyumba viwili  na 
kuwanyang’anya wapangaji mali pamoja na fedha.
  Aliwataja wanaoshikiliwa kwa tuhuma hizo ni walinzi hao  wa kampuni 
binafsi ya ulinzi ya Mass Security ya mjini Singida ambao ni Juma  
Mwangwi (35), Zakaria Pastory (23) na Donald Samson (19) na Mhudumu wa 
hoteli  hiyo, Alistides Salvatory  (24).
  Kamanda Kamwela alitaja vitu vilivyoporwa kuwa ni  kompyuta mpakato 
moja, simu tatu za mkononi zenye thamani ya sh milioni moja,  saa mbili 
za mkononi moja yenye thamani ya dola 500 za Marekani  pamoja na fedha 
taslimu sh 800,000 na dola  500
Chanzo;Tanzania Daima 
0 comments:
Post a Comment