Home » » Polisi yaua majambazi wawili

Polisi yaua majambazi wawili

JESHI la Polisi mkoani Singida limewaua kwa kuwapiga risasi majambazi wawili waliokuwa wakijiandaa kufanya uhalifu katika Kijiji cha Manga nje kidogo ya mji wa Singida.
Kamanda wa Polisi mkoani Singida, Godfrey Kamwela alisema tukio hilo limetokea juzi, saa 12:00 jioni baada ya polisi kupata taarifa za siri kutoka kwa raia wema.
Kamwela alisema majambazi hayo yalikuwa na bunduki moja aina ya SMG yenye namba 34555 ikiwa na risasi saba kwenye magazine, huku wakitumia pikipiki T 634 BTW Sanlg.
Aidha, Kamanda Kamwela alisema askari polisi walifika katika eneo hilo, na watu hao walistuka kwa kuwa wanafuatiliwa na askari na hivyo kuanza kukimbia kuelekea Kijiji cha Uhamaka kwa kutumia pikipiki hiyo.
Hata hivyo, alisema walipoona polisi wanawakaribia waliitelekeza pikipiki hiyo na kuanza kukimbia porini kwa miguu, lakini hali ilipokuwa ngumu zaidi walianza kuwarushia polisi risasi, hivyo polisi nao walilazimika kujibu.
“Majibizano hayo ya risasi yalipelekea majambazi wawili kujeruhiwa huku mmoja akifanikiwa kukimbia. Majeruhi hao walifariki dunia wakati wakikimbizwa hospitali ya mkoa kwa matibabu. Maiti zimehifadhiwa hospitalini hapo kwa ajili ya kutambuliwa na ndugu zao,” alisema Kamwela.
Alisema kwenye eneo la tukio ilipatikana bunduki moja aina ya SMG ikiwa na risasi saba na pikipiki iliyokuwa wakiitumia kukimbia. Polisi wanaendelea na uchunguzi   ili kubaini kama kuna mtandao wa majambazi pamoja na kumsaka mtuhumiwa aliyekimbia.
Wakati huohuo, polisi mkoani hapa inawashikilia watu wanne akiwemo mhudumu wa nyumba ya kulala wageni ya Lake Hill Singida Motel kuhusiana na tukio la ujambazi lililotokea kwenye hoteli hiyo.
Kamanda Kamwela alisema wizi huo ulitokea juzi, saa 9:30 usiku, ambapo watu ambao idadi bado haijajulikana wakiwa na bunduki walivamia hoteli hiyo na kuwapora wapangaji vitu mbalimbali.
Alisema watu hao walipofika katika hoteli hiyo walifyatua risasi hewani kwa lengo la kuwatisha wapangaji na walinzi na kufanikiwa kuwafunga kamba walinzi wote watatu na kuingia katika vyumba viwili na kuwanyang’anya wapangaji mali pamoja na fedha.
Aliwataja wanaoshikiliwa kwa tuhuma hizo ni walinzi hao wa kampuni binafsi ya ulinzi ya Mass Security ya mjini Singida ambao ni Juma Mwangwi (35), Zakaria Pastory (23) na Donald Samson (19) na Mhudumu wa hoteli hiyo, Alistides Salvatory  (24).
Kamanda Kamwela alitaja vitu vilivyoporwa kuwa ni kompyuta mpakato moja, simu tatu za mkononi zenye thamani ya sh milioni moja, saa mbili za mkononi moja yenye thamani ya dola 500 za Marekani  pamoja na fedha taslimu sh 800,000 na dola 500
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa