Home » » Wajasiriamali waelezwa umuhimu wa soko la hisa

Wajasiriamali waelezwa umuhimu wa soko la hisa

MKUU wa Mkoa wa Singida, Dk. Parseko KoneMKUU wa Mkoa wa Singida, Dk. Parseko Kone, ameelezea umuhimu wa soko la hisa katika upatikanaji wa mitaji ya muda mrefu na uwekezaji kuwa haviwezi kuletwa na masoko ya mitaji pekee.
Kwa mujibu wa mkuu huyo, dhima ya kupata rasilimali na kuzitumia kikamilifu kwenye miradi yenye tija, husababisha ukuaji wa uchumi na kuongeza utajiri.
Dk. Kone amebainisha hayo juzi mjini Singida wakati akifungua semina ya siku mbili kwa wafanyabiashara na wajasiriamali juu ya soko la kukuza ujasiriamali (EGM) iliyofanyika kwenye ukumbi wa Aque Vitae.
Alisema ni muhimu ieleweke wazi kwamba kuna uhusiano wa moja kwa moja baina ya mafanikio ya masoko ya mitaji na uchumi wa nchi na kusisitiza kwamba moja ya sababu ni serikali kuanzisha na kusaidia maendeleo ya Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE).
Aidha, alibanisha kwamba kampeni hiyo imekuja wakati muafaka ambao serikali imepania kujenga sekta binafsi imara itakayokuwa injini ya uchumi wa taifa.
“Napenda kuchukua fursa hii kuwahakikishia kwamba serikali inatambua mchango wa wadau mbalimbali katika maendeleo ya masoko ya hisa hapa nchini, mwamko kama huu unalenga kujenga uelewa kwa sekta binafsi na umma juu ya fursa zipatikanazo na soko la hisa zinaungwa mkono na serikali.
“Pia nitumie fursa hii kuwataka wadau na wahusika wote kwa ukamilifu wenu kutumia tukio hili ili kutumia fursa zipatikanazo kwenye soko la hisa,” alisema Dk. Kone.
Hata hivyo Dk. Kone alisema tafiti nyingi zimeonyesha kwamba upatikanaji wa mitaji ya wajasiriamali wadogo na wa kati ni changamoto kwa maendeleo ya kukua kwa shughuli za ujasiriamali na sekta hiyo kwa ujumla.
Awali Meneja Uhusiano wa kitaasisi kutoka DSE, Mary Mniwasa, alimweleza mkuu wa mkoa kuwa lengo la semina hiyo ni kampeni ya umma ya kupunguza umaskini hapa nchini.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TCCIA Mkoa wa Singida, Francis Mashuda, alisema wafanyabiashara wanakumbana na changamoto kubwa ya ukosefu wa mitaji.
Semina hiyo ilitarajiwa kuhudhuriwa na wafanyabiashara wa kada mbalimbali na wajasiriamali wasiopungua 65, imefadhiliwa na DSE chini ya uratibu wa TCCIA Mkoa wa Singida.
Chanzo;Tanzania Daimma

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa