Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
            

 
MBUNGE wa Singida 
Mashariki, Bw. Tundu Lissu (CHADEMA), amedai Serikali imekuwa ikitoa 
taarifa za uongo kwa wananchi juu ya mgawanyo wa madawati katika 
halmashauri mbalimbali nchini yaliyotokana na fedha zilizozidi kununulia
 rada 'chenchi ya rada'.
Bw. Lissu aliyasema 
hayo bungeni Mjini Dodoma jana wakati akichangia Bajeti ya Serikali Kuu 
kwa mwaka wa fedha 2014/15. Alisema katika hotuba ya Waziri Mkuu, 
jedwali la mgawanyo wa madawati lilionesha Serikali iligawa madawati 
93,740 lakini Naibu Waziri alidai madawati hayo hayajatolewa yote.
Alisema katika jedwali 
hilo, lilionyesha kulikuwa na mgawo wa madawati hewa 3,048 kwenye Mkoa 
wa Singida ikifafanua kila halmashauri ilipewa madawati 508 wakati 
hakuna dawati hata moja hivyo ni wazi kuwa wananchi wamedanganywa na 
Serikali yao.
Naye Mbunge wa Tumbe, 
Bw. Rashid Ally Abdallah (CUF), alisema Bajeti ya Serikali Kuu kwa mwaka
 2014/15, haiendani na hali halisi ya maisha ya wananchi kwani haiwezi 
kutekelezeka.
Alisema kasi ya ukuaji 
uchumi haiendani na mahitaji ya wananchi kutokana na matumizi makubwa 
kuliko mapato kama ilivyotokea katika Bajeti ya 2013/14 ambapo Wizara ya
 Fedha imeshindwa kutekeleza sera mbalimbali za Serikali.
"Ipo haja ya kujua 
tatizo ni nini, Wizara mbalimbali hazipewi fedha wanazoomba kwa ajili ya
 kutekeleza mipango mbalimbali... baadhi ya wabunge walishauri vyanzo 
vipya vya mapato, mimi naona ushauri huu ni kazi bure kama Serikali 
inakosa fedha," alisema.
Aliongeza kuwa, 
Serikali haina nidhamu ya matumizi ya fedha kutokana na vitendo vya 
rushwa, ufisadi ambavyo ni janga la kitaifa kwenye sekta mbalimbali 
ikiwemo ya ujenzi wa miundombinu na utoaji tenda.
"Ripoti ya Mdhibiti na 
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), imeeleza wizi mkubwa wa fedha 
katika halmashauri... kama wananchi wanalipa kodi na fedha zinafujwa 
kwanini tuendelee kuishauri Serikali kuwa na vyanzo vipya vya mapato," 
alihoji Bw. Abdallah.
Alionesha wasiwasi wake
 juu ya ziara za viongozi kutumia fedha nyingi ikihoji sera ya Wizara ya
 Mambo ya Nje kutokana na msafara wa Rais kuwa na watu wengi pamoja na 
matumizi ya vyombo vya usafiri hivyo alishauri jambo hilo liangaliwe.
"Lazima Wizara iweke 
utaratibu kuhusu safari za viongozi vinginevyo kila siku watakuwa 
wakitumia zaidi ya bilioni 50...ifahamike watu ambao wanaongozana na 
Rais wanakwenda kwa lengo gani," alisema.
Mbunge wa Kisesa, Bw. 
Luhaga Mpina (CCM), aliishukia Kamati ya Bajeti kuendelea na vikao vyake
 nje ya Bunge wakati wabunge wakijadili Bajeti ya Serikali Kuu.
Alisema lipo tatizo 
kubwa la kushuka kwa thamani ya shilingi ya Tanzania hivyo ni vyema 
Serikali ikatoa majibu na kufafanua juu ya hatua zilizochukuliwa hadi 
sasa.
 
 
 
0 comments:
Post a Comment