Home » » LISSU AISHUKIA SERIKALI BUNGENI

LISSU AISHUKIA SERIKALI BUNGENI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

MBUNGE wa Singida Mashariki, Bw. Tundu Lissu (CHADEMA), amedai Serikali imekuwa ikitoa taarifa za uongo kwa wananchi juu ya mgawanyo wa madawati katika halmashauri mbalimbali nchini yaliyotokana na fedha zilizozidi kununulia rada 'chenchi ya rada'.

Bw. Lissu aliyasema hayo bungeni Mjini Dodoma jana wakati akichangia Bajeti ya Serikali Kuu kwa mwaka wa fedha 2014/15. Alisema katika hotuba ya Waziri Mkuu, jedwali la mgawanyo wa madawati lilionesha Serikali iligawa madawati 93,740 lakini Naibu Waziri alidai madawati hayo hayajatolewa yote.

Alisema katika jedwali hilo, lilionyesha kulikuwa na mgawo wa madawati hewa 3,048 kwenye Mkoa wa Singida ikifafanua kila halmashauri ilipewa madawati 508 wakati hakuna dawati hata moja hivyo ni wazi kuwa wananchi wamedanganywa na Serikali yao.

Naye Mbunge wa Tumbe, Bw. Rashid Ally Abdallah (CUF), alisema Bajeti ya Serikali Kuu kwa mwaka 2014/15, haiendani na hali halisi ya maisha ya wananchi kwani haiwezi kutekelezeka.

Alisema kasi ya ukuaji uchumi haiendani na mahitaji ya wananchi kutokana na matumizi makubwa kuliko mapato kama ilivyotokea katika Bajeti ya 2013/14 ambapo Wizara ya Fedha imeshindwa kutekeleza sera mbalimbali za Serikali.

"Ipo haja ya kujua tatizo ni nini, Wizara mbalimbali hazipewi fedha wanazoomba kwa ajili ya kutekeleza mipango mbalimbali... baadhi ya wabunge walishauri vyanzo vipya vya mapato, mimi naona ushauri huu ni kazi bure kama Serikali inakosa fedha," alisema.

Aliongeza kuwa, Serikali haina nidhamu ya matumizi ya fedha kutokana na vitendo vya rushwa, ufisadi ambavyo ni janga la kitaifa kwenye sekta mbalimbali ikiwemo ya ujenzi wa miundombinu na utoaji tenda.

"Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), imeeleza wizi mkubwa wa fedha katika halmashauri... kama wananchi wanalipa kodi na fedha zinafujwa kwanini tuendelee kuishauri Serikali kuwa na vyanzo vipya vya mapato," alihoji Bw. Abdallah.

Alionesha wasiwasi wake juu ya ziara za viongozi kutumia fedha nyingi ikihoji sera ya Wizara ya Mambo ya Nje kutokana na msafara wa Rais kuwa na watu wengi pamoja na matumizi ya vyombo vya usafiri hivyo alishauri jambo hilo liangaliwe.

"Lazima Wizara iweke utaratibu kuhusu safari za viongozi vinginevyo kila siku watakuwa wakitumia zaidi ya bilioni 50...ifahamike watu ambao wanaongozana na Rais wanakwenda kwa lengo gani," alisema.

Mbunge wa Kisesa, Bw. Luhaga Mpina (CCM), aliishukia Kamati ya Bajeti kuendelea na vikao vyake nje ya Bunge wakati wabunge wakijadili Bajeti ya Serikali Kuu.

Alisema lipo tatizo kubwa la kushuka kwa thamani ya shilingi ya Tanzania hivyo ni vyema Serikali ikatoa majibu na kufafanua juu ya hatua zilizochukuliwa hadi sasa.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa