Home » » Maadhimisho kupinga ukeketaji kufanyika Singida

Maadhimisho kupinga ukeketaji kufanyika Singida

KUKITHIRI kwa vitendo vya ukeketaji kwa watoto wachanga katika Mkoa wa Singida, kumefanya maadhimisho ya kupinga vitendo hivyo kwa mwaka huu kufanyika mkoani humo ili kutoa elimu kwa wananchi.
Kaimu Mkurugenzi wa Kituo cha Haki za Binadamu (LHRC), Imelda Urio,  alitoa kauli hiyo jijini Dae es Salaam jana kwa niaba ya Mtandao wa Kupinga Ukeketaji unaojumuisha jumla ya mashirika 12.
Urio alisema maadhimisho hayo yanayotarajiwa kufanyika Februari 6, wanaamini wataweza kufikisha elimu  ya kupinga vitendo hivyo ambavyo vina athari kwa watoto na wanawake.
Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, mtandao ulishajaribu kupambana na vitendo hivyo kwa kuwakagua watoto pindi wanapopelekwa kiliniki, lakini zoezi hilo lilishindikana kutokana na kina mama kuacha kuwapeleka watoto, hivyo kuwanyima haki ya kupata chanjo nyingine zitakazosaidia kulinda afya zao.
Alitaja athari zinazotokana na ukeketaji kuwa ni fistula, kupata shida wakati wa kujifungua, kupata maumivu wakati wa tendo la ndoa na kupata athari za kisaikolojia.
Hata hivyo, kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2012 mikoa inayoongoza kwa vitendo hivyo na asilimia kwenye mabano ni  Manyara (71), Arusha (55) na Mara (40).
Kutokana na hali hiyo, waliitaka serikali kuonyesha utashi wa kisiasa kwa kutekeleza sera na mpango wa kitaifa wa kupinga na kutokomeza ukeketaji kwa kufuatilia utendaji wake ili kutokomeza mila kandamizi.
Kwa upande wa asasi, Urio alitaka ziendelee kupiga kampeni za ushawishi na inapobidi kupitia tena mikakati ili kuleta matukio mazuri na ya kudumu.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa