KUKITHIRI kwa vitendo  vya ukeketaji kwa watoto wachanga katika Mkoa
 wa Singida, kumefanya maadhimisho  ya kupinga vitendo hivyo kwa mwaka 
huu kufanyika mkoani humo ili kutoa elimu  kwa wananchi.
  Kaimu Mkurugenzi wa  Kituo cha Haki za Binadamu (LHRC), Imelda Urio,  
 alitoa kauli hiyo jijini Dae es Salaam jana kwa niaba ya Mtandao wa  
Kupinga Ukeketaji unaojumuisha jumla ya mashirika 12.
  Urio alisema  maadhimisho hayo yanayotarajiwa kufanyika Februari 6, 
wanaamini wataweza  kufikisha elimu  ya kupinga vitendo hivyo  ambavyo 
vina athari kwa watoto na wanawake.
  Kwa mujibu wa mkurugenzi  huyo, mtandao ulishajaribu kupambana na 
vitendo hivyo kwa kuwakagua watoto  pindi wanapopelekwa kiliniki, lakini
 zoezi hilo lilishindikana kutokana na kina  mama kuacha kuwapeleka 
watoto, hivyo kuwanyima haki ya kupata chanjo nyingine  zitakazosaidia 
kulinda afya zao.
  Alitaja athari  zinazotokana na ukeketaji kuwa ni fistula, kupata 
shida wakati wa kujifungua,  kupata maumivu wakati wa tendo la ndoa na 
kupata athari za kisaikolojia.
  Hata hivyo, kwa mujibu  wa takwimu za mwaka 2012 mikoa inayoongoza kwa
 vitendo hivyo na asilimia kwenye  mabano ni  Manyara (71), Arusha (55) 
na  Mara (40).
  Kutokana na hali hiyo,  waliitaka serikali kuonyesha utashi wa kisiasa
 kwa kutekeleza sera na mpango wa  kitaifa wa kupinga na kutokomeza 
ukeketaji kwa kufuatilia utendaji wake ili  kutokomeza mila kandamizi.
  Kwa upande wa asasi,  Urio alitaka ziendelee kupiga kampeni za 
ushawishi na inapobidi kupitia tena  mikakati ili kuleta matukio mazuri 
na ya kudumu.
Chanzo;Tanzania Daima 
0 comments:
Post a Comment