Home » » Mt. Gaspari yatibu wagonjwa 53,000

Mt. Gaspari yatibu wagonjwa 53,000

Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspari ZAIDI ya wagonjwa 53,000 walipatiwa huduma za matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Gaspari iliyopo katika mji mdogo wa Itigi, wilayani Manyoni, Singida kwa kuanzia mwaka 2006 hadi mwaka jana.
Mkurugenzi wa hospitali hiyo, Padre Seraphine Lesiriam, alisema hayo kwenye risala aliyosoma kwa mgeni rasmi Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Kardinali Polycarp Pengo wakati wa ufunguzi wa kliniki ya upasuaji wa watoto hospitalini hapo.
Padre Seraphine alifafanua kwamba katika kipindi cha kuanzia mwaka 2006 hadi 2012 watoto waliohitaji huduma za upasuaji hususani wa moyo hupelekwa katika Hospitali ya Bambino Gesu iliyopo Italia.
Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, kipindi hicho jumla ya watoto 13 wamenufaika na huduma za upasuaji, kati yao 12 walifanyiwa upasuaji wa moyo na mmoja alifanyiwa ‘plastic surgery’.
Hata hivyo aliweka wazi kwamba mwaka jana jumla ya wagonjwa wa nje 9,450 wenye chini ya miaka mitano walihudumiwa wakati wagonjwa wengine wa nje 36,353 wenye zaidi ya miaka mitano walihudumiwa hospitalini hapo.
Kuhusu wagonjwa waliolazwa, alisema kwa kipindi cha mwaka uliopita jumla ya wagonjwa 8,133 ambao kati yao watoto ni 3,711 walilazwa hospitalini hapo.
Padre Lesiriam alibainisha kwamba uwepo wa huduma za upasuaji kwa watoto na tiba nyingine katika hospitali hiyo ni tunda la moyo wa ukarimu na ushirikiano kati ya hospitali ya Bambino Gesu na Shirika la Wamishenari wa Damu Azizi.
Akifafanua zaidi, mkurugenzi huyo alisisitiza kwamba hospitali ya Bambino Gesu imechangia euro 250,000 sawa na zaidi ya sh 525,000,000 ili kuanzisha huduma za upasuaji kwenye kliniki ya watoto.
“Fedha hizo zimetumika kwenye ununuzi wa vifaa na kufanya marekebisho kwenye mojawapo ya majengo katika idara ya watoto ili kuanzisha huduma hizi za upasuaji,” alisisitiza padre huyo.
Rais wa hospitali ya Bambino Gesu, Profesa Giuseppe Profiti, akinukuu maandiko matakatifu alisema: “Msifanye mambo mema kwa ajili yetu tu bali mnapaswa kufanya mambo mema kwa ajili ya wengine pia.”
Hata hivyo, aliweka bayana kwamba wao wanapenda kushirikiana nao na watafanya kila kitu ambacho wataweza kukifanya, hivyo alitumia fursa hiyo kuomba msaada kwa watendaji wa hospitali hiyo ili wafanikishe malengo yao.
Akifungua kliniki hiyo, Kardinali Pengo alitumia fursa hiyo kuwaasa viongozi wa vyama vya siasa na serikali kutoingilia na kuharibu ufanisi wa huduma zinazotolewa na wafadhili kwa Watanzania ambao kwa namna moja au nyingine hawana uwezo  wa kuzilipia.
Alifafanua kuwa huduma zinazoanzishwa kwa faida ya watu wasiokuwa na uwezo, hususani watoto, zinatakiwa zisiingiliwe na baadhi ya watu ambao wanataka kwa manufaa yao.
Awali Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Hassani Liana, alisema serikali inatambua ushirikiano unaofanywa na watu binafsi na mashirika ya dini hasa kwenye afya na elimu hapa nchini.
Chanzo;Tanzania Daima 
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa