Home » » Kisima chagharimu Sh22 milioni

Kisima chagharimu Sh22 milioni


Gasper Andrew, Singida  
MBUNGE wa Jimbo la Singida mjini, Mohammed Gullam Dewji, ametumia zaidi ya Sh 22 milioni, kugharamia uchimbaji wa kisima kirefu cha maji cha kitongoji cha Mtisi, kata ya Mtamaa. 
  
Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa kisima alisema, fedha hizo zimetumika pamoja na mambo mengine,kufanyia  utafiti wa eneo lenye maji,uchimbaji  na ununuzi wa pampu ya mkono. 
  
“Hapa naomba niweke mambo wazi, gharama hii inajumuisha pia uchimbaji wa kisima ambacho kwa bahati mbaya baada ya uchimbaji kina kirefu sana, kikawa hakina maji.  Pamoja na kukosekana huko kwa maji, lakini fedha nyingi  ilitumika”,alifafanua. 
  
Dewji alisema, ameamua kutumia fedha zake binafsi kugharamia uchimbaji huo wa kisima, kwa lengo la kuwapatia maji safi na salama wakazi wa kata ya Mtamaa. 
  
“Mimi binafsi naamini kwamba maji safi na salama, yatasaidia kuondoa uwezekano wa kutokea kwa magonjwa ya mlipuko ikiwamo, ugonjwa wa kuharisha”,alisema. 
  
Aidha, mbunge huyo aliwataka wakazi wa kijiji cha Mtamaa na vijiji jirani, kukitunza kisima hicho ili kiweze kutoa huduma endelevu. 
  
Dewji alisema kazi ya uchimbaji wa  visima, ni ya gharama kubwa mno, hivyo ni muhimu kisima hicho kikatuzwa  vizuri na kila mkazi wa eneo hilo, awe mlinzi ili kisiharibiwe. 
  
Awali diwani wa kata ya Mtamaa (CCM), Mbua Chima, alitumia fursa hiyo kumshukuru mbunge huyo kwa msaada wa kuwachimbia kisima wakazi wa kata hiyo.
Chanzo: Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa