Home » » DC AHIMIZA UJENZI WA MAABARA

DC AHIMIZA UJENZI WA MAABARA

Na Nathaniel Limu, Singida

SERIKALI ya Wilaya ya Singida, imewaagiza wakazi wa Manispaa ya Singida, kuunganisha nguvu zao pamoja kuchangia ujenzi wa maabara katika shule zote za sekondari za kata.

Kasi na nguvu zilizotumika kujenga shule za sekondari za kata, ziongezeke zaidi ili ifikapo Oktoba 20, mwaka huu, majengo ya maabara yawe yamefikia hatua nzuri ya kupauliwa.

Agizo hilo, limetolewa juzi na Mkuu wa Wilaya ya Singida, Queen Mlozi, wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Utemini.

Alisema, suala la ujenzi wa maabara ni muhimu, wakati huu wa dunia ya sayansi na teknolojia.

Alisema wazazi na walezi, lazima watambue hilo, ili waweze kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa maabara mahali watoto wao, watajifunza kwa vitendo masuala ya sayansi.

“Tuanze na majengo kwanza, mambo mengine kama ya vifaa na huduma ya umeme, hayo yatafuata baadaye,” alisema mkuu huyo wa wilaya.

Alisema jengo la maabara, likiwepo ni rahisi mno kupatiwa vifaa au msaada wa kuunganishiwa umeme.

Alisema kata zitakazowahi kuanza ujenzi wa maabara na kufikia hatua nzuri ya kupaua kabla ya Oktoba 20, mwaka huu, ataziunga mkono kwa kuzisaidia fedha.

“Kwa hapa kwenu Utemini, nyie andaeni tu siku ya kufanya harambee ya kuchangia ujenzi wa maabara, mimi nawaahidi nitakuja pamoja na wadau wa maendeleo, ili kwa pamoja tuje tuwaunge mkono,” alisema Mlozi.

Kuhusu ombi la kuipatia shule hiyo umeme na barabara bora, aliahidi kulifanyia kazi mapema iwezekanavyo.

DC Mlozi, yupo kwenye ziara ya kujitambulisha kwa wakazi wa Manispaa ya Singida, kuhimiza ujenzi wa maabara na ujenzi wa vyumba vya madarasa, kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha kwanza mwakani.

Halmashauri ya Manispaa ya Singida, ina jumla ya shule za sekondari 17, zikiwemo za Serikali na tatu za madhehebu ya dini na watu binafsi. Kati ya shule hizo, tatu tu ndizo zenye maabara.
Chanzo: Mtanzania

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa