Home » » DIWANI; WATENDAJI WANAOKULA FEDHA WACHAPWE VIBOKO

DIWANI; WATENDAJI WANAOKULA FEDHA WACHAPWE VIBOKO

DIWANI wa Rungwa, Tarafa ya Itigi, wilayani Manyoni, Singida, Edward Machapaa, amependekeza adhabu ya kuchapwa viboko itolewe kwa watendaji wanaokula fedha za wananchi zilizotolewa na serikali kwa ajili ya kukamilisha miradi mbalimbali ya maendeleo.
Machapaa alitoa pendekezo hilo kwenye mkutano maalumu wa Baraza la Madiwani wa halmashauri ya wilaya hiyo uliofanyika mjini Manyoni alipokuwa akijadili hoja ya matumizi mabaya ya fedha za miradi ya maendeleo.
Alisema kumekuwepo malalamiko mengi na ya mara kwa mara juu ya fedha za miradi kutumika vibaya au hata kwa baadhi ya watendaji kula fedha hizo, hivyo umefika wakati wa kubadili mbinu ya kutoa adhabu kwa kutoa adhabu ya viboko.
“Ndugu mkurugenzi, kwa hili hapa inatakiwa tutafute dawa, huyu mtu anayekula hela kama ni mtendaji kwanini asichapwe bakora 12, ili akamuonyeshe mkewe?” alisisitiza Machapaa na kusababisha madiwani wenzake pamoja na wakuu wa idara kuangua kicheko.
Diwani huyo alitumia fursa hiyo kuwashawishi madiwani wenzake kubadilika na kuonya kwamba endapo hawatabadilika serikali itaendelea kutuma wakaguzi na adhabu ya kuwakata mishahara itaendelea kuwepo mwaka hadi mwaka.
Pia alipendekeza watendaji hao wafukuzwe hata watatu kwa kuanzia na huenda wengine wakaogopa baada kuona adhabu hiyo.
Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Supeet Mseya, alisema katika kipindi cha mwaka 2013/2014 halmashauri hiyo ilipata mafanikio mengi na kuyataja baadhi kuwa ni kuendelea kupata hati safi ya ukaguzi wa matumizi ya fedha na halmashauri kuendelea kupata ruzuku ya CDG.
Mafanikio mengine ni kuboreshwa kwa huduma za afya kwa asilimia 95 kwa kutoa kinga na tiba kwa ajili ya magonjwa mbalimbali, uendelezaji wa ujenzi wa vituo vitatu vya afya katika kata za Makuru, Mitundu na Itigi, ujenzi wa zahanati tatu katika vijiji vya Ntope, Igwamadete Rungwa, na ukamilishaji wa hosteli nne katika shule za Itigi, Makuru, Rungwa na Sanza.
 Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa