Home » » Singida yatenga bajeti bil. 31/-

Singida yatenga bajeti bil. 31/-

HALMASHAURI ya Manispaa ya Singida, inatarajia kutumia sh bilioni 31.7 katika bajeti yake ya mwaka wa fedha wa 2014/2015.
Kaimu Mkurugenzi wa manispaa hiyo, Deus Luziga, alibainsha hayo alipokuwa akitoa mapendekezo ya bajeti ya mwaka ujao wa fedha mbele ya kikao maalumu cha bajeti cha Baraza la Madiwani kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa manispaa hiyo.
Alisema kwa mwaka wa fedha wa 2014/2015 Halmashauri ya Manispaa ya Singida imeandaa bajeti yake kwa kuzingatia mwongozo wa bajeti wa taifa, sera ya taifa ya kuondoa umasikini.
Alisema kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 15.287 ni mishahara ya watumishi, ruzuku ya serikali kuu kwa matumizi mengineyo sh bilioni 1.860, sh bilioni 11.621 ni ruzuku ya miradi ya maendeleo wakati sh bilioni 2.986 ni mapato ya ndani.
Alisema wanatarajia serikali kuu itawapatia ruzuku ya sh milioni 181 kwa ajili ya kufidia ushuru na kodi iliyofutwa.
Kaimu mkurugenzi huyo alisema bajeti ya Manispaa ya Singida imeongezeka kwa sh bilioni 13 ambayo ni sawa na aslimia 43 ya lengo la kukusanya zaidi ya sh bilioni 18.1 katika bajeti ya mwaka wa fedha wa 2013/2014.
“Ongezeko hili limechangiwa pamoja na kuongezeka kwa ajira mpya na nyongeza za mishahara na kuongezeka kwa miradi ya maji ambayo maelekezo yake ni kutekeleza miradi katika vijiji 20,” alifafanua.
Aidha, alisema katika bajeti ya mwaka wa fedha 2013/2014 halmashauri iliidhinishiwa kutumia sh bilioni 18.125 kwa ajili ya kutoa huduma mbalimbali ikiwemo mishahara ya watumishi.
Hata hivyo, alisema mapato ya ndani yameongezeka kutoka sh bilioni 1.928 mwaka 2013/2014 hadi kufikia sh bilioni 2.986 kwa mwaka 2014/2015.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa