Home » » MUUGUZI AISHI CHUMBA CHA KUJIFUNGULI

MUUGUZI AISHI CHUMBA CHA KUJIFUNGULI


HUDUMA za kujifungua kwa wajawazito katika zahanati ya Kata ya Iglansoni, wilayani Ikungi, Singida zimesimama kwa muda usiojulikana kutokana na chumba kilichokuwa kikitumika kwa shughuli hizo kubadilishwa matumizi.
Chumba hicho sasa  kimekuwa nyumba ya kuishi muuguzi mkunga wa zahanati hiyo.
Hatua hiyo imefikiwa na uongozi wa kata hiyo baada ya muuguzi mkunga huyo, Meriani Misai kutokuwa na nyumba ya kuishi baada ya dari la nyumba aliyokuwa akiishi kuanguka na popo kugeuza makazi yao kwa kipindi kirefu sasa.
Ofisa Mtendaji wa Kata ya Iglansoni, Rehema Majii alieleza muuguzi huyo alikuwa akikosa usingizi, hasa wakati mvua zinapoanza kunyesha na hivyo kumfanya kukaa kwenye kiti bila kulala kutokana na nyumba kuvuja.
“Kwa kweli nyumba ya nesi haifai inavuja, kwani mpaka ikafikia siku moja akashinda akiwa amekaa kwenye kiti bila kulala na mvua ikiwa inanyesha…kwa hiyo ilibidi tufanye utaratibu, tumemhamishia zahanati,” alifafanua Majii.
Kwa mujibu wa ofisa mtendaji huyo, kutokana na mtumishi huyo kuhamia kwenye chumba kinachotegemewa kutoa huduma za wajawazito, huduma za aina hiyo zimekuwa hazitolewi kama ilivyokuwa awali.
“Kwahiyo kwa sasa hata zile shughuli za kuhudumia wagonjwa zimekuwa hazitolewi kama zinavyostahili kutokana na mhudumu huyo kuhamia kwenye zahanati hiyo,” alisisitiza ofisa mtendaji huyo.
Kwa upande wake, muuguzi mkunga, Misai, alisema alikuwa akiteseka  kwa kuwa nyumba aliyokuwa akiishi ni mbovu, popo wamegeuza makazi kwa kipindi cha miaka mitatu sasa licha ya kutoa taarifa kwa wakuu wa idara wilayani.
Kwa mujibu wa Misai, wajawazito wanalazimika kutembea umbali wa zaidi ya kilomita 50 kufuata huduma hizo katika zahanati ya Kata ya Muhintiri au mbele zaidi kwenye makao makuu ya Tarafa ya Ihanja.
Akizungumzia malalamiko ya mtumishi huyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi, Magayane Protace, licha ya kukiri jitihada zinazofanywa na idara ya afya, lakini hakusita kutoa suluhisho la awali la mtumishi aliyekuwa akiishi ndani ya nyumba hiyo.
Alisema  wameamua kumsaidia muuguzi mkunga huyo wakati idara inaendelea na jitihada za kulitatua tatizo hilo, alimuagiza Ofisa Mtendaaji wa kata hiyo, Majii, kumtafutia mara moja nyumba ya kupanga  na kwamba halmashauri itamlipia gharama za pango kwa kipindi cha miezi mitatu.
Kaimu Mganga mkuu wa wilaya ya Ikungi, Dk. Henry Mbando alisema kutokana na dharura hiyo wameshafanya tathimini ya zaidi ya sh milioni sita za CHF kwa ajili ya kuifanyia ukarabati nyumba hiyo.
Chanzo;Tanzania daima 

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2011. Singida Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogz za Mikoa