HUDUMA za  kujifungua kwa wajawazito katika zahanati ya Kata ya 
Iglansoni, wilayani  Ikungi, Singida zimesimama kwa muda usiojulikana 
kutokana na chumba kilichokuwa  kikitumika kwa shughuli hizo 
kubadilishwa matumizi.
  Chumba hicho  sasa  kimekuwa nyumba ya kuishi muuguzi  mkunga wa zahanati hiyo.
  Hatua hiyo  imefikiwa na uongozi wa kata hiyo baada ya muuguzi mkunga 
huyo, Meriani Misai  kutokuwa na nyumba ya kuishi baada ya dari la 
nyumba aliyokuwa akiishi kuanguka  na popo kugeuza makazi yao kwa 
kipindi kirefu sasa.
  Ofisa Mtendaji wa  Kata ya Iglansoni, Rehema Majii alieleza muuguzi 
huyo alikuwa akikosa usingizi,  hasa wakati mvua zinapoanza kunyesha na 
hivyo kumfanya kukaa kwenye kiti bila  kulala kutokana na nyumba kuvuja.
  “Kwa kweli nyumba  ya nesi haifai inavuja, kwani mpaka ikafikia siku 
moja akashinda akiwa amekaa  kwenye kiti bila kulala na mvua ikiwa 
inanyesha…kwa hiyo ilibidi tufanye  utaratibu, tumemhamishia zahanati,” 
alifafanua Majii.
  Kwa mujibu wa ofisa  mtendaji huyo, kutokana na mtumishi huyo kuhamia 
kwenye chumba kinachotegemewa  kutoa huduma za wajawazito, huduma za 
aina hiyo zimekuwa hazitolewi kama  ilivyokuwa awali.
  “Kwahiyo kwa sasa  hata zile shughuli za kuhudumia wagonjwa zimekuwa 
hazitolewi kama  zinavyostahili kutokana na mhudumu huyo kuhamia kwenye 
zahanati hiyo,”  alisisitiza ofisa mtendaji huyo.
  Kwa upande wake, muuguzi mkunga, Misai,  alisema alikuwa akiteseka  
kwa kuwa  nyumba aliyokuwa akiishi ni mbovu, popo wamegeuza makazi kwa 
kipindi cha miaka  mitatu sasa licha ya kutoa taarifa kwa wakuu wa idara
 wilayani.
  Kwa mujibu wa  Misai, wajawazito wanalazimika kutembea umbali wa zaidi
 ya kilomita 50 kufuata  huduma hizo katika zahanati ya Kata ya 
Muhintiri au mbele zaidi kwenye makao  makuu ya Tarafa ya Ihanja.
  Akizungumzia  malalamiko ya mtumishi huyo, Mkurugenzi Mtendaji wa 
Halmashauri ya Wilaya ya  Ikungi, Magayane Protace, licha ya kukiri 
jitihada zinazofanywa na idara ya afya,  lakini hakusita kutoa suluhisho
 la awali la mtumishi aliyekuwa akiishi ndani ya  nyumba hiyo.
  Alisema  wameamua kumsaidia muuguzi mkunga huyo wakati  idara 
inaendelea na jitihada za kulitatua tatizo hilo, alimuagiza Ofisa  
Mtendaaji wa kata hiyo, Majii, kumtafutia mara moja nyumba ya kupanga  
na kwamba halmashauri itamlipia gharama za  pango kwa kipindi cha miezi 
mitatu.
  Kaimu Mganga mkuu  wa wilaya ya Ikungi, Dk. Henry Mbando alisema 
kutokana na dharura hiyo  wameshafanya tathimini ya zaidi ya sh milioni 
sita za CHF kwa ajili ya  kuifanyia ukarabati nyumba hiyo.
Chanzo;Tanzania daima  
0 comments:
Post a Comment